Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Swissport Tanzania Bw. Gaudence Temu (Katikati) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) juu ya utendaji wa kampuni yake mara baada ya mkutano mkuu wa kampuni hiyo kumalizika uliofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Pamoja nae kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Swissport, Bw. Juan Jose Andres Alvez na Bw, Jeroen L. de Clercq ambaye ni Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo nchini Kenya. 

KAMPUNI ya Swissport Tanzania Plc imepata ongezeko la faida kwa asilimia 73 (baada ya makato ya kodi na gharama nyingine zote), mafanikio yaliyotokana na maendeleo makubwa ya Sekta ya Usafiri wa Anga hapa nchini.

Kampuni hiyo  inayotoa huduma zake kwenye viwanja vya ndege vya Julius Nyerere (JNIA), Kilimanjaro  pamoja na ule wa Mtwara, ilitangaza mafanikio hayo hivi karibuni jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wake mkuu  wa thelathini.

Akizungumza mbele ya waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni hiyo, Bw Juan Alvez alitaja sababu za mafanikio hayo kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa mashirika ya ndege yanayofanya safari zake katika viwanja vya ndege vya Tanzania na ongezeko la wingi wa safari kwa mashirika yaliyopo.

“Ongezeko hili la asilimia 73 ni matokeo ya ongezeko la faida kutoka sh. bilioni 7.496 mwaka 2013 hadi kufikia sh. Bilioni 12.937 iliyoripotiwa  mwaka 2014,’’ alisema.

Akifafanua zaidi Bw Alves alisema jumla ya abiria 1,111,156 walihudumiwa katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita ambao ni sawa na ongezeko la asilimia 23 ikilinganishwa na idadi ya abiria 905,347 waliohudumiwa katika kipindi cha mwaka 2013.

Kufuatia mafanikio hayo ambayo pia yameonekana kwenye idara nyingine ikwemo ya ubebaji wa mizigo, Bw Alves alisema wana hisa wa kampuni hiyo  wana kila sababu ya kutabasamu kwa kuwa watapokea Sh287.50 ya gawio kwa kila hisa ikilinganishwa na sh 166.58 ya mwaka 2013 ili kuhakisi ongezeko hilo la asilimia 73.

Akizungumzia uwekezaji uliofanywa na kampuni hiyo kwa 2014, Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo Bw. Gaudence Temu alisema kampuni hiyo ilifanikiwa kununua vifaa vya usaidizi ardhini (GSE) vyenye thamani ya sh. Bilioni 1.7huku akiongeza kuwa vifaa hivyo tayari vimeshafika na vimeanza kutumika.

“Ongezeko lingine la sh. bilioni 2.7 katika uwekezaji  linatarajiwa kufanyika ndani ya mwaka huu na litahusisha mabasi mawili ya kubebea abiria katika viwanja vyetu sambamba na kifaa cha kupakia na kushusha mizigo mizito chenye uwezo wa hali ya juu,’’ alibainisha Bw. Temu.

Kampuni hiyo inajumuisha pia wanahisa wa Kitanzania wapatao 11,500 ambao wanamiliki asilimia 49 ya hisa zote huku asilimia 51 zikiwa zinamilikiwa na kampuni ya Swissport International.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...