Kampuni ya ujenzi ya CRJE kutoka China imekanusha vikali kuhusika na jengo la ghorofa lililoporomoka katika makutano ya mitaa ya Indira Gandhi na Asia jijini Dar es Salaam mwezi Machi mwaka 2013.
Taarifa iliyotolewa na kampuni hiyo jijini Dar es Salaam jana, inaeleza kuwa kampuni hiyo haikuwahi kushiriki katika ujenzi wa jengo hilo lililoanguka.
“Tumesikitishwa sana na taarifa iliyochapishwa kwenye gazeti moja la wiki inayoeleza kuwa kampuni yetu ilikua mkandarasi wa jengo lililoporomoka. Hatujawahi kuhusika kwa namna yoyote na ujenzi wa jengo lile,” Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo Bw. Hu Bo alisema.
Aidha, kampuni hiyo ilieleza kuwa haijawahi kupewa kazi ya kubomoa jengo hilo. Watu kadhaa walipoteza maisha na wengine kujeruhiwa katika ajali hiyo. Hata hivyo, Bw. Hu alisema kuwa kampuni yake ilishiriki katika shughuli za uokoaji kwa misingi ya kibinadamu.
Alisema kuwa juhudi za kampuni hiyo zilitambulika na kampuni ilizawadiwa cheti cha shukrani kutoka kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
CRJE imekuwa ikiendesha shughuli zake nchini Tanzania tangu mwaka 1970 na imepokea tuzo ya mkandarasi bora wa kigeni mara tatu. Kampuni hiyo imeshiriki katika ujenzi wa miradi mikubwa nchini kote ikiwa ni pamoja na ujenzi wa reli ya TAZARA, ujenzi wa hoteli ya Kilimanjaro Hyatt Regency jijini Dar es Salaam na ujenzi wa jengo la Bunge mjini Dodoma. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...