Na Ramadhani Kissimba na Farida Ramadhani, WF, Nairobi- Kenya

Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) imeahidi kuendeleza ushirikiano uliopo kati yake na Tanzania kwa kuendelea kufadhili miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba katika kikao kati ya Tanzania na Benki ya Maendeleo Afrika Mashariki, kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, alisema Tanzania ni mojawapo ya nchi zinazofaidika na uwepo wa Benki hiyo, kutokana na uhusiano mzuri uliopo kati ya pande hizo mbili.

Dkt. Mwamba alisema Benki hiyo imekuwa ikifadhili miradi mbalimbali nchini ikiwemo miradi ya taasisi za Serikali kama vile Shirika la Nyumba, benki za biashara kama Benki ya Uwekezaji Tanzania (TIB) na miradi inayotokana na sekta binafsi.


Aidha Dkt. Mwamba alisema sanjari na ufadhili wa miradi ya EADB kwa Tanzania Bara, pia mazungumzo yanaendelea kuhusu miradi mingine kwa upande wa Zanzibar hasa miradi ya ujenzi wa nyumba za bei nafuu.


“Tunaendelea kuzungumza kuhusu miradi mingine, hususan Zanzibar ambapo tumezungumza kuhusu mradi wa ujenzi wa makazi ambao kwa sasa tutaufuatilia kwa karibu ili kuona unafanikiwa”, alisema Dkt. Mwamba.


Dkt. Mwamba aliongeza kuwa Benki hiyo imeonesha nia ya kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kutekeleza miradi ya maendeleo na kwa sasa Tanzania ina asilimia 73 za miradi ambayo inatekelezwa na Benki hiyo.


Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeikaribisha Benki ya EADB kufanya mazungumzo yatakayosaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Maendeleo visiwani humo.


Dkt. Akili aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Shirika la Nyumba Zanzibar (ZHC) inatafuta ufadhili wa kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba takribani 3,000 za bei nafuu, hivyo Zanzibar inaona ni fursa kuitumia Benki hiyo kutekeleza mradi huo.


‘’Kuna Shirika la Nyumba Zanzibar ambalo kwa sasa linaendelea kutafuta wafadhili ili kutekeleza ujenzi wa nyumba za bei nafuu, hivyo tumewaalika Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki ili tuzungumze nao kuhusu utekelezaji wa ujenzi wa nyumba hizo” , alisema Dkt. Akili.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Bi. Viviene Yeda ametoa wito kwa Tanzania na nchi nyingine za Afrika Mashariki kuchangamkia fursa zinazopatikana katika Benki hiyo kutokana na uwiano uliopo katika umiliki wa hisa unatokana na Benki hiyo ambapo Tanzania, Kenya na Uganda zina hisa sawa.


Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) ni mshirika wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Standard Charter Bank ambayo inahudumia nchi wanachama sita (6) ikiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudani Kusini.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Maendeleo Afrika Mashariki, Bi. Vivienne Yeda (hayupo pichani), walipokutana na kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Benki hiyo, kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Dkt. Mwamba anamwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba katika Mikutano hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Maendeleo Afrika Mashariki, Bi. Vivienne Yeda akizungumza na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba (hayupo pichani) walipokutana na kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Benki hiyo, kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Dkt. Mwamba anamwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba katika Mikutano hiyo.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na ujumbe wa Tanzania (kushoto) wakisikiliza taarifa za huduma mbalimbali zinazotolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo, Bi. Vivienne Yeda (wa pili kulia), walipokutana na kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Benki hiyo, kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Katika Mikutano hiyo Dkt. Natu anamwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.
Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje kutoka Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Zanzibar, Bw.Yusuf Ibrahim Yussuf (kulia) akifafanua jambo wakati wa kikao kati ya ujumbe wa Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki ulioongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil.
Kamishna Msaidizi wa Fedha za Nje kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Robert Mtengule akizungumza katika kikao kati ya ujumbe wa Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki, ulioongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Katibu Mkuu anamwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba (wa pili kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Maendeleo Afrika Mashariki, Bi. Vivienne Yeda (wa pili kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Shaabani baada ya kikao kati ya ujumbe wa Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki ulioongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, kando ya Mikutano ya Mwaka 2024 ya Bodi ya Magavana (Mawaziri wa Fedha kutoka nchi wanachama) wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Jijini Nairobi nchini Kenya. Dkt. Natu anamwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba katika Mikutano hiyo.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Nairobi - Kenya)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...