Na: Calvin Gwabara – Dodoma.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya
Kilimo imenunua na kuipatia Mamlaka ya
Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) ndege moja ya kisasa kwaajili ya
kupambana na visumbufu vya mimea ikiwemo kwereakwerea na nzige huku Serikali
ikitenga zaidi ya shilingi bilioni 20 kwaajili ya kununua ndege zingine tatu za
kisasa kusaidia wakulima kupambana na majanga hayo nchini.
Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe (Mb) akikagua na kupata maelezo ya ndege hiyo kutoka kwa rubani aliyeisafirisha kutoka nchini Marekani hadi Tanzania. |
Hayo yamesemwa na Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe (Mb) kwenye
hafla ya kupokea ndege hiyo ya kisasa aina ya THRUSH 510P2+ iliyofanyika kwenye uwanja wa ndege wa jijini
Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na mshirika yasiyo ya
kiserikali, Wabunge, wandau wa maendeleo ya Kilimo na Wananchi.
“ Hivi sasa tuna takribani hekta laki tisa za umwagiliaji
nchi nzima na tunataabika, lakini tunafikiria kufikia hekta milioni 3 au 5 naamini utakuwa mtihani mkubwa hivyo ni lazima
tujiandae, Kwahiyo maelekezo yangu kwa TPHPA na Mwenyekiti wa bodi na katibu
Mkuu wa Wizara ni kwamba, Mchakato ule tulioupitia wa miaka miwili wa kununua
ndege hii ya kwanza sitaki tuurudie tena”. Alisisitiza Mhe. Bashe.
Aliongeza “ Kwakuwa kwenye bajeti ijayo tumepitisha kunzisha
vituo vinne vya kilimo Anga kwa maana ya Arusha, Mbeya pale Songwe Airpot na
Mwanza Vituo hivi vyote vinatakiwa kuwa na ndege na ndege zisizo na rubani
(DRONES) kwahiyo naagiza mchakato wa
kununua ndege zingine tatu kama hii ya leo uanze mara moja maana ni lazima kama
nchi tujitegemee maana dunia ya kubebana haipo, lakini niwashukuru sana Shirika
la Chakula Duniani (FAO) wamesaidia sana kuiboresha TPHPA kufanikisha kuwa na
vutuo 36 kwenye mipaka yetu ambavyo vitakuwa na vifaa na maabara za kisasa”.
Aisha Mhe. Bashe amesema wamefanikiwa kununua droni kwaajili
ya kufanya ufuatiliaji na mwaka huu wanatarajia kuongeza zingine za kisasa kwaajili
ya kufanyakazi ya kupulizi viautilifu kwenye mazao lakini amewataka watanzania
kutambua kuwa Tanzania imepata bahati mbaya ya kuwa na maumbile ya mazalia ya Nzige kwenye
mikoa ya Dodoma, Katavi na Rukwa na kwa
bahati mbaya ni Nzige wekundu.
Waziri huyo wa kilimo amemtaka Katibu Mkuu wa Wizara hiyo
kuanza mchakato wa kuongea na Mamlaka ya Viwanja vya ndege nchini kuwapatia
maeneo kwenye viwanja hivyo kwaajili ya kujenga vituo vya Mamlaka ya afya ya
mimea kwenye viwanja hivyo na kuweka vifaa vyote muhimu kwenye kanda zote nne
kila kanda iwe na ndege yake na vifaa vyake kwaajili ya kupambana na majanga ya
wadudu hao hatari wanashambilia mazao.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof.Joseph Ndunguru
ameseama ujio wa ndege hiyo ni ukombozi mkubwa kwa wakulima na kuimarisha
usalama wa chakula nchini hasa kwa wakulima wa maeneo ya Bahi Dodoma, Kondoa
Singida, Mvomero na Kilosa Mkoani Morogoro,Mbarali na Kapunga Mkoani Mbeya,Ruvu
Mkoani Pwani, Simiyu, Mara na maeneo
mengine mengi ambayo yamekuwa yakikumbwa na changamoto za nzige na kwelea kwelea
na kuwapa wakulima hasara kubwa.
“Udhibiti wa ndege hao kwa miaka yote tumekuwa tukitumia
ndege ya kukodi ya Shirika la udhibiti wa Nzige wa Jangwani (DLCO -EC) kutoa
nchini Kenya na hivyo muda mwingine kujikuta tunachelewa kuwasaidia wakulima wetu
wanapotuhitaji kwa wakati kutoka na sababu mbalimbali hasa za kiutawala kuhitajika
kusubiria foleni yetu ifike kwakuwa ndege hiyo kuwa inatumiwa na nchi mbambilimbali
za afrika mashariki, hivyo ujio wake ni mkombozi mkubwa kwa wakulima wetu”
Alibainisha Prof. Joseph Ndunguru.
Aliongeza “Ndege hii unaweza kuiona ni ndogo lakini inauwezo
mkubwa sana, kwani ina tenki la mafuta la ujazo wa lita 863 ya kuiwezesha kukaa
angani bila kutua kwa zaidi ya masaa manne, lakini pia ina uwezo wa kubeba
viuatilifu lita 1930 karibu lita 2000 kwahiyo kuifanya kuwa na uwezo wa kudhibiti
ndege hao kwenye eneo la ukubwa wa ekari 2400 kwa mara moja sambamba na kuwa na
vifaa vya kisasa kufanya ufuatiliaji na kutoa takwimu zinazowezesha kufanya mipango
ya kuwadhibiti”.
Prof. Ndunguru amesema kuwa kwa kumia ndege hiyo sasa
watakuwa na uwezo wa kufikia maeneo mapana kwa muda mfupi zaidi kuliko
ilivyokuwa huko nyuma walipotumia mbinu za kizamani kuhakikisha kwamba athari
za ndege aina ya Kwelea kwelea zinapungua na hivyo kulinda mazao ya wakulima na
hatimaye kuhakikisha upatikanaji wa chakula kwa taifa.
Mkurugenzi huyo Mkuu wa TPHPA amesema Halmashauri za wilaya
40 nchini huvamiwa na ndege waharibifu aina ya Kwelea kwelea wanaokadiriwa
kufikia milioni 200 kila mwaka wenye uwezo wa kuharibu takribani tani 450,000
za nafaka lakini pia kwa kipindi cha kiangazi skimu za umwagiliaji wa mpunga 38
zimekuwa zikivamiwa na ndege hao wapatao takribani milioni 100 kila mwaka wenye
uwezo wa kula na kuharibu karibu tani za mpunga 225,000.
Hivyo Prof. Joseph Ndunguru ameishukuru Serikali ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa
kuweka histosria hii katika kipindi chake cha uongozi wa Serikali ya wamu ya
sita kwa kufanya mageuzi makubwa katika mamlaka hiyo ikiwemo kununua ndege hiyo
aina ya THRUSH 510P2+ kwa gharama za shilingi bilioni 6 za kitanzania ili
kusaidia wakulima nchini.
Nae mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Viwanda,Biashara,
Kilimo na Mifugo Mhe. Mariamu Ditopile Mzuzuri kwa niaba ya Bunge ameipongea
Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Waziri
wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe na Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru
na na watumishi wengine kwa kufanikisha ndoto hiyo ambayo imeotwa kwa muda
mrefu.
“Toka tumeanza Bunge kwenye Serikali hii ya awamu ya sita
Mhe. Waziri pamoja na timu yako kuna mambo mengi ambayo umekuwa ukija nayo
kwenye kamati hizi tunashangaa kwakuwa ni
vitu ambavyo hatujazoea kabisa kwenye kilimo, hata lilipokuja swala la ununuzi
wa ndege hii tuliona ni maneno maneno lakini
sasa tunaona fahari kwa kazi hii nzuri na kuzingatia mapendekezo na ushauri
ambao umekuwa ukitolewa na Wabunge Bungeni” alisema Mhe. Mzuzuri.
Aliongeza “Kwakweli huu ni ukombozi kwa wakulima wetu maana
tumekuwa tukisikia malalamiko mengi kwa wakulima kwenye maeneo mbalimbali kama
ambavyo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Staki Senyamule alivyosema lakini
kumbe ndege tuliyokuwa tunaitumia ni ya kukodi kutoka Kenya na ilikuwa
ikitumiwa na nchi zingine pia, hivyo wanafika wanakutana na foleni ya kusubiria
wakati wakulima mazao yanazidi kushambuliwa sasa tumepata ndege yetu wenyewe itakayowakomboa
wakulima wetu na kuwafuta machozi ya kuharibiwa kwa mazao yao”.
Kwa upande wake Mweyekiti wa bodi ya Wakurugenzi ya (TPHPA) Prof.
Andrew Temu kwa niaba ya wajumbe wa bodi na wafanyakzi wote wa ameahidi
kuitunza ndege hiyo na vifaa vyote ambavyo Serikali inavitoa katika kuhakikisha
vinafanya kazi iliyokusudiwa kwa maslahi mapana ya taifa sambamba na kutoa
mafunzo kwa watumishi namna ya kutumia vifaa hivyo vya kisasa kwa na kupeleka
mtu kusomea namna ya kuendesha ndege hiyo na fundi wa kuifanyia matengenezo.
Aidha amesema amepokea maelekezo ya kuanza mchakato wa
kununua ndege zingine tatu na kupata moja ya kufanya ufuatiliaji ili kuipa
ndege hii iliyopokelewa nafasi ya kufanya kazi kubwa ya kupulizia viuatilifu na
kuua wadudu huku akiona fursa ya kutumia kiwanda cha kuunganisha ndege cha
Morogoro katika kupata ndege hizo zingine zitakazofuata.
Ndege hiyo ikipata heshima ya watal saluti mara baada ya kutua kwenye uwanja wa ndege wa Dodoma kwa mara ya kwanza nchini Tanzania. |
Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof.Joseph Ndunguru akitoa salamu za Mamlaka hiyo na maelezo ya ndege hiyo. |
Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe (Mb) akizungumza wakati wa mapokezi ya ndege hiyo.
|
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...