Na: Calvin Gwabara – Dodoma.

Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) yazindua kifaa maalumu cha kisasa aina ya MinION cha kutambua vinasaba (DNA) za mimea, Wadudu na magonjwa ambacho kinauwezo wa kufanya uchunguzi na kutoa majibu papo hapo shambani ndani ya muda mfupi na hivyo kusaidia jitihada za serikali za kutatua changamoto visumbufu vya mazao ya wakulima na kuongeza uzalishaji.

Watumishi wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA)wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wao Prof. Joseph Ndunguru wakishangilia uzinduzi wa kifaa hicho kama hatua mpya ya matumizi ya sayansi ya juu katika kusaidia wakulima nchini. 

Akizungumza na Waandishi wa habari, wadau wa kilimo na wananchi wengine kwenye banda la TPHPA ndani ya viwanja vya maonesho ya kilimo nanenane kitaifa jijini Dodoma Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru amesema kuwa kupatikana na kifaa hicho ni mkombozi katika utatuzi wa ya changamoto ya visumbufu vya mimea kwa wakulima nchini.

“Kifaa hiki kilibuniwa nchini Uingereza kwa lengo la kutambua virusi vya Zika na Ebora lakini sisi tumeweza kufanya majaribio ya kina na kisha kuthibitisha kwa asilimoa 100% kuwa kinauwezo mkubwa wa kutumika kwenye sekta ya kilimo na hivyo kuifanya Tanzania kuwa wa nchi ya kwanza kuitumia teknolojia hii kutambua vinasaba vya wadudu, mimea lakini pia utambuzi wa magonjwa kwa haraka mnoo” alibainisha Prof. Ndunguru.

Mkurugenzi huyo amesema kupitia ushirikiano kati ya Umoja wa Ulaya (EU), Shirika la chakula Duniani (FAO) na Serikali ya Tanzania kupitia (TPHPA) wameweza kufanikiwa kupata vifaa hivyo 20 ambavyo vitakwenda kuwekwa kwenye vituo vya Mamlaka hiyo  kwenye kanda zote na kushirikiana na wataalamu wengne wa kilimo kubaini vinasaba mbalimbali vya wadudu na magonjwa sugu na ya mlipuko kwenye maeneo yote ya Tanzania.

Aidha amebainisha kuwa kwa kutumia kifaa hicho sasa Tanzania itaweza kuzalisha vyakula na bidhaa zinazokidhi mahitaji ya masoko ya kimataifa kwakuwa watakuwa na uwezo wa kupima na kuthibitisha ubora wa mazao kama yamekidhi viwango lakini pia kuzuia uingizwaji wa mazao hasa vyakula ambavyo vina zuio kutokana na kuwa na vidudu au magonjwa hatari kwa usala wa chakula na kilimo nchini.

“Teknolojia hii sio kwamba tutaitumia sisi kwenye kilimo tuu la hasha, bali tunaweza kushirikiana na wenzetu kwenye Wizara na Taasisi mbalimbali kwenye kutambua vinasaba na majonjwa kama vile katika masuala ya uhifadhi kwenye kutambua mimea, viumbe maji, lakini hata kwa wanyamapori na magonjwa ya binadamu inaweza kutoa majibu haraka sana kuliko teknolojia tulizonazo sasa” alieleza Prof. Ndunguru.

Aliongeza “Tanzania tunajivunia kuwa wa kwanza kutumia teknolojia hii na ni kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa na serikali yetu ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha changamoto za visumbufu vya mazao vinabainishwa na kukabiliwa kwa kutumia viuatilifu sahihi badala ya kubahatisha na kumuacha mkulima akilia na kupoteza mazao yake”.

Awali Mkurugenzi wa Kurugenzi ya afya ya mimea kutoka TPHPA Dkt. Benignus Ngowi amebainisha kuwa zipo changamoto nyingi ambazo zinawatesa wakulima hususani magonjwa na wadudu na nyakati nyingine yanapotokea magonjwa ya mlipuko huchukua muda mrefu kupata majibu toka sampuli zinapochukuliwa na kupelekwa maabara lakini kwa kifaa hicho sasa wanauwezo wa kupata majibu hapohapo shambani ndani ya dakika ishirini na kutambua tiba yake.

Dkt. Ngowi amesema kumekuwa na vilio kwa wakulima wa Nyanya, Migomba, Mihogo, Mahindi na mazao mengine ya bustani na hiyo imekuwa ikitokana na wakulima kutumia viuatilifu kwa kubahatisha bahatisha lakini kupitia kifaa hicho sasa hakutakuwa na kubahatisha katika kukabili magonjwa na wadudu visumbufu.

“ Ukienda kwa wakulima wa mbogamboga na matunda mfano nyanya utakutana na kilio cha mdudu hatari tuta ablsoluta wakulima wanamuita “Kantangaze”, lakini pia kuna wadudu wengine kwenye matunda kama vile Nzi weupe “White flies”, ukienda kwenye mihogo kuna magonjwa ya Batobato na michirizi ya kawahawia ambayo inasambabishwa na wadudu hao lakini mkulima akiwaangalia anaweza kuona wanafanana au ni mdudu wa aina moja lakini kuna aina nyingi za wadudu hao ambao wanadhibitiwa kwa aina tofauti na sio dawa moja kama wakulima wanavyodhani na mwisho wa siku hulalamika wametumia dawa na wadudu bado wanashambulia lakini sasa kifaa hiki ni mkombozi” alifafanua Dkt. Ngowi.

Baada ya maonesho hayo tayari timu ya wataalamu kutoka TPHPA wanatarajia kuweka kambi kwenye Halmashauri ya wilaya ya Kilolo kwaajili ya kubaini changamoto za magonjwa na wadudu wanasababisha hasara kwa wakulima wa mazao ya mbogamboga katika eneo hilo maarufu kwa mazao hayo.

MATUKIO KATIKA PICHA WAKATI WA UZINDUZI WA TEKNOLOJIA HIYO.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) Prof. Joseph Ndunguru akielezea Waandishi wa habari na wadau wa kilimo namna teknolojia hiyo inavyofanya kazi na faida yake kwa taifa.
 

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Afya ya Mimea kutoka TPHPA Dkt. Benignus Ngowi akieleza kwa kina changamoto za visumbufu vya mimea vinavyosumbua wakulima na vinavyoweza kubainishwa kirahisi kwa kutumia kifaa hicho.
  









Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...