Wanahisa wamepitisha Ripoti ya Wakurugenzi, Ripoti ya Wakaguzi wa Hesabu na taarifa za fedha zilizokaguliwa kwa mwaka ulioishia tarehe 31 Desemba 2025.

Mkutano Mkuu wa Wanahisa (AGM) umethibitisha mgao wa muda (interim dividend) uliolipwa kwa mwaka huo na kuidhinisha kampuni ya PricewaterhouseCoopers kuwa wakaguzi wa hesabu wa nje kwa mwaka 2026.

TBL imehitimisha mwaka kwa ongezeko la faida, ukuaji endelevu wa chapa zake na kuendelea kuwekeza katika mfumo wake wa ndani wa uchumi.

Dar es Salaam, Tanzania – Alhamisi, tarehe 2 Julai 2026: Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL Plc) leo imefanya Mkutano Mkuu wa 53 wa Wanahisa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, huku wanahisa wengine wakishiriki kupitia mfumo wa mkutano wa mtandaoni.

Mkutano huo uliwapa wanahisa fursa ya kupitia utendaji wa kampuni kwa mwaka 2025, kuidhinisha masuala muhimu ya utawala bora wa kampuni na kujadiliana na Bodi ya Wakurugenzi pamoja na Menejimenti kuhusu mwelekeo wa kampuni.

Katika mkutano huo, wanahisa walipitisha kumbukumbu za Mkutano Mkuu wa 52 wa Wanahisa, wakapitisha Ripoti ya Wakurugenzi, Ripoti ya Wakaguzi wa Hesabu na taarifa za fedha zilizokaguliwa kwa mwaka ulioishia tarehe 31 Desemba 2025, pamoja na kuthibitisha mgao wa muda uliolipwa kwa mwaka huo.

Wanahisa pia waliidhinisha uteuzi wa kampuni ya PricewaterhouseCoopers kuwa wakaguzi wa hesabu wa nje kwa mwaka wa fedha unaoishia tarehe 31 Desemba 2026.

TBL iliripoti mwaka wenye ukuaji mkubwa wa faida ambapo mapato yaliongezeka kwa asilimia 13 na faida ya uendeshaji ikaongezeka kwa asilimia 35. Matokeo hayo yalichangiwa na ongezeko la mahitaji ya bia na vileo vikali, usimamizi madhubuti wa gharama, uwekezaji endelevu katika chapa pamoja na maboresho katika mfumo wa usambazaji wa bidhaa sokoni.

Balozi Ami R. Mpungwe, Mwenyekiti wa Muda wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanzania Breweries PLC, alisema kuwa Mkutano Mkuu wa Wanahisa umeendelea kuthibitisha dhamira ya kampuni ya kuzingatia utawala bora, kuimarisha imani ya wanahisa na kuendelea kujenga thamani ya muda mrefu.

"Mkutano Mkuu wa Wanahisa unabaki kuwa jukwaa muhimu la uwajibikaji kwa TBL. Unawapa wanahisa taswira ya wazi kuhusu utendaji wa kampuni, utawala wake na mwelekeo wake wa baadaye. Bodi itaendelea kutoa usimamizi madhubuti, kulinda maslahi ya wanahisa na kuunga mkono Menejimenti huku kampuni ikiendelea kukua kwa uwajibikaji na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Tanzania."

Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle N. Kilpin, alisema kuwa matokeo ya mwaka 2025 yanaonesha nguvu ya chapa za kampuni, wafanyakazi wake, wateja na wadau wote katika mnyororo wa thamani.

"Matokeo yetu ya mwaka 2025 yamechochewa na uimara wa chapa zetu, utekelezaji wenye nidhamu pamoja na imani ya watumiaji wetu, wateja na wanahisa. Tutaendelea kuwekeza katika chapa zinazopendwa na watumiaji, kuimarisha mifumo yetu ya kidijitali, kuongeza matumizi ya malighafi za ndani na kuboresha ufanisi wa shughuli zetu. Lengo letu ni kukua kwa uwajibikaji huku tukitengeneza thamani kwa wanahisa wetu na mfumo mzima unaoiunga mkono TBL nchini Tanzania."

Mbali na mafanikio ya kifedha, TBL iliendelea kuimarisha mchango wake katika mnyororo wa thamani wa ndani. Mwaka 2025 ulikuwa mwaka wa kwanza kamili wa uendeshaji wa Kiwanda cha Kimea cha Kilimanjaro, ambacho kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha tani 8,000 za kimea kwa mwaka na hivyo kuongeza matumizi ya shayiri inayolimwa nchini.

Kampuni pia iliendelea kupanua mfumo wa kidijitali wa kuagiza bidhaa, kuimarisha ushirikiano na wauzaji wa rejareja pamoja na kuwaunga mkono wakulima wadogo wa shayiri na mtama.

Uendelevu uliendelea kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa muda mrefu wa TBL. Mwaka 2025, asilimia 92 ya vifungashio vya kampuni vilikuwa vinaweza kurejeshwa au vilitengenezwa kwa kiwango kikubwa kutokana na malighafi zilizorejelewa. Aidha, matumizi ya maji yaliendelea kuwa wastani wa hekta lita 2.55 kwa kila hekta lita moja ya uzalishaji. Kampuni pia iliendelea kuhamasisha matumizi yenye uwajibikaji ya bidhaa zake na kusaidia maendeleo ya wafanyabiashara wa rejareja nchini kote.

Bodi ya Wakurugenzi pamoja na Menejimenti waliwashukuru wanahisa kwa kuendelea kuiamini kampuni na kusisitiza dhamira ya TBL ya kuendelea kukuza biashara, kuimarisha chapa zake, kutekeleza mikakati yake kwa nidhamu na kujenga thamani endelevu.

Kadri TBL inavyoadhimisha Mkutano Mkuu wake wa 53 wa Wanahisa, kampuni inaendelea kujenga juu ya historia yake ndefu ya ushirikishwaji wa wanahisa, ukuaji wa chapa zake na mchango wake katika uchumi wa Tanzania. Dhamira yake inaendelea kuwa kukuza biashara kwa uwajibikaji, kuwekeza katika chapa zinazoaminika na kuendelea kutengeneza thamani kwa wanahisa, wateja, wafanyakazi, wasambazaji, wauzaji wa rejareja, wakulima na jamii nchini kote.

Kutoka kushoto ni Ami R. Mpungwe (Mwenyekiti wa Mpito wa Bodi ya Tanzania Breweries PLC), Michelle Kilpin, Mtendaji Mkuu wa TBL (Katikati)  akizungumza na wanahisa katika Mkutano Mkuu wa Wanahisa, ambapo wanahisa wamepitisha taarifa ya fedha ya mwaka wa mapato wa 2025/2026 kufuatia ukuaji wa faida uliotangazwa. Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Fedha TBL, Avito Swai




Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...