Na Rahma Khamis /Takdiri Ali- Maelezo Zanzibar                          

Wizara ya Afya Zanzibar imesema Kitengo cha Mifupa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja kinaendelea kufanya kazi zake za kutoa Matibabu Masaa 24 kama kawaida kwa kufuata utaratibu maalum uliowekwa Hospitalini hapo.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo huko katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani wakati alipokuwa akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Muyuni Jaku Hashim Ayoub aliyetaka kujua lini Serikali itaweka daktari katika Hospitali hiyo kwa Masaa 24.

Amesema Hospitali ya Mnazi Mmoja ni Hospitali Pekee ya Rufaa kwa Zanzibar ambayo inafanya kazi ya kutoa huduma bora za afya na kwamba kwa sasa ina Madaktari bingwa wa Mifupa Wawili wanaopatikana kwa muda wa Masaa 24.

Amefahamisha kuwa kwa sasa Hospitali ya Mnazi Mmoja inautaratibu maalum wa Madaktari wa zamu kwa kila Idara kuwepo Hospitali kwa masaa 24 ili kuweza kutoa huduma pindipo anapofika mgonjwa.

Awali Jaku alidai kuwa Wagonjwa wa Ajali wanaofika kutafuta huduma kwa Madaktari hao wa Mifupa wanasumbuka na kupata huduma siku ya pili jambo ambalo halipendezi kwa Hospitali hiyo ya Rufaa.

Hata hivyo Naibu WAziri wa Afya alisema wagonjwa wote wanaofika Hospitali wakiwemo wagonjwa wa ajali hutakiwa wapitie kitengo cha huduma za dharura (Emergency department) kwa kupatiwa matibabu ya haraka zaidi katika kitengo hicho ambacho Madaktari hupatikana kwa masaa 24 .

Waziri Mahmuud aliongeza kuwa Hospitali hiyo imeweka usimamizi maalum kwa kufuatilia kazi za kila siku kwa watendaji wake na kuweza kutatua tatizo lolote linapotokezea.

Kuhusu malalamiko ya Madaktari Naibu Waziri huyo amewashauri Wananchi kupeleka malalamiko yao katika Ofisi ya Daktari Mkuu katika Jengo la Utawala Hospitalini hapo ili yaweze kufanyiwa kazi

IMETOLEWA NA MAELEZO ZANZIBAR.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...