Na Paul Kayanda, Kahama


MWENYEKITI wa Mtaa wa Mwime, Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, Stella Bhayugile, amesema utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali inayoongozwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan umeendelea kuleta matumaini mapya kwa wananchi.

Huku vijana na wanawake wakinufaika kwa kiwango kikubwa kupitia vikundi vyao vya uzalishaji na ujasiriamali.

Akizungumza katika mahojiano maalumu ofisini kwake Jumatano, Julai 15, 2026, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime unaendelea kushuhudia maendeleo makubwa yanayochochewa na usimamizi mzuri wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alisema kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, vikundi zaidi ya 12 vya vijana na wanawake katika mtaa wa Mwime tayari vimepatiwa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, hatua ambayo imewawezesha kuanzisha na kupanua shughuli mbalimbali za kiuchumi.

"Mpaka sasa zaidi ya vikundi 12 vya vijana na wanawake vimepata mikopo katika kipindi cha robo mbili za mwaka wa fedha. Mikopo hii imewapa uwezo wa kujiajiri, kuongeza kipato cha familia na kuboresha maisha yao.

Tunamshukuru sana Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira yanayowainua wananchi kiuchumi," alisema Bhayugile.

Alibainisha uongozi wa mtaa huo umeendelea kushirikiana kwa karibu na wananchi katika kusimamia miradi ya maendeleo ili kuhakikisha fedha zinazotolewa na Serikali zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayoonekana.

Mbali na mikopo hiyo, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime umefanikiwa kujenga zahanati inayotoa huduma za afya kwa wananchi, hivyo kupunguza adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.

Aidha, alisema eneo hilo lina shule ya msingi yenye wanafunzi zaidi ya 1,886, huku juhudi zikiendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia kupitia ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu.

Alieleza matundu 16 ya vyoo yamejengwa, na kwa sasa unaendelea mradi wa kufumua mfumo wa mashimo ya zamani ili kujenga vyoo vipya vya kisasa vitakavyokidhi mahitaji ya wanafunzi na walimu.

Katika sekta ya miundombinu, Bhayugile alisema Serikali imetoa zaidi ya Sh milioni 15 kwa ajili ya ukarabati wa barabara za Mtaa wa Mwime na maeneo jirani, hatua ambayo imeboresha usafiri na kurahisisha shughuli za kiuchumi kwa wananchi.

Pia alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu, wakiwemo wenye ulemavu wa kusikia, uoni hafifu,mtindio wa ubongo na makundi mengine yanayohitaji mazingira rafiki ya kujifunzia.

Bhayugile alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya wananchi, viongozi wa Serikali za Mitaa na Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, akisisitiza kuwa maendeleo haya ni ishara ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nyuma.

Aliwataka wananchi kuendelea kushiriki katika shughuli za maendeleo, kulinda miradi inayotekelezwa na kutumia ipasavyo fursa zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...