Na Rose
Masaka
WAZIRI wa Fedha Bi. Saada Mkuya amefanya
ziara yake ya kikazi katika Wilaya za Mkoa wa Dar es Salaam ili kupata taarifa za makusanyo ya kodi za
majengo ikiwa ni eneo moja kati ya maeneo sita ambayo yamepewa kipaumbele
katika suala la ukusanyaji wa kodi kama vile eneo la kilimo na miundombinu.
Bi. Saada Mkuya aliahidi kufanya
ziara hiyo katika kikao kilichofanyika wiki iliyopita baada ya kurudisha zoezi
la ukusanyaji wa kodi za majengo katika Serikali za Mitaa ili kuona kinachoendelea,
kupata uhalisia na changamoto zinazowakabili watendaji wote wa Manispaa ya
Ilala, Kinondoni naTemeke.
“Tumerudisha makusanyo ya kodi za
majengo kwenye mitaa kwasababu ni rahisi na wanajua nyumba zote” alisema Bi. Mkuya.
Kodi ya majengo imekuwa ni moja ya
chanzo kikubwa kinachotegemewa na Halmashauri za wilaya zote za Mkoa wa Dar es
Salaam. Serikali iliona hili mnamo mwaka 2013 na kuteua chanzo hiki kuwa mfano
katika mpango wake wa matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Kwa upande wake Mweka hazina wa Wilaya
ya Ilala Bw. Stima Kabikile amesema kuwa Halmashauri ya Illala kupitia kitengo
chake cha uthamini kwa kushirikiana na viongozi wa kata na mitaa wamejiwekea
malengo ya kuyatambua majengo 10,000 ambayo hayakuwepo katika jedwali la awali
kwa kutumia njia rahisi ya haraka ya uthamini.
“Tumeweza kubaini na kuongeza idadi
ya majengo 6,820 kati ya 10,000 tuliyokadiria yenye thamani ya Shilingi bilioni
989.6 yenye tozo ya kiasi cha shilingi trilioni 1.5 na kuweka kwenye mfumo
tayari kwa malipo”. Alisema Bw. kabikile.
Mtaalamu wa kodi za majengo Wilaya ya
Ilala Bw. Joseph Kawiche amesema kuwa kila mmiliki wa nyumba hulipa kutokana na
asilimia zake ingawa kuna baadhi ya watu ambao hawajaona umuhimu wa suala hili
na kuwa wanafichiana majina,kwa hiyo wameona ni vizuri kutumia njia mbadala ya
picha ili kuwabaibni wanaokwepa kulipa kodi.
Kwa upande wa Manispaa ya Kinondoni, Mstahiki
Meya wa Wilaya hiyo Bw. Yusuph Mwenda amesema kuwa ameona umuhimu mkubwa wa
kutumia Serikali za Mitaa na kutoa matangazo kwenye vyombo vya habari na vipaza
sauti ili kujenga uelewa kwa wananchi
kuhusu kulipa kodi za majengo.
“Wenyeviti wa mitaa 171,watendaji wa Kata
34 na Watendaji wa Mitaa 171 wanashiriki na kuainisha majengo yaliyoachwa
wakati wa uthamini”. Alisema Mwenda.
Mkurugenzi wa wilaya ya Kinondoni Mhandisi
Mussa Natty amesema kuwa jumla ya Shilingi bilioni 1.1 zimekwishakusanywa
katika majengo 3123,aidha majengo 3120 yaliyobakia yenye wigo wa kodi bilioni
1.4 yao katika hatua nzuri ya ulipaji.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Manispaa ya Temeke amesema kuwa Halmashauri imekusanya kiasi cha shilingi
milioni 165.7 kutokana na majengo ambayo awali hayakuwepo katika daftari la
majengo ambapo mapato yanatarajiwa kuongezeka kwa hali ya juu katika mwaka huu
wa fedha baada ya majengo yote 10,000 kuthaminiwa.
Baadhi ya changamoto zinazozikabili Wilaya
hizo ni pamoja na waraka wa msamaha wa kulipa kodi ya majengo wakati sheria ipo
kimya wakati wanamiliki majengo ya makazi,kupangishana biashara ambao raia na wanajeshi wastaafu wanao,pia
shule binafsi kudai kutoa huduma wakati ada zao zipo juu, hivyo Manispaa zote
tatu zimetoa wito kwa wananchi wa Tanzania kulipa kodi kwa hiari na Serikali iweke
wazi sheria za misamaha kama zipo.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Manispaa ya (kulia) Ilala akimsomea taarifa ya makusanyo ya kodi za majengo na
mikakati yake ya kufikia malengo waliojipangia ili kuongeza mapato Mhe.
Waziri wa Fedha Bi. Saada Mkuya wakati wa ziara ya siku moja katika Manispaa za
Ilala, Temeke na Kinondoni.
Waziri wa Fedha, Mhe. Saada Mkuya
akipitia moja ya taarifa alizopewa na uongozi wa Halmashauri wilaya ya Kiondoni
wakati alipofanya ziara yake ya siku moja ofisi hapo.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni
Bw. Yusuph Mwenda (kulia) akitoa maelezo yake kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Saada
Mkuya (kushoto) wakati wa mkutano na viongzoi wa Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Waziri
wa Fedha, Mhe. Saada Mkuya akitoa hotuba fupi yenye kuwaelekeza viongzoi wa
Manispaa ya Temeke huku akiwasisitizia kutumia mifumo ya TEHAMA katika kuleta
ufanisi ukusanyaji kodi kama njia rahisi inayowasaidia walipaji kodi kutopata
usumbufu wakati wa ulipaji.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...