THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: ikulucommpress@googlemail.com
Website : www.ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425
| ![]() |
PRESIDENT’S OFFICE,
STATE HOUSE,
1 BARACK OBAMA ROAD,
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete , Jumamosi, Oktoba 10, 2015 amezindua mtambo mkubwa na miundombinu ya kisasa kabisa ya kuchakata na kusafirisha gesiasilia katika uwekezaji mkubwa ambako Serikali imewekeza kiasi cha dola za Marekani bilioni 1.33, sawa na sh trilioni 2.926, na kukamilisha uhakika wa kuongeza upatikanaji wa gesi kwa ajili ya matumizi ya uzalishaji na matumizi ya umeme viwandani, majumbani na kwenye magari.
Rais Kikwete amezindua mtambo huo katika eneo la Madimba, kilomita 25 kutoka mjini Mtwara, na kwa kuzindua miundombinu hiyo, Serikali sasa imekamilisha uunganishaji wa maeneo yanayozalisha gesiasilia kwa sasa ya Mnazi Bay na Songo Songo yanayotarajiwa kuzalisha gesi baadaye ya Ntorya, Kiliwani Kaskazini (Songo Songo) katika Mkoa wa Mtwara na Mkuranga katika Mkoa wa Pwani pamoja na gesi itakayotoka Bahari ya Hindi.
Akizungumza katika sherehe kubwa ya uzinduzi iliyohudhuriwa na mamia kwa mamia ya wananchi, mabalozi, wawekezaji katika sekta ya gesiasilia nchini, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Dr. James Mataragio amemwambia Rais Kikwete kuwa fedha za kuwekeza katika mradi huo mkubwa zimetokana na mchango wa Serikali ya Tanzania na mkopo kutoka Serikali ya Watu wa China kupitia benki yao ya EXIM.
Miundombinu hiyo iliyozinduliwa na Rais Kikwete inahusisha mitambo ya Madimba yenye uwezo wa kusafisha gesi futi za ujazo milioni 210 kwa siku, mitambo mingine kama hiyo katika eneo la Songo Songo yenye uwezo wa kusafisha gesi futi za ujazo zipatazo milioni 140 kwa siku, bomba lenye urefu wa kilomita 18 kutoka eneo la Mnazi Bay, Msimbati hadi Madimba na bomba la kusafirisha gesiasilia kutoka Mabimba hadi Kinyerezi mjini Dar es Salaam lenye urefu wa kilomita 477.
Aidha, mitambo hiyo ni pamoja na bomba la kusafirishia gesi la kilomita 29 kutoka Bahari ya Hindi hadi Songo Songo hadi Somanga Fungu na bomba lenye urefu wa kilomita 28 kutoka Kinyerezi hadi Ubungo hadi Tegeta kwa ajili ya kuzalisha umeme zaidi nchini.
Ujenzi wa miundombinu hiyo ulianzishwa na Rais Kikwete wakati shughuli rasmi ya utandazaji bomba kutoka Madimba hadi Dar es Salaam Novemba 21 mwaka 2012 wakati alipoweka jiwe la msingi katika ujenzi wake eneo la Kineyerezi Dar es Salaam na hivyo kuwezesha wakandarasi wakuu kuanza kazi ya ujenzi wa miundombinu hiyo ambayo inamilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Tanzania kupitia TPDC.
Wakandarasi wakuu watatu ni makampuni matatu kutoka China ambayo ni Kampuni ya China Petroleum Technology and Development Corporation (CPTDC), China Petroleum Pipeline Bureau (CPP) na China Petroleum Engineering Company (CPE). Makampuni hayo yote matatu ni tanzu ya Shirika la Mafuta la China la China National Petroleum Company (CNPC).
Mkurugenzi huyo wa TPDC ambayo inashiriki katika Mradi wa miundombinu hiyo kupitia kampuni yake tanzu ya GASCO amesema kuwa uzinduzi wa miundombinu unaifanya Tanzania kuingia katika orodha ya nchi zenye nishati ya gesiasilia duniani. “Na siyo ya kutosha tu bali ya kukidhi mahitaji muhimu kwa uwekezaji mkubwa, wa kati na hata wa kijasiriamali na hivyo kuwa na msingi mkuu na muhimu wa kuchochea maendeleo ya viwanda na ukuaji wa uchumi wa kasi zaidi.”
Akizungumza katika sherehe hizo, Rais Kikwete ametaka wote wanaohusika na huduma ya umeme kuhakikisha wanakomesha kukatika kwa umeme nchini kwa sababu sasa hakuna sababu ya kuwepo kwa tatizo hilo nchini.
Aidha, ameitaka TPDC kutimiza wajibu wake wa kijamii kwa kuwajengea wananchi huduma za afya, zahanati, shule na mahitaji mengine madogo wakazi wa maeneo ambako gesi hiyo inatoka na hata katika maeneo ambako bomba lao kuu linapitia.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
11 Oktoba, 2015
THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: ikulucommpress@googlemail.com
Website : www.ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425
| ![]() |
PRESIDENT’S OFFICE,
STATE HOUSE,
1 BARACK OBAMA ROAD,
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete , Jumamosi, Oktoba 10, 2015, amefungua kiwanda kikubwa zaidi cha kuzalisha saruji kuliko kingine chochote katika Afrika Mashariki kinachomilikiwa na Kampuni ya Dangote Group ya Nigeria ambayo Mwenyekiti na Rais wake, Alhaji Aliko Dangote ndiye tajiri mkubwa zaidi Barani Afrika.
Uzinduzi huo umefanyika kwenye kiwanda hicho kipya kilichoko eneo la Msijute, Mtwara Vijijini, Mkoa wa Mtwara kiasi cha kilomita 20 kutoka mjini Mtwara kwenye Barabara ya Mtwara-Lindi na kuhudhuriwa na wafanyabiashara kiasi cha 170 kutoka Nigeria ambao wamehudhuria sherehe hiyo kama wageni wa Alhaj Dangote.
Aidha, ujumbe huo wa Dangote Group umeongozwa na Mheshimiwa Mallam Nasir Ahmad El Rufai, Gavana wa Jimbo la Kaduna ambaye pia ameiwakilisha Serikali ya Nigeria ambayo imekuwa inawaasa wafanyabiashara wake kusambaza uwekezaji wao katika Bara la Afrika na hasa katika nchi zenye utulivu wa uhakika kama Tanzania.
Kiwanda hicho kipya pia kinatarajia kuajiri watu 1,500 katika ajira ya moja kwa moja na watu 9,000 kwa ajira isiyokuwa ya moja kwa moja
Kiwanda hicho ambacho kitazalisha tani za ujazo milioni tatu kwa mwaka kimegharimu dola za Marekani milioni 600, ikiwa ni uwekezaji mkubwa zaidi kutoka nje kuingizwa katika uchumi wa Tanzania na ambacho uzalishaji wake unatarajiwa kushusha kwa kiasi kikubwa bei ya bidhaa muhimu ya saruji nchini ambayo katika baadhi ya maeneo ya Tanzania mfuko wa kilo 50 wa saruji unagharimu kiasi cha sh. 20,000.
Uzalishaji wa saruji wa kiwanda hicho ni mkubwa kuliko uzalishaji wa viwanda vyote vya saruji vilivyoko nchini kwa sasa na kuwepo kwake kutabadilisha uchumi wa Mkoa wa Mtwara na kuchangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania ambayo inatumia kiasi cha tani za kimetriki milioni tatu kwa shughuli za ujenzi wa nyumba, madaraja na barabara.
Sherehe hizo za ufunguzi wa kiwanda hicho ambacho kimejengwa katika muda mfupi sana wa miaka miwili unusu pia zimehudhuriwa na Waziri Mkuu wa Chad na Mawaziri kutoka nchi za Malawi na Mozambique. Aidha, Alhaj Dangote amefuatana na watoto wake watatu wa kike na wajumbe wa Bodi ya Dangote Group katika sherehe hizo.
Akizungumza katika sherehe hizo za kufana zilizofanyika kwenye eneo la kiwanda hicho kikubwa, Rais Kikwete amesema kuwa kiwanda hicho kimezinduliwa wakati mwafaka kwa sababu sekta ya ujenzi imekuwa kwa kiasi kikubwa katika miaka 10 iliyopita na kwa sasa inachangia asilimia 12.5 katika Pato la Taifa kutoka asilimia saba.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
11 Oktoba, 2015
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...