Na Mwandishi Wetu

Meneja Kanda ya Kati wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Bi. Hawa Lweno, ametoa wito kwa mafundi umeme kutembelea banda la Mamlaka hiyo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya John Malecela jijini Dodoma, ili kupata elimu kuhusu umuhimu wa kupata leseni za ufundi umeme zinazotolewa na EWURA, pamoja na utaratibu wa kuomba leseni hizo.

Amesema kuwa leseni za ufundi umeme ni muhimu katika kuhakikisha huduma za ufungaji, ukarabati na matengenezo ya mifumo ya umeme zinafanywa na mafundi wenye sifa na wanaozingatia viwango vya ubora na usalama, hivyo kupunguza ajali zinazoweza kusababishwa na kazi za umeme zisizokidhi matakwa ya kitaalamu.

“Hili linaendana sambamba na wito kwa wananchi kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mifumo yao ya umeme kila baada ya miaka mitano tangu mfumo huo ulipofungwa,” ameeleza.

Bi. Lweno amesema EWURA pia inatumia Maonesho ya Nanenane kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia unaolenga kuongeza matumizi ya nishati safi kwa Watanzania.

Aidha, maeneo mengine yanayotolewa elimu ni pamoja na fursa za uwekezaji wa vituo vya mafuta katika maeneo ya vijijini, taratibu za kuwasilisha na kushughulikia malalamiko yanayohusu huduma zinazodhibitiwa na EWURA, pamoja na matumizi salama ya huduma za mafuta, umeme na gesi.

     

Mchungaji wa Makanisa ya Mlima wa Moto, Rose Mgeta akizungumza jijini Dar es Salaam leo Agosti 07, 2026 wakati wa Ibada ya Shukrani ya mwanzilishi wa shule za St. Mary’s.
Meneja wa Shule za St. Mary’s, Muta Rwakatare  akizungumza jijini Dar es Salaam leo Agosti 07, 2026 wakati wa Ibada ya Shukrani ya mwanzilishi wa shule za St. Mary’s.

Na Mwandishi Wetu
MENEJA wa Shule za St. Mary’s, Muta Rwakatare, amesema mabadiliko ya mitaala ya elimu yanayoendelea nchini yanaifanya shule hiyo kujiandaa zaidi kukidhi mahitaji mapya ya wazazi, wanafunzi na taifa kwa ujumla.

Rwakatare ameyasema hayo leo Agosti 7, 2026 wakati wa ibada ya shukrani kufuatia kifo cha Mchungaji Getrude Rwakatale ambaye alikuwa mmiliki wa shule hizo amesema mtaala wa sasa umeelekezwa zaidi katika matumizi ya teknolojia za kidijitali na ujuzi wa kiufundi, hivyo St. Mary’s imejipanga kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu inayokwenda sambamba na mahitaji ya wakati.

“Ni kweli mtaala umebadilika. Sasa hivi uko kiufundi na kidijitali zaidi. Lakini kwa St. Mary’s tumejipanga kuhakikisha kwamba mtaala uliopo sasa, ambao umeletwa ukiwa mpya, unakidhi mahitaji ya wateja wetu ambao ni wazazi wetu,” amesema.

Amesema pamoja na masomo ya kitaaluma, shule hiyo itaendelea kuzingatia michezo, sanaa na tasnia mbalimbali katika malezi ya wanafunzi ili kukuza vipaji vyao na kuwaandaa kukabiliana na mahitaji ya jamii na taifa.

Aidha, ameiomba Serikali kuendelea kushirikiana na shule katika utekelezaji wa maboresho ya elimu, hususan katika eneo la teknolojia za kidijitali, akisema hatua hiyo itasaidia kurahisisha utoaji wa elimu na kuongeza ufanisi katika shule, ikiwamo binafsi.

“Kikubwa ni kwamba kwenye tasnia ya sasa tuko kidijitali zaidi. Kwa kutusaidia katika kuboresha mtaala huu, tunaamini elimu itakuwa nyepesi na nzuri zaidi kwa shule zote, hususan shule binafsi,” amesema.

Kwa upande wake, Mchungaji wa Makanisa ya Mlima wa Moto, Rose Mgeta, amesema mabadiliko ya mitaala yanahitaji jamii ya shule kujiandaa ipasavyo ili wanafunzi wapate elimu inayokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Mgeta amesema Serikali inapaswa kuendelea kushirikiana na shule binafsi katika kuwezesha matumizi ya teknolojia katika elimu, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha michezo, sayansi na masomo mengine yatakayowawezesha wanafunzi kuwa na ujuzi unaohitajika katika dunia ya sasa.

“Tunaiomba Serikali itusaidie katika hilo ili tujikite zaidi kwenye michezo na vilevile katika tasnia ya elimu kwa ujumla, lakini zaidi katika eneo la kidijitali. Tuwe na mtaala wa kidijitali zaidi, sayansi na masomo mengine yote ili tuweze kukidhi vigezo vya wazazi wetu,” amesema.

Licha ya hayo amesema shule hizo zinaendeleza misingi na tamaduni zilizoachwa na Askofu Mama, Getrude Rwakatare, huku akieleza kuwa uongozi wa sasa unaendelea kuthamini na kuendeleza kazi nzuri inayofanywa na viongozi wa Kanisa na taasisi za St. Mary’s, akiwamo Bishop Rose Mgeta.

“Kwa hiyo, kwa wazazi ambao bado hamjapata nafasi ya kuleta watoto wenu katika shule hizi, huu ni wakati sahihi na sehemu sahihi ya kuwapeleka watoto wenu kusoma katika shule za St. Mary’s,” amesema Mgeta

Amesema shule hizo zinaongozwa na wakurugenzi wenye hofu ya Mungu, maadili na upendo kwa watoto, jambo ambalo amesema ni muhimu katika kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kujifunza na kukua.

Kwa mujibu wa Mgeta St. Mary’s inalenga kuhakikisha watoto wanapata elimu bora huku wakipewa malezi yanayowajenga kuwa na maadili mema na kuwawezesha kutumia vipaji vyao kwa manufaa yao na Taifa kwa ujumla.







Matukio mbalimbali katika picha.

NA DENIS MLOWE- DAR ES SALAAM


VICTORIA Group ambao ni waandaaji wa mbio za VG Fun Run 2026 wamesema maandalizi ya tukio hilo yamekamilika kwa asilimia 100 huku washiriki 250 wakitarajiwa kushiriki katika mbio hizo zitakazofanyika siku ya kesho Agosti 8, 2026.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya VG Fun Run, Isdori Msaki, alisema maandalizi yote muhimu yamekamilika na kila kitu kiko tayari kuhakikisha tukio hilo linafanyika kwa mafanikio.

Alisema washiriki watashiriki mbio za kilomita tano na kilomita 10, huku wale wasioweza kukimbia wakipata nafasi ya kushiriki mazoezi ya aerobics kama sehemu ya kuhamasisha afya na mtindo bora wa maisha.

"Tumekamilisha maandalizi kwa asilimia 100. Tunatarajia washiriki 250, huku hadi sasa watu 210 tayari wamethibitisha ushiriki wao. Tunaamini idadi hiyo itaongezeka siku ya tukio," alisema Msaki.

Aliwashukuru wadhamini mbalimbali waliochangia kufanikisha tukio hilo akiwemo wanachama wa Victoria Group, Victoria Finance, Victoria Insurance Brokers, Mayfair Insurance, Elique, Heameda Hospital, IB Solution, CRDB Foundation , Melissa pamoja na Hill Water.

Msaki alisema Heameda Hospital itatoa huduma za afya kwa washiriki wote kupitia madaktari na wauguzi watakaokuwepo eneo la tukio ili kuhakikisha usalama wa washiriki wakati wote wa mbio.

Alisema IB Solution imechangia huduma za ubunifu wa michoro na usimamizi wa mitandao ya kijamii, huku CRDB Foundation ikiwa mmoja wa wadhamini wakuu waliowezesha maandalizi ya tukio hilo kufanikiwa.

Aliongeza kuwa Victoria Group imekuwa na ushirikiano wa muda mrefu na CRDB kwa zaidi ya miaka 26, jambo ambalo limeendelea kuimarisha ushirikiano katika shughuli mbalimbali za kijamii na maendeleo.

Msaki, washiriki wote wanatakiwa kufika eneo la tukio saa 12:00 asubuhi ambapo shughuli zitaanza kwa mazoezi ya kupasha mwili joto kabla ya kuanza rasmi kwa mbio.

Alisema mgeni rasmi wa tukio hilo atakuwa Mtendaji Mkuu wa CRDB Foundation, Tuli Mwambapa, ambaye anatarajiwa kuongoza uzinduzi wa mbio hizo kutokana na mchango wa taasisi hiyo katika kuunga mkono shughuli za kijamii.

Msaki alisema Victoria Group imeendelea kukua kwa zaidi ya miaka 26 ikiwa na wanachama 113, huku ikijumuisha familia zinazofanya jumla ya zaidi ya watu 700 wanaoshiriki shughuli mbalimbali za kijamii na maendeleo.

Aliongeza kuwa pamoja na wanachama wa Victoria Group, viongozi wa serikali, wafanyabiashara, wataalamu kutoka sekta binafsi pamoja na marafiki wa kundi hilo wanatarajiwa kushiriki katika mbio hizo.

Aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo ambalo linalenga kuhamasisha mazoezi ya mwili, kuimarisha afya, kujenga urafiki na kuendeleza mshikamano katika jamii.

"Tunawakaribisha Watanzania wote kushiriki nasi. Mbali na kufanya mazoezi, tukio hili ni fursa ya kuimarisha afya, kukuza urafiki na kuendelea kujenga umoja katika jamii," alisema Msaki.



Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Benki ya Ushirika Tanzania (COOP BANK) imeweka mkakati wa kuongeza tija katika sekta ya kilimo ndani ya kipindi cha miaka mitano ijayo kwa kuwawezesha wakulima kupata teknolojia za kisasa, zana bora za kilimo pamoja na pembejeo zitakazosaidia kuongeza uzalishaji na kukuza kilimo biashara nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Ushirika, Godfrey Ng’urah, amesema benki hiyo imelenga kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo ili kuleta mabadiliko chanya katika uzalishaji, hasa kwa kuwawezesha wakulima na vyama vya ushirika kupata vifaa muhimu vya kisasa kwa gharama nafuu.

Amesema hatua hiyo imeanza kutekelezwa kupitia makubaliano maalum yaliyosainiwa kati ya Benki ya Ushirika na Kampuni ya CMC Agri, taasisi inayojihusisha na utengenezaji na usambazaji wa zana za kilimo, kwa lengo la kuwapatia wakulima, vyama vya ushirika na wadau wa mnyororo wa thamani wa mazao ya chakula fursa ya kupata teknolojia na zana za kisasa kwa mfumo wa malipo ya awamu.

Kwa mujibu wa Ng’urah, ushirikiano huo utarahisisha upatikanaji wa vifaa vitakavyowawezesha wakulima kuongeza ufanisi katika shughuli mbalimbali za kilimo ikiwemo umwagiliaji, upaliliaji, uvunaji, uchakataji, ufungashaji na uhifadhi wa mazao.

Ameeleza kuwa matumizi ya teknolojia hizo yatasaidia kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo pamoja na kuimarisha uwezo wa wakulima kushindana katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

“Tunataka kuona wakulima wanapata zana na teknolojia zitakazowawezesha kuongeza uzalishaji na kuhamia katika kilimo cha kibiashara chenye tija,” amesema Ng’urah.

Aidha, amesema Benki ya Ushirika inalenga kufikia zaidi ya wateja wadogo 10,000 ifikapo mwaka 2030 kupitia huduma mbalimbali za kifedha ikiwemo mikopo na huduma za akaunti, hatua itakayosaidia kuwaunganisha wakulima wengi zaidi na fursa za kifedha.

Amesisitiza kuwa ushirikiano huo ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo katika kuunga mkono jitihada za kukuza sekta ya kilimo na kuwawezesha wakulima nchini kutumia fursa zinazotokana na teknolojia na huduma jumuishi za kifedha.






Na mwandishi wetu, Arusha


MKUU wa wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, Fakii Lulandala amewasihi wakulima, wafugaji na wavuvi kushiriki maonyesho ya kilimo nane nane ili kuongeza ujuzi na kufanya shughuli zao kwa tija.

DC Lulandala ameyasema hayo akizungumza baada ya kukagua baadhi ya mabanda ya maonyesho hayo ya kanda ya kaskazini yanayoendelea katika eneo la Themi jijini Arusha.

Amesema wakulima, wafugaji na wavuvi wakishiriki kwenye maonyesho hayo watapata fursa ya kukutana na wataalamu na kuweza kuongeza ujuzi katika shughuli zao.

"Nawapongeza sekretarieti ya maonyesho haya kwa kuandaa vyema kwani wakulima, wafugaji, wavuvi na wadau wengine wameshiriki na kupata ujuzi, ubunifu na kujifunza upya kufanya shughuli zao za uzalishaji kiuchumi kwa tija," amesema DC Lulandala.

Amesema kilimo, ufugaji na uvuvi ukifanyika kwa kufuata maelekezo ya wataalamu, utafanyika kwa tija na jamii kunufaika zaidi kiuchumi kuliko kufanya kazi kwa mazoea.

"Japokuwa tupo mwishoni mwa maonyesho hayo ya nane nane nawasihi wadau wa kilimo, mifugo na uvuvi kushiriki ili kupata elimu kwa wataalamu juu ya namna ya kuboresha shughuli zao," amesema DC Lulandala.

Mmoja kati ya wajumbe wa sekretarieti wa maonyesho hayo, Samwel Dahaye amemweleza mkuu huyo wa wilaya kuwa watu wengi wamehamasika kushiriki nane nane.

"Maonyesho haya ni ya kanda ya kaskazini kuna wakulima, wafugaji na wavuvi wametoka maeneno mbalimbali ikiwemo Babati na Hanang', Arumeru na Same," amesema.

Mwenyekiti wa chama cha walimu nchini (CWT) wilaya ya Simanjiro, Mwalimu Abraham Kisimbi amesema maonyesho hayo ni mazuri kwani hata wanafunzi wanatembelea kupata elimu mbalimbali.

"Tumeona wanafunzi wa shule tofauti za mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro, wakishiriki maonyesho hayo ya kilimo, mifugo na uvuvi, wakiuliza maswali na kupatiwa majawabu," amesema mwalimu Kisimbi.

Kauli mbiu ya mwaka huu ya maonyesho hayo ya kilimo nane nane ni 'Tambua soko, ongeza tija kutekeleza Dira 2050.


Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda, akipata maelezo kuhusu ubunifu wa ubunifu wa Samani za Majumbani  katika banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) alipolitembelea wakati wa Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda, akipata maelezo kuhusu ubunifu wa zana za kilimo za mashine za Kilimo pamoja na  Ufugaji katika banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) alipolitembelea wakati wa Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda, akipata maelezo kuhusu ubunifu wa mashine ya kuchanganya chakula cha mifugo  katika banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) alipolitembelea wakati wa Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda, akiingalia Asali katika  banda la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) alipolitembelea wakati wa Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

 


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imewataka wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali nchini kutumia elimu ya ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji kama nyenzo ya kuongeza thamani ya bidhaa zao, kupanua masoko na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Hamad Hassan Chande, alipotembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) katika Maonesho ya 33 ya Kilimo ya Kimataifa ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Mhe. Chande amesema elimu inayotolewa na FCC imekuwa na mchango mkubwa katika kuwajengea uwezo wazalishaji na wafanyabiashara kuzalisha bidhaa zenye ubora wa kushindana katika soko la ndani na la kimataifa.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara yanayozingatia ushindani wa haki, fursa sawa kwa washiriki wa soko na ulinzi wa maslahi ya walaji.

"Msingi huo unachochea uwekezaji, huongeza tija katika uzalishaji na kuimarisha mchango wa sekta mbalimbali katika kukuza uchumi wa Taifa," amesema Chande.

Aidha, amewahimiza wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kutumia kikamilifu elimu inayotolewa na FCC kwa kuzingatia sheria za ushindani, kuepuka vitendo vinavyopotosha soko na kujikita katika uzalishaji wa bidhaa bora zinazokidhi mahitaji ya walaji.

Amesema hatua hiyo itaongeza thamani ya mazao, kuinua kipato cha wazalishaji na kufungua fursa zaidi za biashara ndani na nje ya nchi.

Naibu Waziri huyo pia ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kutoa elimu kwa umma kuhusu haki za walaji na ushindani wa haki, akieleza kuwa juhudi hizo zinaimarisha mazingira ya biashara yenye uwazi na usawa kwa manufaa ya wazalishaji na watumiaji wa bidhaa na huduma.

Amesisitiza kuwa Maonesho ya Nane Nane yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuwapa maarifa yatakayowawezesha kuongeza ubora wa mazao na bidhaa zao.

Aidha, ametoa rai kwa FCC kuendeleza kampeni za elimu katika maeneo mbalimbali nchini ili Watanzania wengi zaidi wanufaike na fursa zinazotokana na soko lenye ushindani wa haki na hivyo kuchangia kwa kiwango kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dkt. Aneth Komba leo tarehe 07/08/2026 amefungua mafunzo ya maafisa Elimu kata na wakuu wa shule 868Tanzania Bara kwa njia ya mtandao kupitia Darasa Janja (Smart class).

Akizungumza na washiriki Dkt. Komba amesema,  mafunzo hayo yamelenga utambuzi wa Mkakati wa Kisayansi wa Kumudu Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) na kutoa wito kwa washiriki wa mafunzo hayo kufuatilia kwa makini ili kwenda kusimamia utekelezaji wake.

Ameendelea kusema, TET imejipanga vyema katika utoaji wa mafunzo mbalimbali ili kuwapa wasimamizi wa Elimu na walimu kuweza kupata maarifa yatakaosaidia katika utendaji wao ili kuendelea kuinua kiwango cha Elimu nchini. 

Aidha,  Dkt. Komba amewataka washiriki  kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan za kuboresha elimu nchini zinazoendana na uzinduzi wa mkakati wa KKK alioufanya mwaka 2025.

“Tumeona tutoe mafunzo haya kwanza kuanza nanyi viongozi ili tuweze kuwa katika ukurasa mmoja wa kuelewa mkakati  na kutekeleza dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 ambayo inasisitiza umuhimu wa kila mtoto wa Kitanzania anapata stadi za KKK kama msingi wa kila mtoto katika ushiriki wake katika ngazi  mbalimbali za elimu.”Amesema Dkt. Komba.

Hata hivyo Dkt. Komba ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Tekonolojia  na Ofisi ya Waziri Mkuu , TAMISEMI  kwa kuendelea kuhakikisha inatoa rasilimali fedha katika utekelezwaji wa majukumu mbalimbali ya kielemu.

Jumla ya washiriki  868 wameshiriki mafunzo hayo ya KKK, ambayo yanawezeshwa na  wataalamu wa TET  ambapo yanatarajiwa kuwafikia waratibu elimu wa kata  idadi ya 3000.









Na. Saidina Msangi, WF, Dar es Salaam.

Serikali imezindua Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), hatua inayotarajiwa kuimarisha uwazi wa soko la fedha, kuongeza ufanisi wa maamuzi ya uwekezaji na kuvutia mitaji ya ndani na nje ya nchi.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amezindua Kielelezo hicho katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Bw. Tutuba alisema kupitia Kielelezo hicho wawekezaji wataweza kuona na kufuatilia mwenendo wa faida halisi katika soko la upili la Dhamana za Serikali, jambo litakalowasaidia kufanya maamuzi ya uwekezaji kwa kuzingatia taarifa sahihi na zinazoaminika.

‘‘Kielelezo hicho kitawawezesha wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kulinganisha viwango vya faida vya Dhamana za Serikali ya Tanzania na fursa nyingine za uwekezaji ndani ya nchi, pamoja na masoko ya kikanda na kimataifa, hivyo kuongeza uwazi wa soko, kuvutia wawekezaji wa kigeni na kuimarisha ushindani wa soko la fedha nchini’’, alisema Bw. Tutuba.

Aidha Bw. Tutuba alisema Kielelezo hicho pia kitaakisi matarajio ya soko kuhusu ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei na mwelekeo wa sera ya fedha, hivyo kitakuwa nyenzo muhimu kwa Benki Kuu katika kuimarisha utekelezaji wa sera ya fedha inayotegemea viwango vya riba.

‘‘Soko letu limeshuhudia ukuaji mkubwa katika kipindi cha miaka 25, ambapo mwaka 2001, Dhamana za Serikali ambazo zilikuwa hazijaiva zilifikia shilingi bilioni 499, na kuongezeka mpaka kufikia shillingi trilioni 32.3 hivi sasa’’, alisema Bw. Tutuba.

Vilevile, alisema uthaminishaji wa Dhamana za Serikali zinazowasilishwa na mabenki ya biashara kama dhamana ya kupata mikopo kutoka Benki Kuu utafanyika kwa kutumia kielelezo hicho, hatua inayotarajiwa kuongeza usahihi na uwazi katika shughuli za kifedha.

‘‘Kwa upande wa sekta ya fedha, mabenki, mifuko ya hifadhi ya jamii, makampuni pamoja na wawekezaji binafsi watanufaika kwa kutumia taarifa za kielelezo hicho kama kiwango salama cha rejea katika kupanga viwango vya riba vya mikopo, mikopo ya nyumba, hatifungani za makampuni na bidhaa nyingine za uwekezaji’’, alifafanua Bw. Tutuba.

Bw. Tutuba aliwashukuru wadau wote wa soko kwa ushiriki wao ambao umeiwezesha Serikali kupata fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo kupitia Dhamana za Serikali pamoja na kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050.

Alisisitiza kuwa kuna umuhimu wa Benki Kuu na Serikali kwa ujumla kuendelea kutoa elimu ya uwekezaji ili kuhakikisha soko linaendelea kukua kwa kasi na kuongeza idadi ya wawekezaji kutoka 32,631 walioko sasa kwani idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya watu nchini.

Awali, akizungumza katika tukio hilo, Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, alisema kuwa soko la hisa limeendelea kukua ambapo
katika mwaka wa fedha 2025/26, thamani ya miamala iliyofanyika ilikuwa zaidi ya shilingi trilioni 6.7.

Alisema soko hilo ni fursa muhimu katika kuelekea utekelezaji wa Dira 2050 ambayo sehemu kubwa ya utekelezaji wake inatarajiwa itokane na sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 hususani katika upatikanaji wa kitaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, alisema kuwa Kielelezo hicho kitaongeza miamala na ukwasi katika soko la dhamana na kuchochea maendeleo ya aina nyingine za mali zinazouzwa katika soko la hisa.

Alipongeza Benki Kuu ya Tanzania kwa kuchapisha Kanuni za Marekebisho ya Udhibiti wa Fedha za Kigeni za mwaka 2026 na uzinduzi wa Kielelezo hicho kuwa hatua hiyo itaimarisha zaidi mfumo wa fedha nchini na kuweka mazingira yatakayowezesha Tanzania kuwa na soko la mitaji lenye ufanisi, uwazi na ushindani.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi rasmi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia ni Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine (wa tatu kushoto), Naibu Gavana, Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Yamungu Kayandabila (wa pili kushoto) na Kaimu Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa  Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Nicodemas Mkama.


Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakifurahia baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha Bw. Japhet Justine, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Bw. Nicodemas Mkama, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya washiriki wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, (Katikati, walioketi), wakiwa katika picha ya pamoja na wadau baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam.)