NA MWANDISHI WETU ,DAR ES SALAAM .


JUMUIYA ya Wazazi na Watu wanaoishi na hali ya kifafa (UWAKITA),imezindua rasmi kampeni za kuhamasisha uelewa juu ya maradhi ya kifafa, yenye kauli mbiu: "Elimika juu ya kifafa,tokomeza unyanyapaa, pata tiba sahihi."

Tukio hilo limefanyika mapema 9 Mei ,2024 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili , mbele ya Waandishi wa habari, wadau na Madaktari ambapo kwa pamoja wamepinga unyanyapaa kwa watu wenye Kifafa .

Ambapo amebainisha kuwa, Unyanyapaa, ubaguzi na vitendo vya ukatili uliopo ndani ya jamii unachangia kwa kiwango kikubwa na kudhoofisha haki za msingi kwa watu wanaoishi huku wakikabiliana na ugonjwa wa kifafa,

Kwa kauli moja wamepaza sauti kuiomba jamii kuacha vitendo hivyo kwa kutambua kwamba watu wenye ugonjwa huo wana haki sawa na wale wasio nao, hapa duniani.

Mwenyekiti wa UWAKITA, Dkt.Said Kuganda amesema:

“Lengo letu hasa ni kuondoa unyanyapaa dhidi ya hali ya kifafa kwa watu wanaoishi na ugonjwa huo,” amebainisha.

Kuganda ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili Hospitali ya Taifa Muhimbili [MNH] amesema ni kweli hali hii ya kifafa inasumbua ulimwengu mzima na Tanzania.

“Kuna baadhi ya maeneo kwa tafiti zilizofanywa zinaonesha kuna hali ya juu ya kiwango cha kifafa kuliko kwengine,” amebainisha.

Ametolea mfano, “Baadhi ya maeneo ya Morogoro kulibainika kuna watu wengi wameathirika na hali ya kifafa wapo kwenye matibabu na tafiti zinaendelea.

“Inaonesha kuna tofauti ukilinganisha na maeneo mengine ikiwamo Dar es Salaam, ila kila eneo lipo katika kila watu 1000, watu 20 hadi 37 wana hali ya kifafa.

“Hasa katika maeneo ambako kuna hali ya juu ya ugonjwa. Sisi tunahamasisha watu wote ambao wana hizo hali za kifafa wawe makini, wafuatilie dawa na matibabu yao sahihi,” amesema.

Ameongeza “Ikifuatiliwa matukio kama haya yanapungua, kuna ajali wanagongwa, au wanaendesha gari inapotea njia anagongwa au inapinduka.

“Nyumbani alikuwa anapika bahati mbaya akaanguka anaungua, ila akiwa kwenye dawa au matibabu sahihi anakuwa sawa.

“Kuna elimu mbalimbali tunawapa inawafanya waishi salama, waendelee kufurahia maisha kwa sababu tuna haki sawa ya kufurahia maisha,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Mary Kipongili akizungumza kwa niaba ya watu wanaoishi na kifafa wakati wa uzinduzi huo, amesema,

“Kuna visa vya watoto kufukuzwa shule, kutokuajiriwa kufutwa kazi, kuvunjika kwa mahusiano au ndoa mtu anapogundulika na hali hii [ya kifafa].

Ameongeza “Pia kufanyiwa vitendo vya kishirikina, vitendo hivi huleta msongo wa mawazo kwa watu wanaoishi na hali ya kifafa.

“Kwa bahati mbaya uelewa wa jamii juu ya hali hii ya kifafa bado ni mdogo sana, kumekuwapo na unyanyapaa na kubaguliwa,” amesema Mary.

Ameongeza “[Hii] imepelekea watu hawa kukosa haki zao za msingi katika maisha yao ya kila siku, hivyo kudhoofisha ubora wa haki zao.

Kifafa ni miongoni mwa Magonjwa Yasiyoambukiza [NCD’s] ambayo yanashika kasi kwa ongezeko la idadi ya wagonjwa hivi sasa ulimwenguni, ikiwamo Tanzania.

Tafiti zinaeleza takribani watu 5 kati ya 10 wanaoishi na kifafa hupata tatizo la wasiwasi na ugonjwa wa Sonona.

Wagonjwa wa kifafa pia wapo katika hatari zaidi ya kufariki mapema [premature dealth] mara tatu zaidi kuliko watu wa kawaida.

“Kukabiliana na hali ya kifafa ni rahisi zaidi kuliko unyanyapaa wa hali ya kifafa,” amesema Mary na kufafanua..,

“Kutokana na hofu ya kunyanyapaliwa na kubaguliwa wengi wanaoishi na kifafa hawaendi vituo vya afya kupata tiba sahihi.

Kwa mujibu wa Mary, hiyo imepelekea usugu au ukali wa tatizo pia kuongeza madhara mengine.

“Hivyo sisi tukiungana na Serikali ya tanzania na taasisi zote za kijamii na kitaaluma, katika jitihada zao na kampeni za kuelimisha jamii kuhusu kifafa,

“.., kampeni hizi zitatusaidia kutokomeza unyanyapaa ili kupata tiba sahihi kwa watu wanaoishi na hali ya kifafa,” amesema.

Ameishukuru Serikali kwa kuongeza nguvu katika kupambana na [NCD’s.

Hata hivyo upande wa Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Afya Ulimwenguni [WHO], kuna watu wapatao Mil. 50 duniani wanaosumbuliwa na hali za kifafa.

Kulingana na ripoti za WHO, Barani Afrika inakadiriwa kuna zaidi ya watu Mil. 10 wanaoishi na hali ya kifafa.

Shirika hilo linakadiria kuna watu Mil. 6 wanaogundulika kila mwaka duniani wakiwa na hali hiyo.

WHO inaeleza nchini Tanzania kuna zaidi ya watu Mil. 1 ambao wanaishi na hali ya kifafa.






Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...