Na  Bashir  Yakub

Kawaida unapokuwa umeingia katika mkataba au makubaliano katika jambo lolote lile kunakuwa na masharti ambayo unapaswa kuyatimiza au kutimiziwa. Na hapa nazungumzia mikataba yote uwe wa kuuza mbuzi au ule wa kujenga ghorofa mia, yote ni mikataba. Masharti hayo huwa ndio makubaliano yenyewe au twaweza kusema kuwa ndio mkataba wenyewe. Kila upande unawajibika  juu ya utekelezaji wa masharti hayo. Yeyote anayefikia hatua ya kukiuka masharti hayo  au hata kukiuka sharti moja tu, hana namna ila kukubaliana na  hatua na utaratibu wa kisheria kuhusu  uvunjwaji au ukiukwaji wa mikataba. 

1.KUKIUKA  MKATABA   AU   MAKUBALIANO.

Uvunjaji wa mkataba unaweza kutokea katika njia nyingi. Moja ni ile ya kawaida ambapo mtu huamua kujitoa  kwa kusema,kutamka au kuandika kuwa sasa sitafanya hili na lile hata kama lipo katika makubaliano yetu.  Pili njia nyingine  ya kuvunja mkataba ni pale ambapo mtu hasemi kwa kutamka kwamba sasa sitafanya hili wala lile isipokuwa hatimiza wala hatekelezi kile mlichokubaliana. Ifahamike kuwa mtu anapoingia mkataba na mtu mwingine  au kampuni na kampuni  au kampuni na mtu sheria inalazimisha kutekeleza kwa usahihi yale yote yaliyokubaliwa  katika mkataba huo. Utekelezaji wa baadhi ya masharti na kuacha mengine au kutotekeleza yote kabisa ni uvunjaji au ni kujitoa katilka mkataba kwa mujibu wa sheria. Aidha nasisitiza kuwa ili mtu ajitoe katika mkataba sio lazima aseme kuwa nimejitoa katika mkataba. Kitendo cha kutofuata makubaliano  kama yalivyokubaliwa  ni kujitoa katika mkataba moja kwa moja.

2.KUMDAI  FIDIA    ALIYEKIUKA  MKATABA  AU  MAKUBALIANO. 

Si  vyema  mtu akafanya  makubaliano  na mtu mwingine  halafu  akapotea  bila  kutekeleza  kile  kilichokubaliwa. Ni  sababu  hii inayonifanya kuwaambia  watu  kuwadai  fidia  wale  wanaokiuka  masharti. Kudai kulipwa  fidia  baada ya  kuvunjwa  mkataba  ni takwa la  kisheria  na  hivyo  si  ukorofi  kama ambavyo  mtu anaweza kufikiri. 

3.AINA  ZA FIDIA  UNAZOWEZA  KUDAI  UKIVUNJIWA  MKATABA.

( a ) Fidia zipo za aina nyingi.  Kwanza kuna fidia ambayo utatakiwa kulipa kutokana na makubaliano yenu ya awali wakati mnaingia mkataba. Hii ni aina ya fidia ambayo wahusilka katika mkataba hukubaliana  awali kabisa wakati wanaingia katika mkataba  ambapo hupanga kiasi cha fidia ambacho watalipana iwapo mmoja kati yao atakiuka au kujitoa katika mkataba. Kwa kuwa fidia hii huwa  imeandikwa na ipo ndani ya mkataba basi aliyekiuka au kujitoa katika mkataba hutakiwa kulipa fidia hiyo  kulingana na makubaliano yao mara moja. 

( b ) Fidia  nyingine ni ile ambayo mtu hutakiwa kulipa iwapo wakati wanaingia mkataba hakuna fidia yoyote waliyokuwa wamekubaliana kulipa iwapo mmoja wao atakwenda kinyume.  Hii ni aina ya fidia inayotathminiwa na mahakama.  Mahakama hutathmini fidia hii kwa kuangalia mambo mawili yaani  kiwango cha ukiukwaji wa mkataba na hasara  zilizotokana na ukiukwaji huo. Kupitia hayo mahakama huweza  kutangaza kiwango cha fidia anachotakiwa kulipwa mtu ambaye amevunjiwa mkataba.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...