Na Veronica Simba

Serikali ya Tanzania imeendelea kupokea maombi ya wawekezaji hususani katika miradi mbalimbali ya uzalishaji na usambazaji umeme. Hivi karibuni, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alikutana na kuzungumza na Ujumbe kutoka Kampuni ya NARI Group Corporation ambayo ni Kampuni Tanzu ya Shirika la Gridi ya Taifa la China, ambao walimweleza Waziri kuwa, pamoja na madhumuni mengine, wana nia ya kuzalisha umeme.

Makamu Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo, Bao Tianhua alimweleza Waziri Muhongo kuwa, Kampuni yake inao mtaji wa kutosha pamoja na teknolojia ya kisasa katika uzalishaji umeme. Aliongeza kuwa Kampuni ya NARI ina uzoefu mkubwa katika kutekeleza miradi ya umeme kwani ilianza kufanya kazi kutoka miaka ya 1960.

Akijibu swali la Waziri kuhusu kiwango cha umeme ambacho Kampuni yake imejipanga kuzalisha endapo itakubaliwa maombi yake, Tianhua alisema wamejipanga kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 300 hadi 400 kwa kuanzia.

Akieleza zaidi kuhusu nia ya Kampuni yake kuwekeza katika uzalishaji wa umeme nchini, Tianhua alisema kuwa wangependa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) katika mradi huo ambapo NARI watawezesha masuala yote ya kiuchumi katika mradi.

Vilevile, alisema kuwa lengo lao ni kuzalisha umeme kwa kutumia gesi kupitia teknolojia ijulikanayo kitaalam kama ‘combined cycle’.

Akitoa mwongozo kuhusu maombi yaliyowasilishwa, Profesa Muhongo aliwataka wawekezaji hao kukutana na kuzungumza na TANESCO pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) ili kujadili kwa kina kuhusu mapendekezo husika na kwamba, iwapo maombi yao yatakubaliwa, ndani ya kipindi cha mwezi mmoja (Aprili 15 mwaka huu), NARI wanatakiwa wawe wamethibitisha iwapo watafanya uwekezaji huo ama la.

“Muda tunaotoa kwa sasa si zaidi ya mwezi mmoja, hivyo ndani ya mwezi mmoja, iwapo maombi yenu yatakuwa yamekubaliwa, mtapaswa kuwa mmewasilisha jibu lenu.”

Aidha, Waziri Muhongo aliwataka NARI kuwasilisha kwa TANESCO na EWURA mapendekezo mengine waliyowasilisha kwake kuhusu nia ya kuwekeza katika miradi ya umeme vijijini kwa kutumia teknolojia ya makontena maalumu pamoja na miradi ya umeme jua. Aliwataka kuzungumzia hayo katika kikao kilichopangwa kufanyika baina yao.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kushoto), akimsikiliza Meneja wa Kanda ya Ulaya na Afrika wa Kampuni ya NARI Group, Chen Chao wakati alipokutana na Ujumbe kutoka Kampuni hiyo hivi karibuni Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam. Kushoto kwa Waziri ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, anayeshughulikia masuala ya Nishati, Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo pamoja na Viongozi na Maofisa waandamizi wa Wizara. NARI wameonyesha nia kuwekeza katika uzalishaji umeme.
Makamu Meneja Mkuu wa Kampuni ya NARI Group, Bao Tianhua (Kushoto), akimkabidhi Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kulia) zawadi ya picha ya mmoja wa miji maarufu ya China. Anayeshuhudia ni Meneja wa Kampuni hiyo kwa Kanda za Ulaya na Afrika, Chen Chao. Ujumbe kutoka Kampuni ya NARI Group ulikutana na Waziri Muhongo hivi karibuni Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam na kuonyesha nia ya kuwekeza katika uzalishaji wa umeme.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia masuala ya Nishati, Dkt Mhandisi Juliana Pallangyo ( wa pili – kushoto), akizungumza jambo na Meneja wa Kampuni ya NARI Group kutoka China, Chen Chao (Kulia) mara baada ya kikao baina yao na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, ambapo walionesha nia ya kuwekeza katika uzalishaji wa umeme.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...