Usiku wa kuamkia jana Ijumaa Novemba 23, 2012, Wanareli wote nchini na hasa Wafanyakazi wa Kampuni ya Reli Tanzania –TRL wamefikwa na msiba mkubwa kabisa kwa kuondokewa na Mpiganaji asiyekata tamaa katika kutetea maslahi yao  NDUGU  EMMANUEL JOMOLEMA  (pichani) ambaye kiwadhifa katika  Chama cha Wafanyakazi wa Reli Tanzania –TRAWU alikuwa Makamu Mwenyekiti –Taifa
Marehemu ambaye amezaliwa Januari 28, 1967 alijiunga na lililokuwa Shirika la Reli Tanzania –TRC mnamo Januari mwaka 1989 mara baada ya kumaliza elimu ya Kidato cha 4 katika Shule ya Sekondari ya  Shaban Robert ya jijini Dar es Salaam. Baada ya mafunzo ya miaka 3 ( Januari 1989 –Oktoba 1991)   katika Chuo cha Reli Nairobi, Kenya  katika  fani ya fundi Stadi wa Mitambo alihamishiwa katika Chuo cha Reli –Ratco Tawi la Morogoro na kuendelea na mafunzo hayo hadi Oktoba 1992. 
Baada ya kuhitimu  mafunzo hayo Marehemu akaanza kulitumikia Shirika akiwa Fundi Mitambo Stadi hadi pale Oktoba mwaka 2007 alipohamishiwa katika Kampuni ya Reli Tanzania –TRL na kuendelea na utumishi wake hadi mauti yalipomkuta. Kuhusu harakati za kutetea haki za wafanyakazi Marehemu Jomolema alizianza bila ya kuwa na wadhifa rasmi wa Trawu kuanzia 1999 hadi 2002. Mwaka 2002 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Trawu tawi la  Karakana Dar es Salaam hadi mwaka 2011. 
Halikadhalika mnamo mwaka 2005 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kanda ya Dar es Salaam Trawu , wadhifa alioushikilia hadi mwaka 2011 alipochaguliwa katika Wadhifa wa juu wa  Makamu wa Mwenyekiti Trawu.-Taifa. Marehemu akifahamu umuhimu wa kushirikisha wanaharakati wengine katika uongozi wa chama kwa hiyari mwenyewe alijiuzulu nyadhifa za Uenyekiti  wa tawi la Karakana Dar na Kanda ya Dar Trawu.  
 Kimaisha Marehemu alijaaliwa kuoa na ameacha watoto wawili. Marehemu Jomolema alilazwa  katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuanzia Oktoba 16, 2012  akiwa anasumbuliwa na  maradhi ya TB ya Mifupa.
Kwa mujibu wa Ndugu wa Marehemu msiba uko nyumbani kwa Baba wa Marehemu  Mzee  Jomolema  maeneo ya  Mwembe Yanga Temeke jijini Dar es Salaam. 
Ratiba ya Mazishi inaonesha  shughuli za mazishi  zitaanza kesho Novemba 25, 2012 ,  mnamo saa 4 asubuhi mara baada ya kuwasilii mwili wa Marehemu nyumbani. Kwa mujibu wa ratiba kuanzia saa  6 adhuhuri hadi 7:30 waombolezaji watapatiwa chakula na kuanzia saa 7:30 hadi  8:30 utakuwa ni muda wa Ibada. 
Ndugu,  jamaa na marafiki watapata fursa ya kumuaga marehemu kuanzia saa 8:30 mchana hadi saa 9 alasiri. Msafara wa mazishi utaondoka Mwembe yanga kuelekea makaburi ya Kinondoni kuanzia saa 9 alasiri na mazishi yamepangwa kufanyika saa 10 jioni katika makaburi ya Kinondoni ambako  marehemu atapumzishwa katika nyumba yake ya milele ! Bwana Ametoa , Bwana Ametwaa, Jina lake Lihimidiwe- Amina!
  
Imetolewa na Afisi ya  Uhusiano
 Kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa  Kampuni ya Reli Tanzania
Mhandisi Kipallo Amani Kisamfu
Dar es Salaaam
Novemba 24, 2012


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...