Ujumbe kutoka Tanzania ukiongozwa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Kitwanga (wa kwanza kushoto), ukimsikiliza Bw.Stephen Flewelling (aliyesimama), Mtendaji wa kampuni ya Glancore yenye leseni ya kuchimba Nickel katika eneo la Kabanga wilayani Ngara wakati walipofika katika makao makao makuu ya kampuni hiyo yaliyoko Toronto, Canada. Wengine katika picha ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa (Mb.), (wa pili kushoto), Deogratias Ntukamazina (Mb.) (wa tatu kutoka kushoto), Murtaza Mangungu (Mb.) (wa nne kutoka kushoto) pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na Madini.
Serikali kwa kushirikiana na baadhi ya wabunge wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania wameitaka kampuni ya Glancore yenye umiliki wa leseni ya
uchimbaji madini ya Nickel katika mgodi wa Kabanga kuacha kusuasua
katika utekelezaji wa mradi huo.
Hayo yalisemwa na ujumbe wa Tanzania ulioongozwa na Naibu Waziri
wa Nishati na Madini, Charles Kitwanga wakati ulipokuwa katika makao
makuu ya kampuni hiyo yaliyoko Toronto nchini Canada.
Naibu Waziri aliwaeleza watendaji hao kuwa utekelezaji wa mradi huo wa
uchimbaji madini aina ya Nickel katika eneo la Kabanga wilayani Ngara
umechukua muda mrefu kuanza hivyo kuleta shaka kwa wananchi juu
ya nia ya kweli ya kampuni hiyo kuanza uchimbaji wa madini hayo nchini
Tanzania.
"Wananchi walikuwa na matarajio makubwa juu ya mradi na walikuwa
tayari kulipwa fidia ili kupisha ujenzi wa miundondombinu ya utekelezaji
wa mradi na hawajaendeleza maeneo yao kwa muda mrefu, na serikali
pia kwa upande wake iliweka mtambo wa kuzalisha umeme wa megawati
60 jijini Mwanza ambao pamoja na kuhudumia wananchi pia umeme huo
utatumika katika kuendesha mgodi wa Nickel lakini mnachukua muda
mrefu kutekeleza”. Alisema Naibu Waziri.
Agizo hilo la wabunge na Serikali limekuja baada ya Mtendaji wa kampuni
ya Glancore Bw. Stephen Flewelling kuueleza ujumbe huo kwamba
uchimbaji wa madini ya Nickel katika mgodi wa Kabanga unaweza kuanza
kati ya mwaka 2018 na 2020.
Bw. Fleweling alieleza kuwa katika kipindi cha hivi karibu bei ya Nickel
duniani imeshuka mpaka kufikia chini ya Dola 6 za Marekani kwa pound
hivyo kampuni inaona muda muafaka wa kuendeleza mradi huo haujafika
hadi hapo bei ya madini itakapopanda katika soko la dunia.
Naye Mbunge wa Ngara, Deogratias Ntukamazina, aliwaambia watendaji
wa kampuni ya Glancore kuwa mradi huo ulianza miaka ya 1970 ambapo
kampuni mbalimbali zilikuwa zikijaribu kuwekeza kwenye mradi huo
bila mafanikio hata hivyo baada ya kampuni ya Glancore kuja Tanzania
wananchi wanaozunguka eneo la mradi walianza kuwa na matumaini kuwa
uchimbaji wa madini hayo ungeanza na kutoa kila aina ya ushirikiano ili
kufanikisha utekelezaji wa mradi huo.
" Watu walikuwa na matumaini lakini mwaka 2008 mradi ukawa kama
umesimama na ilipofika mwaka 2010 matumaini yakarudi tena baada ya
bei ya Nickel duniani kupanda na wananchi kutoka kipindi hiki waliambiwa
wasilime mazao ya kudumu kwa vile watahamishwa pindi utekelezaji wa
mradi utakapoanza, na serikali kwa upande wake imekuwa ikihakikisha
kuwa masuala muhimu yanayohitajika kwenye mradi huo yanatekelezwa
ikiwamo ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji na upatikanaji wa umeme
wa uhakika"alisema Mbunge wa Ngara.
Mhe. Ntukamazina alieleza kuwa mwaka 2014 kampuni hiyo ya Glancore
ilimpa taarifa kuwa bei ya madini ya Nickel duniani imeshuka kutokana nchi
ya China ambayo ndiyo soko kubwa la Nickel kuanza kuzalisha "Nickel Pig
Iron" ambayo ina matumizi sawa na Nickel jambo linalosababisha mradi
huo kuchelewa na hivyo kuleta wasiwasi wa utekelezaji wa mradi huo.
Akitoa ufafanuzi kuhusu masuala yaliyoelezwa na Naibu Waziri Kitwanga
na Wabunge, Mtendaji wa kampuni ya Glancore alieleza kuwa mradi
wa Kabanga haujafa kwa kuwa tayari wameshawekeza zaidi ya Dola za
Marekani milioni 260 ila changamoto kubwa ni kushuka kwa bei ya madini
ya Nickel katika soko la Dunia na kwamba bado wanaamini kuwa mradi
huo una manufaa kwao na kwa Tanzania.
"Ingawa mradi huo haujaanza kutekelezwa, mawasiliano na wananchi
yanaendelea ili kutoa elimu juu ya maendeleo na hatua stahiki
tunazochukua kuhusu utekelezaji wa mradi huu ili wananchi hawa
wasikose matumaini katika kipindi hiki cha mpito." Alisema Bw. Flewelling.
Kuhusu suala la wananchi wa Kabanga kuendeleza maeneo yao alieleza
kuwa wananchi wameruhusiwa kuendeleza maeneo hayo mpaka hapo
utekelezaji wa mradi utakapoanza rasmi na masuala ya ulipaji fidia kuanza
ambapo jumla ya Dola za Marekani milioni 70 zinategemewa kutumika.
Naye Naibu Waziri Kitwanga aliwaeleza watendaji hao kuwa serikali
sasa inaangalia maendeleo ya nchi na kwamba haihitaji wawekezaji
wanaoshikilia maeneo kwa muda mrefu bila kuyaendeleza hivyo inahitaji
kuona eneo hilo likiendelezwa na si vinginevyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...