Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania,Mh.Ali Hassan Mwinyi amefanya ziara ya siku tatu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Ziara hiyo ya Rais Mstaafu inafuatia mwaliko wa Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu
ya Iran uliomuomba kuwa mgeni mashuhuri katika sherehe za kuadhimisha miaka
hamsini na mbili (52) ya Afrika.
Siku ya Afrika huadhimishwa tarehe 25 Mei na
mataifa ya Afrika pamoja na Mabalozi na Wawakilishi wa mataifa hayo duniani
kote, ikiwa ni sehemu ya kumbukumbu ya kuasisiwa kwa Umoja wa Nchi Huru za
Afrika (OAU) tarehe 25 Mei 1963.
Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya
Iran ina desturi ya kuungana na Waafrika pamoja na wadau wengine wanaounga
mkono hatua za ukombozi na kupinga ubeberu katika maadhimisho ya siku hii
muhimu.
Katika sherehe hizo, Rais Mstaafu Mwinyi alihutubia hadhira iliyoongozwa
na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Dkt Muhammad Javad Zariff na kuhudhuriwa na
Mabalozi na Wawakilishi waliopo Iran, Viongozi na Maafisa waandamizi wa
Serikali ya Iran, na wadau wengine muhimu ikiwemo wanataaluma, wawakilishi wa
sekta binafsi na wanahabari.
Aidha, Rais Mstaafu Mwinyi alipata
nafasi ya kukutana na Mkuu wa Kamisheni ya Usuluhishi ya Jamhuri ya Kiislamu ya
Iran ambaye pia ni Rais Mstaafu wa taifa hilo Ayatollah Hashemi Rafsanjani.
Ayatollah Rafsanjani alikuwa Rais wa Iran wakati Ali Hassan Mwinyi akiwa Rais
wa Tanzania na wawili hao waliimarisha uhusiano wa kidiplomasia wa mataifa haya
mawili ambapo kila mmoja alizuru nchi ya mwenziwe. Rais Mstaafu Mwinyi
aliupokea mwaliko wa taifa hilo kwa lengo la kuzidi kuimarisha uhusiano wa
kidugu baina ya Tanzania na Iran. Katika ziara hiyo, Rais Mstaafu Mwinyi
aliongozana na Mke wake, Mama Khadija Mwinyi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...