Na Albert Kawogo,Bagamoyo
SERIKALI imezitaka taasisi zinazosimamia malezi ya watoto yatima na wale wanaoshi katika mazingira magumu kusimamia miongozo,taratibu na sheria katika matumizi ya misaada mbalimbali wanayopewa ili kujenga imani ya wahisani wanaotoa misaada hiyo
Wito huo umetolewa hivi karibuni na Afisa Ustawi wa Jamii wa Wilaya ya Bagamoyo Abuu Yasin wakati wa sherehe ya miaka 25 ya kuadhimisha kituo cha kuelelea watoto yatima cha Moyo Mmoja kilichoko mjini hapo
Yasin amesema kumekuwa na matatizo ya baadhi ya vituo vya watoto yatima kutumia vibaya misaada ya wahisani hasa fedha jambo ambalo linawakatisha tamaa watoa misaada na madhara yake yanakwenda moja kwa moja kwa walengwa wakuu wa misaada hiyo ambayo ni yatima.
"Sisi kama serikali taratibu na sheria zetu ziko wazi na kazi yetu sisi ni kuwahimiza kufuata miongozo hiyo ili kulinda imani ya wafadhili" Amesema
Aidha Yasin alikisifu kituo cha Moyo Mmoja Trust kuwa kama mfano wa vituo vingine katika kuendesha shughuli zake kwa usahihi jambo ambalo limevutia wahisani kukisaidia kwa muda wa miaka 25 sasa.
Kwa upande wake Meneja wa Moyo Mmoja Trust Shilinde Masangu amesema kwa zaidi ya miaka 25 Taasisi hiyo imeweza kusaidia kwa ufanisi mkubwa watoto waliopoteza wazazi kutokana ajali magonjwa na hali ngumu za maisha.
Shilinde amesema wamelea watoto wengi zaidi ambao wamepata elimu ya Chuo Kikuu na ile ya ujuzi wengine wakiajiriwa na wengine wakijiajiri.
Meneja amesema pamoja na changamoto mbalimbali za malezi ya kielinu lakini kubwa ni Ile ya watoto wanaolelewa hapo kukosa mikopo ya elimu ya juu pindi wakiwa vyuo vikuu.
"Ugumu wa kupata mikopo ya elimu ya juu kwa watoto wetu walioko vyuo vikuu limekuwa ni tatizo licha ya kujaribu mara kwa mara".Amesema Shilinde
Naye Meneja wa Taasisi ya Ushirikia wa Tanzania na Norway TANO Olav Holten amesema Norway kupitia TANO kwa muda wa miaka 25 imekuwa mstari wa mbele kusaidia Moyo Mmoja kwenye misaada ya kufanya kituo hicho kiweze kuendelea kutoa huduma zaidi
Holten amesema TANO inaamini kuwa kila mtoto anahitaji kupata huduma zote muhimu za makuzi ikiwemo upendo elimu afya na uhifadhi hata kama amepoteza wazazi au walezi.
Amesema amefurahi sana kuona watoto wakiwa na sehemu wanayoweza kuita hapa ni nyumbani kwao.
Pia Holten amesema TANO itaendelea kudumisha ushirikiano na kituo hicho kwenye jitihada zote kuimarisha malezi ya watoto ili kulinda ustawi wa utu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...