Serikali ya China imekubali kuendesha mafunzo kwa wana michezo 30 wa Tanzania wanaotegemewa kuiwakilisha Tanzania kwenye michezo ya Nchi za Jumuiya ya Madola  Julai 2014. Vilevile Tanzania na China zimekubaliana kuendeleza ushirikiano wa kiuchumi na kidiplomasia unaoendelea kuimarika kila mwaka hususan kwa sasa nchi hizo zinaposherehekea miaka 50 ya ushirikiano. 

Makubaliano hayo yalifanyika wakati Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania na China walipokutana mjini Beijing wiki iliyopita kuzungumzia masuala yanayohusu maeneo ya ushirikiano wa nchi hizi. Mhe. Wang Yi alisema ushirikiano baina ya nchi hizi ni wa kidugu na hivyo Serikali ya China itaendelea kusaidia kwa hali na mali miradi waliyoahidi kwa maendeleo ya Tanzania na watu wake. 

Mhe. Membe ambaye alikuwa nchini China kwenye ziara ya siku tano, aliahidi kuratibu Wizara na Taasisi za Serikali  zinahusika na miradi ya ushirikiano ili kuhakikisha matunda ya miradi hiyo yanaonekana. Mhe. Membe alisema China ni marafiki wa Afrika lakini ni marafiki wa karibu wa Tanzania hivyo sherehe za miaka 50 ya uhusiano huo zidhihirishwe na miradi ya mafanikio ambayo nchi zote mbili zimekubaliana kwa maendeleo ya watu wake.

Mbali na misaada ya vifaa mbalimbali vya ujenzi na huduma za maji na afya, hadi sasa Serikali ya China imekamilisha miradi mikubwa ya ujenzi wa Ukumbi wa Mikutano wa Mwalimu Nyerere, ukarabati wa Uwanja wa Amaan Zanzibar, ujenzi wa Kituo cha Utafiti wa Kilimo Ifakara na ujenzi wa shule mbalimbali. Miradi mingine kadhaa inaendelea sasa ukiwemo mradi mkubwa wa ujenzi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es salaam. Miradi mingine mingi iko kwenye majadiliano kama vile ujenzi wa jengo la Wizara ya Mambo ya Nje, awamu ya pili ya Mkongo wa Taifa, Nishati ya Umeme wa Upepo Singida, Bandari ya Mbegani Bagamoyo na ukarabati wa Reli ya TAZARA. 

Akiwa kwenye ziara hiyo, Mhe. Membe pia alikutana na Makamu wa Rais wa China Mhe. Li Yuanchao ambaye alielezea China inaitazama Tanzania kama mshirika mwenza kwenye maendeleo, hivyo uhusiano wa nchi hizo una manufaa sawa kwa pande zote mbili. Alisema ukuaji wa uchumi wa nchi nyingi za Kiafrika umesababisha Serikali yake kushawishi wawekezaji wengi kuwekeza Afrika, lakini hali ya usalama na utulivu nchini Tanzania inawavutia wengi kuwekeza zaidi huko.

Mhe. Membe na ujumbe wake pia walikutana na kufanya mzungumzo na Makamu Waziri wa Biashara Mhe. Li Jinzao ambapo aliainisha miradi mbalimbali inayotekelezwa na China kwa sasa. Mhe. Jinzao alisema mbali na miradi mingi inayoendelea kwa sasa mradi wa kukarabati Reli ya TAZARA unapewa kipaumbele na Serikali ya China kwani ndio mradi wa kwanza baina ya nchi hizi mbili.

Katika mazungumzo yake na Makamu Waziri wa Usalama wa Raia Mhe. Wang Hanning, Waziri Membe alipendekeza kuanzisha ushirikiano wa karibu baina ya Wizara ya Usalama wa Raia China na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Tanzania ili kusaidiana katika kutatua changamoto mbalimbali za kiuhalifu duniani. Mhe. Hanning alikubali pendekezo hilo na kueleza kuwa kwa sasa uhusiano wa wananchi wa nchi mbili umeimarika, kuna raia wengi wa China nchini Tanzania na kinyume chake. Hivyo ni wakati muafaka kwa Wizara hizo mbili kuanza ushirikiano wa karibu kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili. 

Mhe. Membe na ujumbe wake pia walifanya mikutano na Makamu Meya wa Jiji la Shenzhen Bw. Chen Biao na Makamu Gavana wa Jimbo la Guangdong Bibi Zhao Yufang na ujumbe wa Serikali ya Guangdong. 

Waziri Membe alimalizia ziara yake kwa kukutana na viongozi mbalimbali wa biashata na makampuni ya sekta binafsi ambao wengi wao ndio wahusika wa miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini Tanzania kwa ushirikiano na China. 

Imetolewa na: KITENGO CHA MAWASILIANO YA SERIKALI, WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA,
DAR ES SALAAM
                      5 MACHI, 2014

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...