THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
wa Tanzania na Marekani
·         Aiomba Serikali ya Marekani kuendelea kuiunga mkono Serikali mpya kama ilivyofanya kwake
·         Aishukuru kwa misaada iliyobadilisha maisha ya Watanzania katika miaka 10 ya uongozi wake

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameihakikishia Serikali ya Marekani kuwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili hautabadilika na kuwa utaendelea kuboreshwa zaidi hata baada ya kuingia madarakani kwa Serikali mpya Novemba mwaka huu, 2015.

Aidha, Rais Kikwete ameiomba Serikali ya Marekani kuunga mkono utawala mpya wa Tanzania unaoingia madarakani Novemba mwaka huu kwa kiwango kile kile ambacho Serikali hiyo imeipatia Serikali yake kwa miaka 10 iliyopita.

Vile vile, Rais Kikwete ameishukuru Serikali na wananchi wa Marekani kwa misaada mingi ambayo imechangia sana kuboreka kwa maisha ya Watanzania na kuinua kiwango cha maendeleo nchini katika miaka 10 ya uongozi wake wa Tanzania.

Rais Kikwete ameyasema hayo , Jumanne, Septemba 22, 2015 wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje ya Marekani, Mheshimiwa Anthony Blinken kwenye Hoteli ya Ritz-Carlton mjini Washington ambako Rais Kikwete amefikia katika ziara yake ya kikazi ya siku mbili kwenye mji huo mkuu wa Marekani.

Rais Kikwete amemwambia Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani: “Sioni uwezekano wowote wa msimamo wa Serikali mpya ya Tanzania kuhusu uhusiano wake na Marekani kuwa tofauti na ule ambao umekuwepo katika miaka 10 iliyopita. Dhahiri uhusiano huo hautabadilika kama Rais mpya atatoka katika chama chetu, lakini hata Rais akitokea chama kingine, sioni kama yanaweze kuwepo mabadiliko yoyote ya msingi ya sera au uhusiano kati ya Tanzania na Marekani.”

Kuhusu ombi lake ya Serikali ya Marekani kuendelea kuunga mkono Serikali ijayo ya Tanzania, Rais Kikwete amesema: “Naiomba Serikali ya Marekani iendelee kuunga mkono Serikali yetu ijayo na wananchi wa Tanzania.”

Ameongeza: “ Nawaombeni muendelee kuunga mkono maendeleo ya Tanzania. Matunda ya misaada yenu sasa yameanza kuonekana. Kwa mfano katika miaka 10 iliyopita Pato la Taifa limepanda mara tatu kutoka dola za Marekani bilioni 14.4 hadi kufikia dola za Marekani bilioni 50 kwa sasa.”
Kuhusu misaada ambayo Serikali ya Marekani imeitoa kwa Tanzania katika miaka 10 ya uongozi unaomaliza muda wake, Rais Kikwete amesema: “Naishukuru sana Serikali na wananchi wa Marekani kwa misaada mingi na kila aina ambayo mmeitoa kwa nchi yetu na Serikali yangu.  Mmeacha nyanyo katika maendeleo ya nchi yetu. Tumepata ustawi usiokuwa wa kawaida katika miaka 10 iliyopita.”

Rais Kikwete amesema kuwa Marekani kupitia mpango wake wa Pepfar, imechangia kupunguza sana makali ya magonjwa ya malaria na ukimwi. “Kwa upande wa malaria, mmesaidia kuokoa mamilioni ya maisha ya watu na vifo kutokana na ugonjwa huo sasa vimepungua kwa kiwango cha asilimia 70. Maambukizo ya ugonjwa wa ukimwi yamepungua sana. 
Matokeo yake ni kwamba wastani wa Watanzania kuishi umepanda kutoka miaka 55 hadi kufikia miaka 62 katika kipindi kifupi sana cha miaka 10 tu.”

Baada ya hapo, Rais Kikwete ameingia katika undani wa misaada ya Marekani katika maeneo mbali mbali kuanzia kwenye kilimo na mipango inayoungwa mkono na Marekani ya Feed The Future na Alliance for Food and Nutrition Sufficiency.

“Kutokana na misaada yenu, sasa tunajitegemea kwa chakula na hata kubakiza kiasi cha kuwauzia majirani zetu. Na hii yote ni kwa kutilia maanani kuwa wakati tunaingia madarakani tulilazimika kuwalisha kiasi cha watu 3.7 milioni kwa sababu ya ukame na ukosefu wa chakula.”

Kwa upande wa misaada iliyotolewa chini ya Mpango wa Millenium Challenge Corporation (MCC - 1), Rais amesema kuwa misaada hiyo katika ujenzi wa barabara, usambazaji umeme na kuanzishwa kwa miradi ya kusambaza maji imechangia mno kuboresha kiwango cha maisha ya Watanzania.

“Chini ya MCC, tumejenga kwa kiwango cha lami barabara zote za Pemba, tumejenga barabara kubwa kama ile ya Tanga-Horohoro, Tunduma-Sumbawanga, Songea-Namtumbo, tumepanua huduma za maji katika miji ya Dar es Salaam na Morogoro na tumesambaza umeme katika mamia ya vijiji katika mikoa 10 ya Tanzania Bara. Mwaka 2015, ni asilimia 10 ya vijiji vyetu vilikuwa na umeme. Sasa kwa msaada wetu, kiwango hicho kimefikia asilimia 46.”

Katika sekta ya elimu, Marekani imesaidia upatikanaji wa vitabu vya kufundishia masomo ya hisabati na sayansi katika shule za sekondari nchini. “Msaada wetu katika eneo hili, umeanza kuboresha elimu yetu. Ubora wa elimu umepanda na viwango vinapanda.”

Rais Kikwete pia ameishukuru Serikali ya Marekani kwa misaada yake katika mapambano dhidi ya madawa ya kulevya na katika masuala ya usalama na vita dhidi ya ugaidi akisisitiza: “kwa sababu ya misaada yenu katika eneo hili, tuko imara zaidi hata kama matishio bado yapo.”

            Rais pia ameishukuru Serikali ya Tanzania katika ujenzi wa utawala bora yakiwemo mapambano dhidi ya rushwa. “Demokrasia yetu inaendelea kuwa bora zaidi. Tunaendelea kupambana na rushwa, hata kama mapambano yenyewe ni magumu. Kama mnavyojua, hata mawaziri wenzangu wawili sasa wako jela baada ya kupatikana na hatia za matumizi mabaya ya madaraka.”

Rais Kikwete pia ameishukuru Serikali ya Marekani kwa mchakato wa kuanzishwa kwa Mpango wa MCC -2, akisisitiza kuwa changamoto ambazo zimejitokeza katika maandalizi ya mpango huo zitashughulikiwa ipasavyo na kwa haraka na Serikali yake.
   
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
24 Septemba, 2015

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Umekua msemaji wetu UKAWA au????tutaamua wenyewe tushirikiane na nani na nani tupige chini!!

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...