Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana  na kiongozi wa Ujerumani Kansela  Angela Merkel kwenye ubalozi wa kudumu wa Ujerumani Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani Ijumaa  jioni.Rais Kikwete yupo katika ziara ya kikazi nchini Marekani ambapo mbali na kukutana na wadau wa Maendeleo anatarajiwa kutoa hotuba yake katika kikao cha 70 cha Baraza Kuu la Umioja wa Mataifa(UN General Assembly
Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza na kiongozi wa Ujerumani Kansela  Angela Merkel kwenye ubalozi wa kudumu wa Ujerumani Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani Ijumaa. Picha na Freddy Maro.


 ------------------------------------
JK: Kampeni zinaendeshwa kwa uhuru wa kumwaga kabisa
·         Afafanua kuwa Tanzania inataka mchakato utakaozaa uchaguzi huru na wa haki

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete  Ijumaa, Septemba 25, 2015 amemwambia Kiongozi wa Ujerumani, Kansela Angela Merkel kuwa upo uhuru mkubwa na usiokuwa kifani kwa vyama vyote ya siasa kufanya kampeni zake kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, 2015.

Aidha, Rais Kikwete amemwambia Kansela Merkel kuwa Jopo la Watu Mashuhuri Duniani linalotafuta kufanya mapendekezo ya jinsi dunia inavyoweza kujiandaa vizuri zaidi kwa magonjwa ya milipuko, sasa linakaribia kumaliza kazi yake na lipo katika hatua ya kuandaa mapendekezo kuhusu nini dunia ifanye katika siku zijazo.

Rais Kikwete amekutana na kuzungumza na Kansela Merkel katika mkutano uliofanyika kwenye Ubalozi wa Ujerumani kwenye Umoja wa Mataifa (UN) mjini New York na kuombwa na Mama Merkel mwenyewe. Viongozi hao wawili wapo New York, Marekani kuhudhuria shughuli za mwaka huu za Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (United Nations General Assembly (UNGA).

Katika mazungumzo hayo, Kansela Merkel alitaka kujua kutoka kwa Rais Kikwete kuhusu mwenendo mzima wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu zinazoendelea nchini na uhuru unaotolewa kwa kila chama kufanya kampeni zake.

“ Kama unavyojua Mheshimiwa Kansela tuko katikati ya Kampeni ya Uchaguzi Mkuu. Kampeni zinakwenda vizuri. Tunao wagombea wa urais nadhani kiasi cha wanane hivi na kila chama kinaendesha kampeni zake kwa uhuru mkubwa na usiokuwa na kifani. Tunataka mchakato ambao utazaa uchaguzi huru na wa haki na hivyo ni muhimu kwa kila chama kuendesha shughuli zake za kampeni kwa uhuru,” Rais Kikwete amemwambia Mama Merkel.
Rais pia amemwambia Kansela Merkel kuhusu baadhi ya mambo makubwa ya kampeni yakiwemo mambo yanayohusu masuala ya huduma za kijamii kama vile afya, elimu na mapambano dhidi ya umasikini. “Kampeni zote kwenye ngazi zote – ngazi ya urais, ngazi za wabunge na ngazi za Serikali za mitaa zinakwenda vizuri kwa uhuru wa kumwaga kabisa.”
Rais Kikwete pia ametumia mkutano wake na Kansela Merkel kumweleza Mama huyo kuhusu kazi ya Jopo ya Watu Mashuhuri Duniani kuhusu Matatizo ya Afya akisisitiza kuwa baada ya hatua ya kuwasilikiza watu mbali mbali, sasa Jopo limeanza kuandaa maoni yake na mapendekezo.
Jopo hilo ambalo liliteuliwa Aprili mwaka huu na Katibu Mkuu wa UN Mheshimiwa Ban Ki Moon kufuatia majonzi makubwa yaliyosababishwa na ugonjwa wa Ebola katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone, linatarajiwa kukabidhi ripoti yake kwa Mheshimiwa Ban Ki Moon Desemba mwaka huu.
Ujerumani ni moja ya nchi zinazoongoza dunia katika kuunga mkono na kugharimia shughuli za Jopo hilo na pia imewekeza fedha nyingi katika kugharimia uboreshaji wa mifumo ya afya katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone.

Baadaye usiku, Rais Kikwete alikuwa mmoja wa viongozi wa nchi nane duniani ambao wamehudhuria chakula cha usiku ambacho kimeandaliwa na Kansela Merkel kwa ajili ya viongozi ambao wanaunda kundi la nchi ambazo zimekubali kubeba wajibu wa kuhakikisha utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development Goals –SDG) ambayo yanachukua nafasi ya Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDG) ambayo muda wake wa utekelezaji wa miaka 15 umemalizika.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 2 mpaka sasa

  1. Tunashukuru sana kwa ujumbe, ila huyu mama sio kansela ni chansela..... Kuna tofauti kubwa

    ReplyDelete
  2. Mtoa Anony namba 1 tunashukuru kwa kurekebisha lakini mbona wasomaji tumemuelewa mwandishi kulikuwa hakuna haja ya kukosoa,je ? unaweza kutusaidia kwa kiswahili maana yake nini?
    wadau
    FFU

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...