MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR BALOZI SEIF ALI IDDI AKIMKABIDHI KATIBU MKUU WA WIZARA YA KAZI, UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI NA USHIRIKA BI ASHA ABDALLA FEDHA SH. LAKI SABA ALIZOAHIDI WAKATI WA KILELE CHA WIKI YA UWEZESHAJI.
MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR BALOZI SEIF ALI IDDI AKIZUNGUMZA NA KATIBU KUU WA WIZARA YA KAZI, UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI NA USHIRIKA BI ASHA ABDALLA ALIYEFIKA OFISINI KWA BALOZI SEIF ILIOPO VUGA MJINI UNGUJA.
Othman Khamis Ame - OMPRZ.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema Mipango mizuri ya kuwajengea uwezo wa uzalishaji wajasiriamali wadogo wadogo inaweza kusaidia kupunguza wimbi kubwa la jamii lisilokuwa na ajira.
Balozi Seif alisema hayo hapo afisini kwake Vuga wakati akikabidhi mchango wa shilingi laki saba alizoahidi wakati wa kilele cha wiki ya uwezeshaji zilizofanyika tarehe 3 Disemba hapo wizara ya kazi uwezeshaji wananchi kiuchumi na ushirika Mwanakwerekwe.
Balozi Seif alikabidhi Mchango huo kwa katibu mkuu Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika Bibi Asha Abdulla.
Mchango huo ni kwa ajili ya kusaidia Kikundi cha Vijana wa Sarakasi cha Talent Group cha Mwanakwerekwe kilichopatiwa Shilingi 500,000/- pamoja na Shilingi 2,000/- kwa Bibi Mwandiwe Ali Makame wa Gamba aliyetokea wa pili katika Mashindano ya Mama Shujaa Tanzania.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Wahasiriamali wengi hivi sasa tayari wameshapata mafunzo na ujuzi wa kutosha, lakini kinachohitajika kwa Taasisi husika ni kuwajengea mazingira bora.
Ameipongeza Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika kwa hatua ilizochukuwa katika kusimamia vyema uanzishwaji wa Soko la Jumapili { Sunday Market } hapo Uwanja wa Kisonge Michenzani ambazo ziko katika hatua za mwisho.
Balozi Seif amesisitiza suala la kuendeleza kuwatunza Vijana ambayo tayari wameshajikusanya pamoja katika vikundi tofauti mfano wa Talent Group.
Alisema hatua hiyo inaweza kusaidia kutambua vipaji vyao na kubwa zaidi ni lile suala la kujipatia ajira.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimpongeza Mama Shujaa Tanzania Bibi Mwandiwe Ali Makame kwa jitihada zake zilizopelekea kushinda nafasi ya pili na kuirusha Bendera ya Zanzibar katika Mashindano hayo.
Akitosha shukrani kwa Niaba ya Wizara ya Kazi pamoja na wahusika waliolengwa wa mchango huo Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika Bibi Asha Abdulla alisema mchango huo utawatia moyo wahusika hao katika kuongeza ajira.
Bibi Asha alimueleza Balozi Seif kwamba Maandalizi ya Uanzishwaji wa Soko hilo la Jumapili yamefikia hatua nzuri na linatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 8 Januari mwaka 2012.




Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...