Na Geofrey Tengeneza

Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mh. Liberata Mulamula ametoa rai kwa vyombo vinavyohusika kuharakisha mchakato wa kuigeuza Bodi ya Utalii (TTB) Tanzania kuwa Mamlaka ya Utalii Tanzania ili kukiwezesha chombo hili kuwa na uhuru zaidi na uwezo mkubwa katika kutangaza vivutio vya utalii na kusimamia sekta ya utalii nchini.

Hayo yalisemwa na Balozi Mulamula hivi karibuni alipomtembelea Mkurugenzi Mwendeshaji wa Bodi ya Utalii Tanzania Dk. Aloyce K. Nzuki ofisini kwake ili pamoja na mambo mengine kuzungumza namna gani Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani utasaidia juhudi za TTB katika kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania katika soko la Marekani.“Ni muhimu ifike mahali TTB iwe na nguvu kisheria na uwezo zaidi katika kutekeleza majukumu yake bila kuingiliwa au kuwepo kwa migongano, hivyo ni vema mchakato huo wa mageuzi ukaharakishwa” alisema Balozi Mulamula.

Akifafanua zaidi kuhusu suala hilo Dr. Aloyce Nzuki alisema tayari Bodi ya Utalii ilikwishaandaa andiko kuhusu kuigeuza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuwa Mamlaka ya Utalii Tanzania (TTA) na andiko hilo kwa sasa liko Wizarani.

Aidha balozi Mulamula ameipongeza TTB kwa kubuni onesho la utalii liitwalo Swahili International Tourism Expo (S!TE) litakalo kuwa likifanyika kila mwaka mwezi Oktoba ambalo litatumika pia kuonesha utamaduni wa mwambao na kukuza lugha ya Kiswahili.

Ameahidi kuweka kiunganisho (link) cha tovuti ya onesho hilo la S!TE katika tovuti ya Ubalozi. Sambamba na hilo amesema pia kuwa kuanzia mwaka huu ofisi yake ambayo imekuwa ikiandaa na kuratibu safari ya wafanyabiashara mashuhuri wa Marekani kutembelea Tanzania (VIP Safari) sasa itakuwa ikiandaa safari hiyo na kuwaleta wafanyabiashara hao mwezi Oktoba wakati wa onesho hilo la S!TE badala ya utaratibu wa zamani wa kuwaleta wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es salaam maarufu kama Sabasaba.

Ameahidi kuwa ubalozi wa Tanzania nchini Marekani utafanya kila liwezekanalo kusaidia juhudi za TTB katika kuitangaza Tanzania kama eneo zuri la utalii duniani na akaiomba TTB kuendelea kuwapa taarifa mbalimbali za vivutio vya utalii kadri iwezekanavyo ili kuwasaidia kutekeleza azma hiyo.
Mkurugenzi Mwendeshaji wa Bodi ya Utalii Tanzania Dr. Aloyce K. Nzuki (kushoto) akimshukuru Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mheshimiwa Liberata Mulamula (kulia) baada ya balozi huyo kumtembelea ofisini kwake na kuwa na mazungumzo naye.
Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mheshimiwa Liberata Mulamula akiangalia nakala ya andiko kuhusu mapendekezo ya kuigeuza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuwa Mamlaka ya Utalii Tanzania (TTA) ambalo limekwisha wasilishwa Wizarani.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...