KAMPUNI ya Haak Neel Production kwa kushirikiana na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), imezindua rasmi Siku ya Msanii Tanzania itakayoenda sambamba na utoaji tuzo kwa kwa wasanii na wadau wanaotoa mchango katika sanaa ili kuenzi, kuhamasisha, kukuza na kuendeleza vipaji vyao.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika Jumamosi usiku katika Hoteli ya Sea Cliff, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukanagara, alisema Siku ya Msanii ni programu iliyobuniwa na Basata mwaka 2008 lakini ilishindikana kutekelezeka kutokana na ufinyu wa bajeti na kukosekana mtu wa kuendesha mradi huo ambaye angeweza kuingia ubia na Basata kama ilivyo kwa Tuzo za Muziki Tanzania.

“Nichukue fursa hii kuwapongeza Kampuni ya Haak Neel Production pamoja na Basata kwa kubuni na kufanikisha uzinduzi wa Siku ya Msanii, lakini program hii itatuwezesha kuungana na wenzetu duniani kuadhimisha ‘Siku ya Kimataifa ya Msanii’ ambayo huadhimishwa kila Oktoba 25,” alisema.

Alisema Wizara inataka wasanii kujituma na kuzalisha kazi bora zitakazotambulika ndani na nje, kutokana na kuwepo Siku ya Msanii.

Alisema amefurahishwa na fursa ambazo zimeelezwa kuwepo katika Siku ya Msanii kama semina, uwepo wa tuzo, ambazo zitaonyesha utambuzi wa kazi za wasanii.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Haak Neel Production, Emmanuel Mahendeka, alisema Siku ya Msanii ni fursa nzuri kwa wasanii kuona na kujifunza kutoka kwa wenzao na hivyo kuboresha kazi zao na Taifa kwa ujumla.

“Uhai wa sanaa yoyote inategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa kurithishana kutoka kizazi hadi kizazi, ni matumaini yangu Siku ya Msanii itasaidia sana kujenga misingi imara na endelevu ya kurithisha sanaa katika jamii zetu,” alisema.

Naye Kaimu Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mungereza, alisema baraza hilo limekuwa likibuni miradi mbalimbali kwa lengo la kuleta maendeleo ya sanii nchini na kushirikiana sekta binafsi katika kuendeleza sanaa na utamaduni na ndio maana wameshirikiana na Haak Neel Production ili kuendeleza sanaa.

Tuzo zitakazotolewa ni Sinema bora yenye ubunifu halisia na vionjo vya Kitanzania, kikundi bora cha sanaa za maonyesho kinachochipukia, Mpigaji mahiri wa ala za asili za muziki , Mbunifu wa mitindo ya mavazi yenye vionjo vya Kitanzania, Msanii chipukizi anayeibukia, Msanii aliyetoa mchango mkubwa katika jamii na Msanii aliyetumia maisha yake vkatika sanaa.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, akipiga Gitaa kuashiria uzinduzi wa siku ya Msanii katika hafla iliyofanyika kwenye hoteli ya Sea Cliff Dar es Salaam.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk Fenella Mukangara akipokea zawadi ya picha aliyochorwa na msanii chipukizi, Meddy Jumanne wakati uzinduzi wa sherehe ya Siku ya Msanii uliofanyika mjini Dar es Salaam.
Meneja wa Masoko wa Siku ya Msanii, Catherine Metili (kulia) akiwa na ofisa Masoko wa Mradi, Veronica Martin (kushoto) wakiangalia kitabu cha wageni wakati wa uzinduzi wa Siku ya Msanii.
Mkurugenzi wa Utamaduni, Profesa Hermas Mwansoko akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Sihaba Juma wakifuatilia tukio la Siku ya Msanii.
Wageni walialikwa wakimesimama kutoa heshima kwa wasanii mbalimbali waliofariki katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita.
Mkurugenzi wa Haak Neel Production, Sebastian Mahendeka akizungumza wakati wa uzinduzi wa Siku ya Msanii.

Burudani ya Ngoma ya Asili.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...