Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Bi.Jane Mutagurwa
akiwasisitiza Wataalam katika Sekta ya Kilimo, Mifugo, Afya, Elimu na Utawala wa kata
ya Mwamalasa, Masanga na Langana Wilayani Kishapu wakati akifungua mafunzo ya
jinsi ya kutekeleza Mradi Wa Kuijengea Jamii Uwezo wa kupunguza Athari Za Maafa
katika kata zao, mafunzo hayo yanaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu
wa Maafa kwa Tarehe 1-5 Septemba, 2014. (Kulia) ni Mratibu Maafa Ofisi ya Waziri
Mkuu Bw. Harison Chinyuka (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Bi.Jane Mutagurwa
amesema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu inaweza kupunguza athari za maafa
ya ukame ikiwa Wataalam katika Sekta ya Kilimo, Mifugo, Afya, Elimu na Utawala wa
kata ya Mwamalasa, Masanga na Langana Wilayani Kishapu watashirikishwa katika
Kuijengea Jamii Uwezo wa kupunguza Athari Za Maafa katika kata zao.
Akiongea wakati akifungua mafunzo ya kuijengea uwezo jamii wa kuzuia, kupunguza
na kukabiliana na maafa yanayotokana na ukame kwa Wataalam waliopo katika Ngazi
ya Kata yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa Maafa kwa
Tarehe 1-5 Septemba, 2014, wilayani Kishapu, Mutagurwa alibainisha kuwa kupitia
mafunzo hayo wataweza kuvieimisha vikundi vya kata zao husika juu ya kuzuia,
kupunguza na kukabiliana na maafa yanayotokana na ukame.
“Katika mafunzo haya nimeambiwa mtafundishwa matumizi ya Taarifa za Hali ya
Hewa, Dhana ya Maafa ikiwa ni pamoja na Sera na sheria ya maafa, namna ya
kubainisha viashiria vya upungufu wa chakula, tathmini ya upungufu wa chakula pia na
mwongozo wa ugawaji wa chakula cha msaada. Napenda niwasihi tumieni fursa hii ya
mafunzo haya vizuri ili muweze kuwaelimisha wananchi wa Wilaya yetu namna bora ya
kupunguza na kukabiliana na maafa yanayotokana na ukame nami naahidi nitafuatilia
kuona jinsi mnavyo elimisha wananchi katika kata zenu” alisisitiza Mutagurwa.
Mutagurwa alifafanua kuwa Kishapu bila athari zitokanazo na maafa ya ukame
inawezekana ikiwa wataalam wa ngazi ya kata watashirikishwa kwa kuwa wao
ndio wanao uwezo mkubwa kwa ngazi ya kata wa kutambua viashiria na vihatarishi
vinavyoweza kusababisha maafa na hatimaye kutoa ushauri sahihi kwa wananchi wa
kupunguza na kukabiliana na maafa yanayotokana na ukame.
“Kwa mfano Maafisa Ugani kwa utaalam wao kutokana na mvua kutonyesha mara kwa
mara katika wilaya yetu, kupitia mafunzo haya wataelewa matumizi ya Taarifa za Hali
ya Hewa ili waweza kuwashauri wakulima matumizi ya mbegu na pembejeo za kilimo
kwa kipindi muafaka cha kulima mazao yanayostahimili ukame, na hatimaye kuepukana
athari ya ukame ambayo ni wilaya yetu kuwa na upungufu mkubwa wa chakula”
alisema Mutagurwa.
Aliongeza kuwa waratibu wa Elimu katika kata na Watendaji wa Kata hawana budi
kuhimiza upandaji wa miti katika kata zao, kwakuwa miti ikipandwa kwa wingi wilayani
humo inaweza kukabiliana vyema na athari za mabadiliko ya Tabia Nchi ikiwemo
ukame.
Awali akimkaribisha Mkurugenzi huyo, Mratibu wa mafunzo hayo kutoka Ofisi ya
Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu Maafa, Bw.Harison Chinyuka alibainisha kuwa mafunzo
hayo ni sehem ya utekelezaji wa Mradi Wa Kuijengea Jamii Uwezo Wa Kupunguza
Athari Za Maafa Kwa Mikoa Iliyoathirika Zaidi Na Ukame ambao unafadhiliwa na Benki
ya Dunia na kusimamiwa na UNICEF chini ya Uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu na
Halmashauri husika wakiwa Watendaji Wakuu wa Mradi huo. Mradi huo unatekelezwa
kwa kipindi cha miezi 18 uliozinduliwa Wilayani Same, mkoani Kilimanjaro tarehe 11
Desemba2013.
Mradi huu ni mzuri sana kwani baadhi ya wafugaji waliogawiwa mbuzi tayari mbuzi wao wameanza kuzaa. Wanavikundi wanafurahi kwani ndani ya muda mfupi wataweza kuwa na uwezo wa kujimudu kimaisha.
ReplyDeleteTatizo la ukame Kishapu ni kubwa mno. Tunaishukuru OWM kutuletea mradi huu. Ombi letu kila taasisi ipewe mbegu za miti ipande. Barabara za miji midogo ya kishapu zote zipandwe miti ya kivuli. Tunaitarajia Kishapu mpya.
ReplyDelete