Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimraribisha Rais Paul Kagame wa Rwanda kwenye ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Kanda ya Kati (Central Corridor Conference) ulioanza jana na kumalizika leo Machi 26, 2015.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na wageni wake Rais Paul Kagame wa Rwanda na Rais Pierre Nkurunzinza kwenye ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Kanda ya Kati (Central Corridor Conference) ulioanza jana na kumalizika leo Machi 26, 2015.
Rais Paul Kagame wa Rwanda akipeperusha bendera kuashiria kuzinduliwa kwa safari za treni za mizigo kuelekea Rwanda katika stesheni ya reli ya Dar es salaam akiwa na mwenyeji wake Rais Jakaya Mrisho kikwete leo Machi 26, 2015.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na mgeni wake, Rais Paul Kagame wa Rwanda, leo, Alhamisi, Machi 26, 2015, wametembelea Bandari ya Dar es Salaam na baadaye Rais Kagame ameanzisha safari ya treni maalum za kusafirisha mizigo ya Rwanda kutoka Tanzania.
Rais Kagame amewasili nchini asubuhi ya leo na kufungua Mkutano wa Wawekezaji katikaUjenzi wa Miundombinu Ukanda wa Kati (High Level Investors Forum – Central Corridor Development Acceleration Programme) uliofanyika kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere mjini Dar es Salaam.
Mara baada ya hotuba ya ufunguzi na kipindi cha maswali kutoka kwa washiriki na majibu kutoka kwa viongozi wa nchi tano zinazounda Shirika la Uwezeshaji wa Usafiri wa Ukanda wa Kati (The Central Corridor Transit Transport Facilitation Agency (CCTTFA), viongozi hao wawili wamekwenda Bandari ya Dar es Salaam.
CCTTFA lilianzishwa Septemba 2, mwaka 2006, na Makubaliano yaliyotiwa saini na nchi tano ambazo zinanufaika na usafiri wa Ukanda wa Kati – Tanzania, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), Rwanda na Uganda.
Katika Bandari ya Dar es Salaam, Rais Kagame na mwenyeji wake wameanza kwa kutembelea ofisi mpya za Mpango wa Ukusanyaji Ushuru kwa Pamoja (Single Customs Territory) miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), mpango ulioanza kutumika Julai mwaka jana, 2014. Chini ya Mpango huo, kila nchi inashughulikia mizigo yake yenyewe, ikiwa ni pamoja na kukusanya kodi yake.
Rais Kagame na mwenyeji wake wametembelea ofisi za Mamlaka ya Kodi ya Rwanda (RRA) na Mamlaka ya Kodi ya DRC ambako walipewa maelezo kuhusu faida za mpango huo.
Miongoni mwa mambo mengine, marais hao walielezwa kuwa chini ya Mpango huo, waagizaji wa mizigo ya Rwanda, kupitia Bandari ya Dar es Salaam, sasa wanajaza fomu moja tu badala ya tatu na sasa mizigo ya Rwanda inachukua siku mbili tu kutoka Bandari ya Dar es Salaam hadi Kigali, badala ya siku kati ya tano na 10 kabla ya kuanzishwa Mpango huo.
Nchi ambazo tayari zimefungua ofisi zao katika Bandari hiyo kutekeleza Mpango huo ni Tanzania yenyewe, Burundi, DRC na Rwanda. Uganda inakamilisha maandalizi ya utekelezaji na Zambia imeonyesha nia ya kujiunga na Mpango huo, kwa sababu inapitishia mizigo yake katika Bandari ya Dar es Salaam, hata kama siyo mwanachama wa EAC.
Kutoka kwa ofisi za Single Customs Territory, viongozi hao wamekwenda kwenye Bandari ya Dar es Salaam ambako wamepatiwa maelezo kuhusu jinsi utendaji wa Bandari hiyo ulivyoboreka katika miaka miwili iliyopita.
Aidha, viongozi hao wameelezwa jinsi gani pia utendaji wa kampuni binafsi ya upakiaji na upakuaji mizigo ya TICTS inavyofanya kazi na ilivyoboresha utendaji wake katika sehemu nne za meli kutia nanga (berths) ambako inafanyia kazi yake katika Bandari hiyo yenye sehemu 11 za kupakia na kupakulia mizigo.
Katika Bandari hiyo, marais hao wameelezwa kuwa katika miaka mitano iliyopita, kiwango cha mizigo inayopitia katika Bandari hiyo kimekuwa kinaongezeka kwa wastani wa asilimia 12.8 kila mwaka.
Wameelezwa pia kuwa mwaka jana, kiasi cha tani milioni 14.6 ya mizigo kilipitia katika Bandari hiyo zikiwemo kontena 621,000 na kuwa kati ya mizigo hiyo kiasi cha asilimia 34, sawa na mizigo tani milioni 5.020 ilikuwa mizigo kwa ajili ya nchi za jirani.
Aidha, viongozi hao wameelezwa kuwa muda wa kontena kukaa Bandarini hapo sasa ni siku tisa tu badala ya siku 21 Februari mwaka 2008, muda wa meli kukaa nje ya Bandari ikisubiri kuingia Bandarini ili ipakuliwe, sasa ni siku moja unusu badala ya siku tatu unusu za mwaka 2013.
Marais Kagame na Kikwete pia wameelezwa kuwa usalama wa mizigo ya waagizaji sasa umeongezeka mno, kiasi cha kwamba halijakuwepo tukio hata moja la wizi wa mizigo ya wateja yakiwemo magari na spea zake kwa miaka mitatu mfululizo sasa.
Bandari ya Dar es Salaam ambayo huhudumia mizigo ya nchi saba – ya Tanzania yenyewe, Malawi, Zambia, DRC, Burundi, Rwanda na Uganda pia huendesha Bandari kwenye maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.
Jana, Jumatano, Machi 25, 2015, Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi pamoja na wawakilishi wa nchi za DRC na Uganda pia walianzisha safari za treni za namna hiyo kwenda katika nchi zao.
Rais Kagame ameondoka nchini kurejea kwao leo baada ya kuanzisha safari hizo na mkutano wenyewe kuhusu Ukanda wa Kati, ambao pia ulihudhuriwa na Rais Yoweri Museveni wa Uganda, umemalizika jioni ya leo.
Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.

26 Machi, 2015

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Naona tumejitahidi kuboresha usafiri wa mizigo kwa njia ya reli kwenda nchi jirani. Endelezeni kazi nzuri.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...