■ Ni madini muhimu kwenye Sekta ya Ujenzi
Imeelezwa kwamba, katika kipindi cha mwaka mmoja wa Fedha 2024/25 Madini Ujenzi na Viwandani yenye thamani ya zaidi ya shilingi Trilioni Moja yalizalishwa.
Hayo yalielezwa Novemba 27, 2025 na Naibu Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa wakati wa utoaji Tuzo za Ujenzi na Miundombinu za Afrika Mashiriki zilizotolewa Jijini Dar es Salaam.
Dkt. Steven Kiruswa alisema kuwa, kutokana na kukua na kuendelea kwa sekta ya ujenzi nchini hususan kwenye ujenzi wa miundombinu na ukuaji wa sekta ya viwanda kimezalishwa kiasi hicho cha fedha kupitia wachimbaji wa madini hayo.
Dkt. Kiruswa aliongeza kuwa, kwa kipindi kirefu mchango wa madini ya viwanda na ujenzi yamekuwa na uwanja mpana kwenye kuchangia uchumi wa Taifa ikiwa pamoja na kutoa ajira kwa jamii, kuunganisha mnyororo wa thamani madini kupitia biashara na wawekezaji wa ndani kuanzia ngazi wilaya mpaka Taifa.
Dkt.Kiruswa alifafanua kuwa Tanzania itaendelea kutumia malighafi zake za ndani kama vile mchanga, kokoto, chokaa, gypsum, kaolini, mawe ya naksi na saruji ili kupunguza gharama , kuharakisha miradi na kuiwezesha sekta binafsi kwenye mnyororo wa uchumi endelevu.
Sambamba na hayo Dkt.Kiruswa aliwapongeza Chemba ya Sekta ya Ujenzi na Miundombinu Tanzania kwa kuandaa hafla ya Tuzo za Ujenzi na Miundombinu Afrika Mashariki, na kueleza itakuwa chachu ya kuongeza nguvu katika uzalishaji, uendelezaji na kuifungamanisha na sekta nyingine za kiuchumi.
Pamoja na mambo mengine Dkt.Kiruswa alitumia jukwaa hilo kuwaomba washiriki wa hafla hiyo kuwaasa vijana wa kitanzania kuipenda na kuilinda miradi ya ujenzi na miundombinu ambayo inajengwa kwa gharama kubwa.








Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...