-Neema yaja kwa wananchi wanaoishi karibu na maeneo ya uwekezaji

Na Beatus Maganja, Dar es Salaam

Katika hatua ya kihistoria na kishindo kwa sekta ya utalii nchini, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), leo Agosti 12, 2025, imesaini mikataba minne ya uwekezaji wa utalii kupitia utaratibu wa Uwekezaji Mahiri (SWICA) na kampuni ya kitanzania ya Uhusiano International ICT Ltd.

Mikataba hiyo inatarajiwa kuingiza mapato ya Dola za Marekani milioni 281.5 (sawa na Shilingi Bilioni 719 za Kitanzania) kwa kipindi cha miaka 20 ikiwa ni wastani wa Shilingi Bilioni 36 kwa mwaka.

Hafla ya utiaji saini imefanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam na imehusu uwekezaji katika vitalu vinne vya Burko Open Area (Monduli – Arusha), Selous MHJ1, Selous MHJ2 na Selous ML1 (Liwale – Lindi), vyote vikiwa chini ya kampuni ya Uhusiano International ICT Ltd inayomilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana amesema uwekezaji huo utaimarisha sekta ya uwindaji wa kitalii na utalii wa picha, sambamba na kuleta ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya uwekezaji. Miradi ya maendeleo itakayoibuliwa na wananchi wenyewe inakadiriwa kugharimu Dola milioni 1.8 (sawa na Shilingi Bilioni 4.6) kwa miaka 20.

Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana pia alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake madhubuti katika kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia filamu za Amazing Tanzania na The Royal Tour, zilizochochea ongezeko la watalii na wawekezaji.

Aliahidi kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kusisitiza umuhimu wa matumizi endelevu ya rasilimali kwa kuzingatia sheria, kanuni na misingi ya uhifadhi bora. Alitoa wito kwa wawekezaji zaidi kuja kuwekeza katika vivutio vya kipekee vya utalii vilivyopo nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAWA, Meja Jenerali (Mstaafu) Hamis R. Semfuko, amesema TAWA imepiga hatua kubwa kwa kusaini mikataba minne mipya ya SWICA na kufikisha jumla ya mikataba 13 kati ya 14 iliyopangwa sawa na asilimia 92.3 ya lengo, hatua iliyowezesha kukusanya zaidi ya Shilingi Bilioni 27.4 kati ya Januari 2024 na Agosti 2025.

Aidha, Meja Jenerali Semfuko alibainisha kuwa TAWA ipo katika hatua za mwisho kusaini mkataba na kampuni ya GBP Trading Ltd (GTL) kwa ajili ya ujenzi wa kambi za kudumu za kitalii katika hifadhi za Kijereshi, Mpanga-Kipengere na Wami-Mbiki, hatua itakayoongeza vitanda 240 na kupunguza uhaba wa malazi kwa watalii.

Awali, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Bw. Mlage Yusuph Kabange, alisema tangu kusainiwa kwa mikataba ya awali ya SWICA mwaka 2024, TAWA imeshuhudia ongezeko kubwa la mapato kutoka Shilingi Bilioni 55 hadi Shilingi Bilioni 87.12 katika mwaka wa fedha 2024/25, sawa na ongezeko la asilimia 158.2.

Aliongeza kuwa TAWA inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa uwekezaji, ikiwemo ujenzi wa kilomita 453.2 za barabara kwa kiwango cha changarawe katika maeneo ya kimkakati sawa na asilimia 40 ya lengo la kujenga kilomita 1,127 ifikapo mwaka 2026.

Kamishna Kabange alisisitiza kuwa TAWA ipo tayari kushirikiana na wawekezaji ili kuhakikisha utekelezaji bora wa mikataba hiyo kwa manufaa ya Taifa na wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Kampuni ya Uhusiano International ICT Ltd, Bw. Zahir Hassan Mulla, alitoa shukrani kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Maliasili na Utalii, pamoja na Bodi na Menejimenti ya TAWA kwa kuridhia pendekezo lao la uwekezaji. Alisema huu ni mwanzo mzuri kwa wawekezaji wa ndani kuonesha uwezo wao katika sekta ya utalii.










Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...