Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete leo amepokea hati za utamblisho kutoka kwa mabalozi watatu wanaoziwakilisha nchi zao hapa Tanzania.Waliowasilisha hati zao leo ikulu jijini Dar es Salaam ni pamoja na Mhe. Hani Bin Abdullah bin Mohamed Mu’minah wa Saudi Arabia, Askofu Mkuu Mhashamu Francisco Mentecillo Padilla wa Vatican, na Mhe.Bi. Judith Kangoma Kapijimpanga wa Zambia.Pichani Balozi mpya wa Vatican nchini, Askofu Mkuu Mhashamu Francisco Montecillo Padilla akiwasilisha hati zake kwa Rais Kikwete.Katikati anayeshuhudia ni Mkuu wa Itifaki Balozi Antony Itatiro.(picha na Freddy Maro).
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, leo Alhamisi, Machi 8, 2012, amepokea Hati za Utambulisho za Mabalozi wa nchi tatu ambao wataziwakilisha nchi zao katika Tanzania.
Katika sherehe fupi iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Rais Kikwete amepokea hati za Balozi Hani Abdullah Mominah wa Saudi Arabia, Askofu Mkuu Francisco Montecillo Padilla wa Vatican na Mheshimiwa Judith Kangoma-Kapijimpanga wa Zambia.
Katika mazungumzo mafupi baada ya kuwa amewasilisha hati zake za utambulisho, Rais Kikwete amemwambia balozi mpya kuwa baada ya Tanzania na Saudia Arabia kufanikiwa kujenga uhusiano wa karibu katika nyanja za kisiasa na kidiplomasia, sasa ni wakati wa kuimarisha uhusiano wa kiuchumi.
Katika mazungumzo yake na Rais Kikwete, Balozi Padilla amemwasilishia Rais ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedict wa 16 ambako kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki duniani amesifu amani, haki, umoja na mshikamano uliojengeka miongoni mwa Watanzania tokea uhuru mwaka 1961.
Rais Kikwete ameshukuru kupokea pongezi na sifa hizo za Baba Mtakatifu na kuongeza kuwa pamoja na majaribio yote bado Tanzania imeendelea kuwa nchi yenye umoja, amani na mshikamano pamoja na kwamba ina makabila mengi, tamaduni tofauti, watu wa rangi mbali mbali na tofauti na imani mbali mbali.
“Yetu ni nchi inayoishi katika amani na mshikamano pamoja na kuwepo kwa tofauti nyingi za makabila, za dini na imani, za tamaduni tofauti “, Rais Kikwete amemwambia Balozi Padilla.
Rais na Kikwete na Balozi Kapijimpanga wa Zambia wamezungumzia hali ya uhusiano nzuri uliopo kati ya nchi hizo mbili na jinsi gani ya kuimarisha zaidi uhusiano huo na jinsi ya kuendelea kushirikiana katika uendeshaji wa miradi ya pamoja.
Mwisho.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
08 Machi, 2012
Hii Vatican ni nchi gain?wadau nisaidieni kujua mipaka yake!
ReplyDelete