Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Mahadhi Juma Maalim (MB) akichangia majadiliano katika Mkutano wa Kamati ya Kwanza na Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa kuhusu silaha za kawaida ( Conventional Weapons) zikiwamo silaha ndogo ndogo na nyepesi Mkutano huo unafanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa. Aliye kaa nyuma yake ni Balozi Mohamed Hamza, Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Nje Zanzibar
Na Mwandishi Maalum
New York
Wakati Jumuia ya Kimataifa ikiendelea kujadialiana, kuvutana na kutokufikia maamuzi ya msingi na madhubuti kuhusu udhibiti wa biashara na matumizi haramu ya silaha ndogo ndogo na nyepesi pamoja na silaha za maangamizi. Maisha ya Mamia ya wanawake, watoto na wanaume yanaendelea kupotea.
Kwa takribani siku tatu mfululizo wiki hii, wajumbe wa Kamati ya Kwanza ya Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa, wamekuwa katika majadialiano yaliyoambatana na upitishaji wa rasimu za maazimio matatu yanayolenga pamoja na mambo mengine. Kutafuta njia muafaka za kudhibiti, kupunguza na kuratibu biashara ya silaha ndogo ndogo na nyepesi, silaha za maangamizi zikiwamo za kibaiolojia pamoja na mabomu ya ardhini, matumizi yake na ulimbikizaji wa silaha hizo.
Karibu kila mjumbe aliyechangia majadiliano hayo, amekuwa akielezea kwa hisia kali namna ambavyo usambaaji wa silaha hizo na matumizi yasiyosahihi yameendelea kuziweka nchi nyingi na raia wake katika hali tete huku pia zikihatarisha uchumi na maendeleo endelevu ya nchi hizo.
Baadhi ya wajumbe walifikia hatua ya kutamka bayana kwamba, je Umoja wa Mataifa ulikuwa unahitaji maazimio mangapi yapitishwe ili itambue kwamba ulimbikizaji ,usambazaji, uuzaji na matumizi haramu ya silaha hizo sasa kunahitaji maamuzi madhubuti ili kunusuru maisha ya watu hasa wale wasiokuwa na hatia.
Akichangia majadiliano hayo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Mahadhi Juma Maalim ( Mb), amewaeleza wajumbe wa mkutano huo kwamba, matarajio ya nchi yake (Tanzania) ni kutoendelea kushuhudia maisha ya watu wasio na hatia yakiendelea kupotea kwa sababu tu dunia imeshindwa kufikia makubaliano juu ya kudhibiti matumizi haramu ya silaha hizo.
“ Ni jambo lililowazi, na hata jumuia ya kimataifa mmekuwa mashahidi,wananchi wetu na wale za nchi jirani kila siku wanaendelea kupoteza maisha kutokana na matumizi mabaya ya silaha hizi. Nchi yangu isingepeda kuendelea kuona maisha ya watu wasio na hatia yanaendelea kupotea” akasema.
Aidha Naibu Waziri amesema tamaa ya madaraka, umaskini na ubinyaji wa misingi ya uhuru na haki mara nyingi vimekuwa chanzo cha matumzi mabaya ya silaha zikiwamo silaha ndogo ndogo na nyepesi.
Mhe. Mahadhi Juma Maalim akasema kuwa ingawa Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na Jumuia za Kikanda zimetumia raslimali nyingi kujaribu kulitafutia ufumbuzi tatizo la kuzagaa kwa silaha, bado ufumbuzi madhubuti haujapatikana na dunia imeendelea kushuhudia matukio ya kutisha.
Akasema ni kwa sababu hiyo, Tanzania inaungana na mataifa mengine katika kusisitiza kwamba Jumuia ya Kimataifa inatakiwa kuungana na kushirikiana ili kulimaliza tatizo la ulimbikizaji, usambazaji na matumizi haramu ya silaha zaina zote zikiwamo ndogo ndogo na nyepesi.
Amesisitiza kwa kusema kwamba Wajumbe wa Kamati hiyo ya Kwanza ambayo jukumu lake kubwa pamoja na mambo mengine ni kusimamia masuala ya amani na usalamana , upokonyaji wa silaha,washirikiane ili dunia iwe mahali salama pa kuishi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Wakati wa Mkutano huo, baadhi ya wazungumzaji wengi wao kutoka nchi za Afrika, Latini ya Amerika na Visiwa vya Carribian walitoa wito wa kutaka nchi zilizoendelea kudhibiti uzalishaji na uuzaji wa silaha hizo ambazo mwisho wa yote huishia katika nchi zinazoendelea.
Aidha wazungumzaji wengine wengi hasa wale wa kutoka nchi za Afrika, wameiomba jumuia ya kimataifa na nchi zilizoendelea kuzisaidia nchi za Afrika katika mchakato wa ukusanyaji na uangamizaji wa silaha haramu hasa zile ndogo ndogo na nyepesi silaha ambazo zimezagaa sana barani Afrika.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...