Serikali ya Tanzania inatarajia kutuma wataalam kwenda nchini Canada katika Kamisheni ya Mafuta na Gesi ya jimbo la British Columbia (BC Oil& Gas Commission), ili kupata uelewa zaidi katika masuala ya udhibiti wa mafuta na gesi nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini anayeshughulikia Nishati, Charles Kitwanga wakati akiongea na watendaji wa Kamisheni ya Mafuta na Gesi ya Jimbo la British Columbia katika Ofisi za kamisheni hiyo zilizo katika mji wa Victoria nchini Canada.

Akiongoza ujumbe wa Tanzania uliotembelea Kamisheni hiyo ili kujifunza masuala ya udhibiti wa sekta ndogo ya gesi asilia, na mafuta, Naibu Waziri alisema kuwa lengo la serikali ya Tanzania ni kuhakikisha kuwa rasilimali zilizopo zinaendelezwa na faida yake kuonekana kwa wananchi hivyo wataalam watakwenda nchini Canada katika Kamisheni hiyo ili kuongeza uelewa katika masuala ya udhibiti ambao kwa kiasi kikubwa unachangia katika kuhakikisha kunakuwa na maendeleo endelevu ya rasilimali zilizopo Tanzania.

" Mtazamo wa wananchi wengi ni kuwa makampuni ya kigeni yanakuja nchini Tanzania kuchukua rasilimali na kuondoka nazo bila wananchi hao kufaidika hivyo serikali inafanya kila jitihada ili faida za rasilimali zetu ziwafikie wananchi wote na moja ya vigezo vya jitihada hizo ni kuwa na mamlaka madhubuti za udhibiti zitakazohakikisha makampuni ya nje na ndani ya nchi yanafanya kazi kwa kuzingatia kanuni na sheria zinazoongoza sekta husika" alisema Kitwanga.

Naibu Waziri alieleza kuwa Tanzania ikiwa katika mchakato wa kutengeneza sheria na kanuni zitakazoongoza sekta ya gesi asilia na mafuta, inahitaji kupata maoni na uelewa zaidi kutoka katika nchi zilizopiga hatua katika uendelezaji wa rasilimali hizo ikiwemo jimbo la British Columbia ambalo limegundua gesi asilia kiasi cha zaidi ya futi za ujazo trilioni 2900.

Naye Ofisa Mkuu wa Operesheni katika Kamisheni ya Gesi na Mafuta ya British Columbia, Mhandisi Ken Paulson alieleza kuwa Kamisheni hiyo ambayo imeanzishwa zaidi ya miaka 15 iliyopita ina jukumu la kudhibiti shughuli zote za mafuta na gesi asilia ikihusisha, utafiti, uendelezaji na usafirishaji wa rasilimali hizo kwa njia ya bomba.

Mhandisi Paulson alieleza kuwa Kamisheni hiyo pia ina jukumu la kukusanya takwimu za kijiolojia zinazotumika katika shughuli za utafutaji wa gesi asilia na mafuta na kuzitangaza kwa njia ya tenda ili makampuni yanayohitaji kufanya shughuli za utafutaji mafuta na gesi katika jimbo hilo yanunue takwimu hizo kutoka Kamisheni hiyo.

Kuhusu matumizi ya gesi asilia, Afisa Mkuu wa Operesheni aliueleza ujumbe huo kutoka Tanzania kuwa asilimia 15 ya kiasi cha gesi kilichogunduliwa katika jimbo hilo kinatumika ndani ya jimbo la British Columbia kwa matumizi mbalimbali na kiasi kinachobaki kinasafirishwa kwenda bara la Amerika Kaskazini.

" Ingawa tunasafirisha gesi kwenda Amerika Kaskazini, mahitaji ya soko hilo yanashuka kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa gesi nchini Amerika, hata hivyo tumejipanga kukabiliana na hali hiyo kwa kutumia gesi hii kwa masuala mengine ikiwemo kuzalisha methano, matumizi ya majumbani na kutumika katika vivuko ambavyo vitakuwa vinatumia mafuta na gesi" alisema Mhandisi Paulson.

Kuhusu mfumo wa ugawanaji mapato (PSA) kati ya makampuni ya utafutaji na uchimbaji gesi asilia na mafuta, Bw. Mhandisi Paulson alieleza kuwa kampuni ikianza uzalishaji wa gesi au mafuta, serikali ya jimbo hilo hukusanya mrabaha wa asilimia 10 hadi 20 ya Mapato.

Katika ziara hiyo ya mafunzo nchini Canada, Naibu Waziri Nishati na Madini ameambatana na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Victor Mwambalaswa pamoja na baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo akiwemo, Murtaza Mangungu (Mb.), Raya Ibrahim (Mb.), Richard Ndasa (Mb.), Deogratias Ntukamazina(Mb.), Shafin Sumar (Mb.) na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na Madini.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Kitwanga (wa tatu kutoka kushoto), Mwenyekiti Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa (wa pili kutoka kushoto) na Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa (wa kwanza kushoto) wakimsikiliza Eng. Ken Paulson, Afisa Mkuu wa Operesheni katika Kamisheni ya Gesi na Mafuta ya Jimbo la British Columbia nchini Canada mara walipofika katika Kamisheni hiyo ikiwa ni sehemu ya ziara ya mafunzo kwa ujumbe huo katika sekta ya uziduaji.
Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (wa kwanza kushoto) akieleza kitu katika mkutano kati ya watendaji wa Kamisheni ya Gesi na Mafuta ya Jimbo la British Columbia nchini Canada pamoja na ujumbe kutoka Tanzania ukiongozwa na Naibu Waziri Nishati na Madini, Charles Kitwanga (wa tano kutoka kushoto).Wengine katika picha ni Mwenyekiti Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa (wa nne kutoka kushoto) Mbunge wa Ngara, Deogratias Ntukamazina (wa pili kutoka kushoto), Richard Ndasa (Mb. Sumve), (wa tatu kutoka kushoto), Raya Ibrahim (Mb.) (wa pili kutoka kulia) pamoja na watendaji kutoka Wizara ya Nishati . Katikati ni Eng. Ken Paulson, Afisa Mkuu wa Operesheni katika Kamisheni ya Gesi na Mafuta ya Jimbo la British Columbia nchini Canada.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...