Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Dkt Pindi Chana leo ametembelea Dawati la Jinsia na Watoto la Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Dodoma Mjini kwa lengo la kukagua utendaji kazi wa madawati haya yaliyoanzishwa kwa lengo kushughulikia kesi zote zinazohusiana na unyanyasaji wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto nchini, kama njia moja wapo ya kuboresha utoaji wa huduma bora za ulinzi na usalama kwa watoto na watu wa jinsi zote.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Dkt Pindi Chana ( mwenye suti nyeusi) akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa Dawati la jinsia na watoto la Polisi wilaya ya Dodoma, Kulia kwake ni Mkuu wa Polisi Wilaya ya Dodoma, Thadeus Malingumu na Kushoto kwake ni Mkuu wa dawati la jinsia na watoto mkoa wa Dodoma, ASP Hamida Hiki.
Kamanda wa Polisi Mkoa Wa Dodoma Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi David Misime akitoa Maelezo mafupi kwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Dkt.Pindi Chana (Mb.) (mwenye suti nyeusi) Wakati alipotembelea Dawati la Jinsia na Watoto katika Mkoa wa Dodoma.
Katika taarifa yake, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma alieleza kuwa Mkoa wa Dodoma una jumla ya Madawati 9 yaliyopo katika Wilaya saba za mkoa huo. aliainisha moja ya changamoto za uendeshaji wa Madawati hayo kuwa ni baadhi ya wananchi kutokuwa tayari kutoa ushahidi wakati kesi hizo zinapofikishwa Mahakamani. Hivyo, Mkoa umejipanga kuendelea kuimarisha utoaji huduma kupitia madawati haya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Maendeleo ya Jinsia na Watoto.
Wakati wa Ziara hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Pindi Chana alilisisitiza Wananchi kutumia madawati ya Polisi ya jinsia na watoto kutoa ripoti za matukio yeyote ya unyanyasaji wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto yanayotokea katika jamii zetu. Aidha, alisisitiza kuwa huduma katika vituo hivi hupatikana pasipo malipo yeyote, na hutolewa kwa usiri stahiki.
Jamani Mheshimiwa waziri tembelea na mkoani singida. Manyanyaso kwa wanawake yamezidi. Imefika mahali mwanamke anapigwa na mumewake watu wanaona ni jambo la kawaida maana hata huyo anaepelekewa lalamiko (Mwanyekiti wa kijiji or balozi)katoka kumpiga mkewe. Sana sana kitakachofuata ni mama wa mwanamke kwenda kumkanda maji mwanae kwa kipigo hicho utadhani anaenda kumkalia mzazi......
ReplyDelete