Wanahisa wa Benki ya Mwanga Hakika (MHB) wameeleza kuridhishwa kwao na ongezeko kubwa la faida la asilimia 53 pamoja na mipango mkakati ya benki hiyo ya kuboresha huduma kwa wateja na kukuza uchumi wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka (AGM) uliofanyika tarehe 31 Mei 2025 wilayani Mwanga, mkoani Kilimanjaro.
Wakiwa wamekusanyika pamoja na Bodi ya Wakurugenzi, Viongozi
wa Serikali na Menejimenti ya benki, wanahisa walipokea taarifa ya mafanikio ya
mwaka 2024 kwa furaha na matumaini makubwa.
Jambo lililowavutia wawekezaji waliokuwepo.katika mkutano
huo ni kuwasilishwa kwa matokeo ya mwaka 2024, yaliyoonyesha ongezeko kubwa la
asilimia 53 ya faida, kufikia Shilingi Bilioni 9.9 kwa mwaka 2024 kutoka
Shilingi Bilioni 6.5 mwaka uliopita 2023.Wanahisa waliona matokeo hayo kama
ushahidi wa utendaji madhubuti wa benki na uthibitisho kuwa uwekezaji wao una
tija.
Katika hotuba yake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya
Benki ya Mwanga Hakika, Bw. Ridhuan Mringo, alielezea mafaniko makubwa ya benki
hiyo pamoja na mipango Madhubuti ya benki hiyo, vilevile alimtaja kwa heshima
mwanzilishi mmojawapo wa benki hiyo, hayati Mhe. Cleopa David Msuya, akisema
alikuwa zaidi ya muasisi kwetu katika benki yetu, hivyo tutaendelea kumuenzi.
Mkuu wa Idara ya Fedha ya Benki ya Mwanga Hakika, Bw.
Chomete Abdallah Hussein, aliwasilisha takwimu zilizodhihirisha kasi ya ukuaji
wa benki. Faida baada ya kodi iliongezeka hadi Shilingi bilioni 14.6, sawa na
silimia 46. Amana za wateja ziliongezeka kwa asilimia 51 hadi kufikia Shilingi
bilioni 214.8, huku jumla ya mali ikifika Shilingi bilioni 324.9.
Kwenye robo ya kwanza ya mwaka 2025, benki imepata faida ya
Shilingi bilioni 4.1 kabla ya kodi, na mali zimefikia Shilingi bilioni 355.5
huku mikopo ikifikia Shilingi bilioni 220 na amana zikiongezeka hadi Shilingi
bilioni 261.2.
MHB pia imeongeza mtaji wake kutoka Shilingi bilioni 17 hadi
bilioni 26, jambo lililosaidia kuongeza mtaji wa wanahisa hadi Shilingi bilioni
48.3, hali inayoimarisha uthabiti wa kifedha wa benki na uwezo wa kupanua
huduma zaidi.
Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wakubwa, Bw. Projest Massawe,
alisema kuwa benki hiyo imeendelea kutoa huduma kwa wateje wakubwa, wadogo na
wa kati, kwa kuendelea kuwapa huduma bora zaidi na zinao kidhi mahitaji yao.
Alisema mafanikio hayo yanatokana na ukaribu wa benki hiyo
na jamii, ambapo siku chache kabla ya mkutano huu, tumefanya zoezi la upimaji
wa afya ya macho bure, pamoja na hutoa miwani kwa waliokutwa na changamoto ya
afya ya macho bure, kwa wakazi Ugweno na Usangi, wilayani Mwanga.
Mmoja wa wanahisa waliokuwepo alisema, “Ninajivunia kuwa
sehemu ya Mwanga Hakika. Hisa zangu zimeongezeka thamani, na kuona benki
inazidi kukua kunanipa matumaini zaidi kwa siku zijazo.
Kwa ujumla, mkutano huo ulihitimishwa kwa ujumbe mmoja mkubwa kutoka Mwanga: Benki ya Mwanga Hakika inaendelea kujenga mustakabali bora wa huduma za kifedha, pamoja na kuendelea kutoa huduma bora zaidi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...