Mkurugenzi Mtendaji wa Benki
ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania, Thomas Samkyi, (pichani kati) akizungumza na waandishi wa
habari katika ofisi za Benki hiyo,Kinondoni kuhusu uzinduzi wa benki hiyo utakaofanyika Agosti 7, 2015,jijini Dar . Kulia ni
Mkuu wa Kitengo cha Mipango na Sera, Bwana Francis Assenga, na kushoto ni
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki, Bi Rosebud Violet Kurwijila.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki
ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania, Bi Rosebud Violet Kurwijila akifafanua jambo mbele ya
waandishi wa habari (hawapo pichani),katika ofisi za Benki hiyo jijini
Dar mapema leo kuhusu uzinduzi wa benki hiyo. Kulia kwake ni Mkurugenzi
Mtendaji wa Benki Thomas Samkyi, na Mkuu wa Kitengo cha Mipango na Sera,
Bwana
Francis Assenga.
Baadhi ya Wanahabari wakiwa kwenye mkutano huo mapema asubuhi ya leo
Rais Jakaya Kikwete
anatarajiwa kuzindua rasmi benki ya kwanza ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania,
ambayo inalenga kuanzisha mtizamo mpya wa kukiendeleza kilimo kupitia kushirikisha
wadau mbali mbali, kuangalia kila mnyororo wa thamani kwa ukamilifu wake,
pamoja na kuwa na ubunifu katika kuchangia kifedha kwenye miradi ya muda mrefu,
ya kati na muda mfupi kwenye sekta ya kilimo. Benki hiyo inatarajiwa kutoa mchango
mkubwa katika ukuzaji wa sekta ya kilimo ambayo imeajiri zaidi ya aslimia 70 ya
Watanzania.
Uzinduzi huo unatarajiwa
kufanyika kwa ngazi mbili: ngazi ya kwanza itahusisha uzinduzi wa Makao Makuu
ya TADB jijini Dar es Salaam mnamo tarehe 7 ya mwezi huu; ambapo ngazi ya pili itahusisha
uzinduzi rasmi wa TADB mbele ya wadau wake wakuu ambao ni Wakulima, kwenye
Maonesho ya Nane Nane Mkoani Lindi, katika kilele cha Siku Kuu ya Wakulima hapo
tarehe 8 Agosti 2015.
Akizungumza
na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya benki hiyo yaliyoko Barabara ya
Kinondoni, Mkurugenzi Mkuu wa benki, Bwana Thomas Samkyi, alisema dhumuni kuu
la uanzishaji wa benki hiyo ni kuboresha tija katika uzalishaji kwenye sekta ya
kilimo kwa kuunganisha nguvu za wadau mbalimbali ili kuwezesha uendelezaji wa
miundombinu ya kilimo kama miradi ya umwagiliaji, usafirishaji, uhifadhi,
mindombinu ya masoko, n.k. ambayo inachangia maendeleo ya sekta ya kilimo.
‘Uanzishwaji
wa benki hii unalenga kuziba mianya mikubwa ya ukopeshaji kwenye kilimo ambayo
inaachwa na benki za biashara, ili kuchochea kukua kwa sekta ya kilimo, kwa
kutoa mikopo na huduma nyingizezo za uwezeshaji wa kilimo kwa wakulima, ambao wengi
wao hawana uwezo wa kupata huduma za kibenki’ alisema Bw. Samkyi.
Akieleza
zaidi kuhusu uanzishwaji wa benki hiyo, Bwana Samkyi alisema Benki ya Wakulima itakuwa
msitari wa mbele katika kusukuma shughuli za kilimo pamoja na kuchagiza benki
na taasisi nyingine za kifedha kushiriki katika kuwezesha shughuli za kilimo.
‘Benki
hii imeundwa ili kutoa mikopo kwa masharti nafuu, pamoja na kutoa huduma
nyinginezo zitakazoongeza uwezo wa wakulima kukopa na kuzalisha. Ili
kufanikisha haya, benki inabidi iwe na vyanzo endelevu vya fedha za kutosha
kwani nchi hii ni kubwa na wadau wa benki ni wengi sana. Lengo kuu ni kubadili
kilimo cha Tanzania kutoka kilimo cha kujikimu kwenda kilimo cha kibiashara’
alisema Bw. Samkyi.
Benki hii pia inatarajiwa
kuwa ni kiungo muhimu cha utekelezaji wa mageuzi ya awamu ya pili ya sekta ya
kifedha, na vile vile kuboresha maendeleo ya kilimo nchini ikizingatia Dira ya Taifa
ya Maendeleo ya 2025 pamoja na mipango mbalimbali ya maendeleo ya miaka mitano
mitano, Mkakati wa Maendeleo wa Sekta ya Kilimo, na Mkakati wa Kukuza Uchumi na
Kupunguza Umasikini (MKUKUTA), pamoja na sera mbali mbali za Serikali
zinazohusu sekta ya kilimo.
Kuhusu Benki ya
Maendeleo ya Kilimo Tanzania
Benki
ya Maendeleo ya kilimo Tanzania (katika kuanzishwa kwake) ni taasisi mpya ya
kifedha iliyoanzishwa na serikali kwa madhumuni ya kuboresha huduma za kifedha
ikiwa ni pamoja na huduma nyinginezo katika sekta ya kilimo nchini Tanzania.
Benki
hii imeanzishwa ili kufikia malengo ya taifa yaliyoafikiwa katika Tanzania
Vision 2025, kusudio likiwa ni kuwezesha na kutosheleza upatikanaji wa chakula,
kuchochea kilimo cha biashara, pamoja na kuleta maendeleo ya kiuchumi na
kupunguza umasikini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...