Na Mwandishi wetu
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola ambaye pia ni Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Lazarus McCarthy Chakwera ameondoka nchini Aprili 16, 2026, kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na kuagwa na viongozi waandamizi wa serikali wakiongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mberwa Kairuki, baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi ya siku 9 nchini Tanzania.
Mhe. Chakwera ambaye aliwasili nchini Aprili 8, 2026 kwa ziara ya kikazi, alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mawaziri akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Sera, Bunge, Uratibu Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi ambaye aliongoza ujumbe wa Serikali kukutana na Mjumbe huyo Maalum.
Katika kikao na ujumbe wa Serikali, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mhe. Chakwera, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka msisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.
Kikao hicho na Mjumbe huyo Maalum kilikuwa chenye mafanikio baada ya Mhe. Chakwera kuelezwa namna serikali inavyoendelea kuchukua hatua mbalimbali hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania na kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kumuwezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo.
Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera alifanya mazungumzo na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi, na pia vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.
Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Mjumbe huyo Maalum pia alikutana na wadau mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.
Akiwa nchini, Mhe. Chakwera alipata fursa ya kujionea namna Tanzania ilivyowekeza katika sekta ya usafiri ambapo wakati akienda Zanzibar kukutana na viongozi wa kisiasa kisiwani humo, alitumia usafiri boti ya kisasa inayofanya safari zake katika ya Dar es Salaam na Unguja, wakati akielekea Dodoma alitumia usafiri wa treni ya mwendokasi (SGR) na kufurahia namna Serikali ilivyowekeza na kuimarisha sekta ya usafiri nchini.
Ziara ya Mhe. Chakwera imekuwa ya mafanikio na kuionesha Afrika na dunia hali ya Amani na utulivuza iliyopo nchini Tanzania, licha ya changamoto zilizojitokeza wakati na baada ya uchaguzi mkuu, na namna ambavyo Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kushughulikia changamoto hizo huku ikisimamia misingi ya kuimarisha demokrasia, Amani, utulivu na kuhakikisha kila mtanzania anashiriki vema katika kujenga uchumi na kuifikia Dira 2050 ambapo ifikapo mwaka 2050, Tanzania inalenga kuwa na uchumi wa dola za Marekani trilioni 1, huku kipato cha mtu mmoja mmoja kikizidi dola za Marekani 7,000.
Katika ziara yake hiyo, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola aliwezeshwa kukutana na wadau wote aliohitaji kukutana nao pamoja na wale wote walioainishwa na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola.


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...