Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage (wa sita kutoka kushoto, mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja Mameneja Tanesco wa mikoa na wilaya katika Nyanda za Juu Kusini Magharibi pamoja na wakandarasi wanaotekeleza miradi ya REA ya usambazaji umeme vijijini, Awamu ya pili katika kanda hiyo, mara baada ya kumaliza kikao kilicholenga kujadili utekelezaji wa miradi husika. Kulia kwa Naibu Waziri ni Meneja Mwandamizi wa Tanesco Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Magharibi, Salome Nkondola na kushoto kwa Naibu Waziri ni Kaimu Meneja wa Tanesco katika mkoa wa Mbeya, Magwila Mbalamwezi.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage (wa nne kutoka kushoto, mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja Mameneja Tanesco wa mikoa na wilaya katika Nyanda za Juu Kusini Magharibi mara baada ya kumaliza kikao kilicholenga kujadili utekelezaji wa miradi ya usambazaji umeme vijijini Awamu ya Pili katika kanda hiyo. Kulia kwa Naibu Waziri ni Meneja Mwandamizi wa Tanesco Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Magharibi, Salome Nkondola na kushoto kwa Naibu Waziri ni Kaimu Meneja wa Tanesco katika mkoa wa Mbeya, Magwila Mbalamwezi.
Na Teresia Mhagama, Mbeya
Serikali imesema kuwa haitolipa fidia kwa wananchi wanaopisha miradi ya
usambazaji umeme vijijini inayotekelezwa na Shirika la Umeme nchini
(TANESCO) kwa kushirikiana na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Hayo yamesemwa mjini Mbeya na Naibu Waziri wa Nishati na Madini,
Charles Mwijage wakati wa kikao chake na mameneja Tanesco wa mikoa
na wilaya katika Nyanda za Juu Kusini Magharibi pamoja na wakandarasi
wanaotekeleza miradi ya REA ya usambazaji umeme vijijini, Awamu ya pili
katika kanda hiyo.
Mwijage amesema kuwa serikali imechukua hatua hiyo baada ya kubaini
kuwa suala hilo limekuwa likichelewesha utekelezaji wa miradi ya
usambazaji umeme vijijini pamoja na kuigharimu serikali fedha nyingi
ambazo zinapaswa kutumika katika kuongeza kasi ya usambazaji umeme
katika maeneo hayo.
Suala hilo la baadhi ya wananchi vijijini kukwamisha miradi ya umeme kwa
kudai fidia lilielezwa pia na baadhi ya wakandarasi wanaotekeleza miradi
hiyo vijijini ambapo limepelekea usitishaji wa ujenzi wa miundombinu ya
usambazaji umeme katika sehemu zenye mapingamizi.
Naibu Waziri aliwaagiza wakandarasi hao kuhakikisha kuwa wanatoa
taarifa kwa wananchi kabla ya kuanza kazi katika maeneo ya wananchi
hao ili kujenga uelewa wa pamoja na hivyo kupunguza changamoto za
kupinga miradi hiyo ya umeme.
Vilevile Naibu Waziri aliwataka wakandarasi hao kuongeza rasilimali watu
katika maeneo waliyopangiwa kusambaza umeme ili miradi hiyo ikamilike
mwezi Juni mwaka huu kama ambavyo makubaliano kati ya serikali na
wakandarasi hao yanavyoelekeza.
"Ongezeni sub cotractors katika maeneo mnayofanyia kazi na kama mna
changamoto yoyote wasilianeni na Wakala wa Nishati Vijijini ili changamoto
hizo zitatuliwe na miradi hii ikamilike kwa wakati" alisema Mwijage.
Alisema kuwa wakandarasi watakaozembea katika ukamilishaji wa miradi
ya umeme, Awamu ya Pili, hawatapata nafasi ya kushindanishwa katika
mchakato wa kuwapata wakandarasi watakaopewa kazi ya kusambaza
umeme vijijini Awamu ya Tatu.
Vilevile Naibu Waziri amewapongeza wakandarasi wanaoendelea
kutekeleza miradi ya usambazaji umeme vijijini licha ya kuwepo kwa
changamoto mbalimbali na kuwahakikishia kuwa Wizara ya Nishati na
Madini inaendelea na jitihada za kuhakikisha kuwa malipo ya wakandarasi
hao yanafanyika kwa wakati.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...