Leo nimesoma katika gazeti moja la Kiswahili kuwa timu ya Azam (Azam FC) wamemfukuza kocha wao baada ya sare mbili mfululizo zikifuatiwa na kufungwa na Simba. 

 Kilichonishtua ni kwamba habari hii nimeiona kama ya kawaida sana. Ufukuzwaji wa makocha umekuwa jambo la kawaida mno, hata nadiriki kusema kuwa umekuwa utamaduni mpya wa klabu zetu za soka. Kwa kweli siamini kuwa hili jambo ni sawa hata kidogo kutokana na hoja zifuatazo:

1. Kocha ni sehemu moja tu ya timu. Katika timu pia kuna wachezaji, viongozi (ambao humtafuta/humsaili kocha), mashabiki, vyama vya soka, n.k. 

Pia kuna vitu vingine kama uwanja, waamuzi, n.k. Ni kweli kuwa hizi timu zetu zikifungwa ama kutoka sare kosa huwa ni la kocha pekee? Uamuzi wa kumfukuza kocha hutokana na uchunguzi ili kubaini tatizo katika mfumo mzima ama hasira kwa vile kocha ndiye mwalimu? 

Kwamba muumini wa dini akienda kinyume na maandiko basi dhambi huwa ni ya kiongozi wa dini? Je, mtoto wa umri wa chini ya miaka 18 akilewa pombe kosa ni lake binafsi, la wazazi/walezi wake, la mmiliki/meneja wa baa, la kampuni ya bia, la sheria za nchi, ama la nani? Kila leo tunasisitizana kuwa "tucheze kama timu", "sisi wote ni kitu kimoja" n.k. kwa maana gani hasa, kwamba tunacheza kama timu ila tukifungwa kosa ni la kocha?

2. Ni timu gani mnazozijua hapa duniani ambazo huwa hazifungwi? Ninachokijua mimi kila timu hufungwa, hata iwe kubwa namna gani? Achilia mbali Azam kufungwa na Simba (timu kubwa nyezie), Simba hiyo hiyo inaweza kufungwa ama kudroo na timu iliyo daraja la tatu. 

Hivi mmeshawahi kutafakari kwa kina hali hiyo husababishwa na nini hasa ama ni suala la ushabiki na kasumba tu kuwa kosa ni la kocha? Huwezi kumuadhibu mwanao eti tu kwa sababu amefeli mitihani, ni lazima utafiti kujua kwanza vitu gani huchangia kumfanya mtoto afaulu kisha upime kama alivipata. 

Pengine hana muda wa kutosha wa kusoma kwa vile anapaswa kufanya kazi kusaidia maisha ya nyumbani, ama kuna wakati akiwa anajiandaa na mitihani alikumbwa na tatizo ambalo lilimuathiri kisaikolojia na kimorali, ama hapati chakula awapo shuleni, n.k. Je, akifeli basi aadhibiwe tu ama apewe pole na msaada anaouhitaji ili afanikiwe kimasomo? 

Iwe ManU, Brazil, Kagera Sugar, Matikiti maji FC, n.k., zote ni lazima zifungwe tu, zitake zisitake! Ni lazima tutafakari upya badada ya kugeuza ufukuzwaji wa makocha kuwa tabia yetu mpya. Tunawaharibia hawa makocha CV zao walizozijenga kwa bidii na muda mrefu kwa ajili ya uvivu wetu wa kufikiria na ushabiki usio na mantiki ya kimaendeleo.

Ni hayo tu kwa sasa.


Mdau, Canada.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 5 mpaka sasa

  1. Zamani nilikuwa sielewi wakati baba yangu ananiambia kuwa mpira wa Tanzania si mpira wa mtu mwenye akili kuufuatilia kwani ni mpira usiokuwa na maendeleo pia wachezaji wake wameshamiri uchawi badala ya vipaji. Jinsi miaka ilivyonizonga na sasa nimekuwa mtu mwenye akili timamu ninayaona aliyokuwa anasema baba yangu. We umeona wapi nchi nzima inatawaliwa na timu mbili tu, kila mwaka simba ama yanga na kama moja kati yao haijatwaa ubingwa basi tambua kuwa wazee wa klabu hiyo wataleta mtafaruku klabuni. Kwa kweli kufuatilia mpira wa Tanzania ni kujipa pressure bure, wachezaji wengi tu wazuri wako mchangani wababaishaji ndo wako simba na yanga. Si ndiyo maana tunafungwa hata na Burundi, wenzetu wanatafuta vipaji sie majina ya uchawi. Mpira ni kipaji kama uchawi ni kidogo sana ila hapa Bongo tumeweka uchawi mbele zaidi ya vipaji. Mie naangalia Man Utd. tu na menchi za nje shauri lenu nyie wapenzi wa pressure (simba na yanga).

    ReplyDelete
  2. Mdau wa canada ningekushauri sana ukatafuta agency ukatafuta kazi ya ubebaji wa box hapo ulipo

    ukitaka kufuatilia sana mambo ya bongo basi chukuwa klm njoo hapa ufuatilie mpira wa bongo

    usijichanganye fanya kazi ndio kilichokupeleka hapo ulipo sisi wabongo hatukusubii wewe, baridi lishaanza hapo TAFUTA KAZI

    ReplyDelete
  3. Anonymous wa Tue Oct 30, 08:57:00 PM 2012, umekua sasa, acha kuropoka usichokijua.

    Tanzania ni Simba na Yanga, RSA ni Orlando Pirates na Kaiser Chiefs, Kenya used to be Gor Mahia na AFC Leopards, Egypt ni Al Ahly na Zamalek, DRC Ni TP Mazembe na DC Motema Pepmbe, Ghana ni Hearts of Oak na Ashanti, Italy Ni Juventus na AC Milan, Spain ni Barcelona na Real Madrid, England ni Manchester United na Chelsea....niendelee??

    Kila ligi duniani hapa ina timu ambazo zipo dominant sasa iwe Simba na Yanga?

    Wewe vipi wewe, ahh!!!!

    ReplyDelete
  4. Samahani mdau wa Tue Oct 30, 09:39:00 PM 2012:
    Unamshambulia jamaa wa Canada kwa vile labda ni mweusi kama wewe lakini mnawakumbatia makocha wazungu waliojaa katika timu zenu kichekesho. Labda umeshau tunaita nini tabia kama hiyo!?,CHUKI, WIVU,KASUMBA. Siyo mtu lazima awe bongo kutoa maoni, au kwa vile hayupo bongo siyo mmbongo. Ndiyo maana mafisadi wanatawala bongo, kwa vile upeo wako mdogo sana.

    ReplyDelete
  5. simpo kwesheni, Azam imefungwa mara ngapi na imefukuza kocha mara ngapi? Kama kafukuzwa manaake hafai, ukimtaka ruksa kumchukua.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...