Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya iliyopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ndio chombo kilichopewa jukumu la kuratibu masuala yote yanayohusu dawa haramu za kulevya hapa nchini kupitia mikakati yake mikuu miwili ya kuzuia matumizi  na ule wa kuzuia biashara haramu ya dawa za kulevya. 

Ikumbukwe kwamba biashara ya dawa za kulevya ndio huchochea matumizi ya dawa hizo na kuleta athari kwa mustakabali wa Taifa letu kiafya, kijamii, kiuchumi, kisiasa na hata kimazingira.

 Tume ikishirikiana na vyombo vya dola hususani Kikosi kazi cha Kupambana na Dawa za Kulevya imeshuhudia ongezeko la biashara hiyo haramu kutokana na  kiasi kikubwa cha dawa za kulevya kinachokamatwa. Mfano; Takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2011 kilo 264.3 za dawa ya kulevya aina ya heroin zilikamatwa ikilinganishwa na kilo 185.8 zilizokamatwa mwaka 2010 ikiwa ni ongezeko la 42% la kiasi cha heroin kilichokamatwa katika kipindi cha mwaka mmoja tu. 

mtumia madawa ya kulevya
Aidha, mwaka 2011 kilo 126 za dawa ya kulevya aina ya cocaine zilikamatwa ikilinganishwa na kilo 63 zilizokamatwa mwaka 2010, ambalo ni ongezeko la 100%. Ongezeko hili kubwa la ukamataji linaashiria kukua kwa biashara haramu ya dawa za kulevya kunakorahisisha upatikanaji wa dawa hizo na kuchangia kuongezeka kwa idadi ya watumiaji nchini.

Ingawa hakuna takwimu sahihi za watumiaji wa dawa za kulevya nchini, inakadiriwa takribani watu 150,000 hadi 500,000 wanatumia dawa hizo. Aidha, ingawa sehemu ndogo tu ya watumiaji wa dawa za kulevya hufika katika vituo vya afya kwa minajili ya kutafuta tiba kumekuwa na ongezeko mahitaji ya tiba katika vituo mbalimbali vya afya. 

Hali hii inazidi kudhihirisha kuwa pamoja na ongezeko la biashara ya dawa za kulevya matumizi ya dawa hizi nayo yameongezeka. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka 2011 jumla ya watumiaji 4,684 wa dawa za kulevya walihudumiwa katika vituo vya afya vya manispaa na majiji nchini.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. AnonymousJune 23, 2012

    Jamani tuwe tunawanyonga Wafanya Biashara ya Madawa na Wasafirishaji kwa kuwa hawa ndio wabaya zaidi wakati Mateja kama huyo Masikini anayejidunga sindano hapo ktk picha wao ni waathirika tuu wanahitaji msaada wetu.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...