Bingwa wa zamani wa dunia wa uzito wa juu, Francois Botha na rais wa chama cha ngumi cha dunia cha WBF, Howard Goldberg wanatarajiwa kuwasili nchini kesho Machi 23, tayari kwa  kusimamia pambano la Mohamed Matumla Jr na Wang Xiu Hua wa China. 

Botha atawasili nchi kwa mara ya pili kwa mualiko maalumu wa Kampuni ya Hall Of Fame inayoandaa mapambano ya ngumi ndani na nje ya nchi. Nguli huyo wa masumbwi anatarajiwa kuwasili saa 12 jioni na ndege ya Shirika la ndege la Afrika Kusini sambamba na Goldberg wakiwa na mkanda wa dunia wa WBF wa uzani wa Super Bantam utakaowania na Matumla Jr na Hua Ijumaa hii kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee. 

Afisa Mtendaji Mkuu wa Hall of Fame, Jay Msangi alisema kuwa, baada ya kuwasili, Botha atashiriki katika programu mbalimbali za pambano hilo ambalo kama Matumla Jr akionyesha kiwango atakata tiketi ya kuzichapa pambano la Utangulizi kwenye lile la dunia kati ya Floyd Mayweather na Manny Pacquiao la Mei 2 jijini Las Vegas,Marekani. 



Wakati huohuo, mpinzani wa Matumla anatarajiwa kuwasili saa saba mchana wa kesho akitokea China tayari kwa pambano lao la Ijumaa. Hua atawasili jijini akiwa ameambatana na kocha wake sambamba na viongozi wengine wa ngumi wa nchi hiyo. Kwa mujibu wa Msangi, baada ya kuwasili bondia huyo ataendelea na mazoezi kabla ya kushiriki zoezi la kupima uzito na afya litakalofanyika Alhamisi hii. 

Katika hatua nyingine, mabondia Ashraf Suleiman, Mada Maugo, Karama Nyilawila, Japhet Kaseba na Thomas Mashali wako katika maandalizi ya mwisho kuelekea kwenye mapambano yao ya Ijumaa. Mabondia hao watapanda ulingoni kuzichapa kabla ya Matumla Jr na Hua kupanda kuwania ubingwa wa dunia. 

Mashali atazichapa na Nyilawila pambano lisilo la ubingwa la uzani wa super bantam wakati Maugo akizichapa na Kaseba kwenye uzani wa super heavy na Suleiman akionyeshana ubabe na bondia kutoka Marekani pambano la uzani wa juu siku hiyo. Kwa nyakati tofauti, mabondia hao kila mmoja alijinadi kumkung'uta mwenzake siku hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...