Mkurugenzi
wa Sensa na Takwimu za Jamii Bw. Epraim Kwesigabo kutoka Ofisi ya Taifa ya
Takwimu akitoa maelezo ya utangulizi ya
kufungua mafunzo ya Wadadisi na Wahariri wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye
Uwezo wa Kufanya Kazi wa mwaka 2014 yaliyofanyika leo katika ukumbi wa Bene uliopo
Morogoro mjini.
Mkuu
wa Mkoa wa Mororgoro Mhe. Joel Bendera akihutubia wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya
Wadadisi na Wahariri wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya Kazi
wa mwaka 2014 yaliyofanyika leo katika ukumbi wa Bene uliopo Morogoro mjini.
Kaimu
Meneja wa Idara ya Takwimu za Ajira na Bei kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu
akitoa neno la shukrani mara baada ya hotuba ya Mgeni rasmi Mhe. Joel Bendera
(hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Wadadisi na Wahariri wa
madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya Kazi wa mwaka 2014
yaliyofanyika leo katika ukumbi wa Bene uliopo Morogoro mjini.
Juu na chini ni Baadhi
ya Wadadisi na Wahariri wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya
Kazi wa mwaka 2014 wakifuatilia kwa makini hotuba ya mgeni rasmi (hayupo kwenye
picha) wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo yaliyofanyika leo katika ukumbi wa
Bene uliopo Morogoro mjini. Picha zote na Veronica Kazimoto
Na Veronica Kazimoto – Morogoro
Utafiti
wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya Kazi popote pale duniani ni kigezo muhimu sana
kinachotumika katika kupima na kufuatilia mwenendo wa mabadiliko yanayotokea
katika soko la ajira ili kuiwezesha Serikali husika kuboresha Sera na Program
mbalimbali za kukuza ajira nchini.
Hayo
yamesemwa leo na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Joel Bendera wakati akifungua mafunzo
ya Wadadisi na Wahariri wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya
Kazi wa mwaka 2014 yaliyofanyika katika ukumbi wa Bene mjini Morogoro.
“Utafiti
huu mbali na kusaidia kufuatilia mwenendo wa soko la ajira nchini, husaidia pia
kupanga na kufuatilia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kama vile Malengo ya Millennia,
Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025 na Malengo ya MKUKUTA”, amesema Bendera.
Bendera
amefafanua kuwa Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya Kazi utatoa viashiria
kama vile hali ya ajira nchini katika sekta rasmi na isiyo rasmi, kiwango cha
ukosefu wa ajira, kiwango cha ajira isiyo timilifu na ajira mbaya ambayo
ni hatarishi kwa watoto.
Viashiria
vingine ni wigo wa hifadhi ya jamii na hali ya kipato kutokana na ajira,
matumizi ya muda na ajira mpya zilizozalishwa katika kipindi cha kuanzia mwaka
2006 hadi 2013.
Kwa
upande wake Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii Epraim Kwesigabo ambaye
amemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifu ya Takwimu, amesema taarifa za
hali ya soko la ajira zinazotumika kwa sasa bado ni zile za mwaka 2006.
“Takwimu
za ajira zinazotumika sasa hazioneshi hali halisi ya mabadiliko yaliyotokea
katika soko la ajira nchini, kutokana na hali hii Serikali pamoja na wadau wa
maendeleo wameamua kufanya utafiti huu mwaka 2014 ili kupata hali halisi ya
sasa”, amesisitiza Kwesigabo.
Jumla
ya wadadisi na Wahariri 100 wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa
Kufanya Kazi wa mwaka 2014 kutoka kanda ya Pwani na Kusini inayojumuisha mikoa
ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Mtwara na Lindi wanaendelea kupewa mafunzo
juu ya Utafiti huo utakaoanza rasmi mwezi Februari hadi Disemba mwaka huu.
Mafunzo
kama haya yanafanyika katika kanda ya Ziwa, kanda ya Kati, kanda ya Kasikazini
na kanda ya Juu Kusini ambapo ufunguzi rasmi umefanyika jana kwa baadhi ya
kanda na leo katika maeneo mengine.
Mafunzo
haya ya Wadadisi na Wahariri wa madodoso ya Utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa
Kufanya Kazi wa mwaka 2014 yanafanyika mara baada ya kukamilika kwa mafunzo ya
Wakufunzi wa utafiti huo takribani wiki tatu zilizopita.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...