Na Profesa Mbele
Kila mwaka, tangu mwaka 2007, nahudhuria tamasha la Afrifest, ambalo hufanyika hapa Minnesota, Marekani.
Imewahi kutokea kwamba nilikuwa Tanzania wakati wa tamasha hilo. Binti zangu wananiwakilisha.Wanafahamu vizuri shughuli zangu, na wanawaeleza watu wanaoulizia kuhusu shughuli zangu na vitabu vyangu.
Hapa naonekana nikiwa na mama mmoja aliyekuja kwenye meza yangu. Nilimweleza yale aliyoulizia. Hata hivi, kwa kumwangalia usoni, hakuonekana anavutiwa na yale niliyokuwa nasema. Niligundua hatimaye kuwa dhana yangu haikuwa sahihi, kwani, bila mimi kutegemea, alitoa pochi yake, akalipia vitabu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales.Baada ya kuchukua hivyo vitabu, akajiondokea zake, kimya kimya. Nilizidi kuamini kuwa huyu mama sio mzungumzaji sana.
Mwaka huu, Afrifest itafanyika North View High School katika mji wa Brooklyn Park, Minnesota, tarehe 2 Agosti. Lakini shughuli za mwanzo zitafanyika siku moja kabla, yaani Agosti 1, kama unavyoona katika tangazo hapa chini. Kwa taarifa zaidi, tembelea www.afrifest.org
Shughuli kama Afrifest ni fursa ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia na tamaduni mbali mbali kukutana. Naamini kuwa kwa watu wazima, vijana, na watoto, hii ni elimu bora kabisa.Hapa kushoto Zawadi anaonekana akiwa na watu wawili kutoka visiwa vya Caribbean.
Hizi "ti-sheti" tulizovaa zina nembo ya kikampuni changu kiitwacho Africonexion: Cultural Consultants, ambacho najaribu kukijenga.
Hapa anaonekana Zawadi, binti yangu wa mwisho, akiwa anangojea watu. Hapo ni wakati alipokuwa mdogo. Alianza kuipenda shughuli hii tangu alipokuwa mdogo sana. Alikuwa akifuatana nami kwenye matamasha ya utamaduni, akinisikiliza ninapoongea na watu. Tangu akiwa na umri ule mdogo, aliweza kuwaeleza watu kuhusu shughuli zangu na kuhusu vitabu vyangu. Kwa mfano, katika mji wa Faribault kulikuwa na tamasha la tamaduni, nami nikiwa Tanzania. Zawadi alihudhuria mwenyewe. Alihojiwa na gazeti la Faribault News, akatoa maelezo vizuri kabisa.
Hapa anaonekana Deta, binti yangu wa kwanza. Siku hiyo sikuwepo.
Congratulations Prof. nimependa sana hiyo shughuli yako na unavyojaribu kuwarithisha watoto wako pia...hongera sana.
ReplyDeletemdau wa London
Asante, ndugu anonymous, kwa ujumbe wako. Sina la kuongeza, ila ukipita pita kwenye blogu zangu na mtandaoni kwa ujumla, utaona zaidi kuhusu shughuli hizi. Ukienda YouTube, utafute jina langu na Afrifest, utanisikia nikiongea kirefu kiasi. Kila la heri.
ReplyDelete