Na Mbaraka Kambona,
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Katiba na Sheria, Mhe. Amon Mpanju amesema kuwa mapenzi ya jinsia moja
hayakubaliki na Serikali ilishaweka msimamo wake katika hilo.
Akizungumza mapema katika
mkutano wa wadau wa haki za binadamu uliofanyika katika hoteli ya Blue Pearl jijini Dar es salaam kujadili mapendekezo ya tathmini ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu (Universal Periodic Review) na kuweka
mikakati ya kuishawishi serikali kukubali mapendekezo mengine ambayo
iliyakataa, Mhe. Mpanju ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi katika mkutano huo
alisema mapendekezo yaliyowasilishwa
Mwezi Mei mwaka huu katika mkutano wa Baraza la haki za binadamu uliofanyika
Geneva, serikali ilikubali mapendekezo Mia thelathini (130) na mengine 72
iliyakataa.
“Sehemu ya mapendekezo hayo
serikali iliyakataa kwa sababu kuna mengine yapo kinyume na katiba, sheria,
mila na desturi zetu, kwani katika mapendekezo hayo yapo yanayotaka mapenzi ya
jinsia moja jambo ambalo haliwezi kukubalika”, Mhe. Mpanju alisema
“Hivyo wakati mkijadili namna ya
kupanga mikakati ya utekelezaji ili serikali ione umuhimu wa kukubali sehemu ya
mapendekezo hayo naomba msijielekeze kwenye yale yaliyo kinyume na imani”, Mhe.
Mpanju alisisitiza
Aidha, Mhe. Naibu Katibu huyo
alisema serikali imefungua milango kwa kushirikiano na tume, wadau wa haki za
binadamu wapeleke serikalini sababu
zenye mantiki ili kuona ni mambo gani
ambayo serikali inaweza
kuyashugulikia na kuyatekeleza.
Akizungumza katika Mkutano huo, Bwana
Onesmo Olengurumwa kutoka taasisi ya watetezi wa haki za binadamu (THRDC)
alisema kuwa wadau wamekutana katika mkutano huo kujadili ni kwa namna gani wataishawishi
serikali ili iweze kuyakubali mapendekezo yaliyobakia na kuyaweka katika utekelezaji.
Akitoa muhtasari wa mkutano huo kabla ya
kumkaribisha Mgeni rasmi, Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na
Utawala Bora, Mhe. Iddi Mapuri alisema kuwa mkutano huo umelenga katika kuweka
mikakati ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa mapendekezo hayo na alipongeza
mchango mkubwa unaotolewa na wadau wa haki za binadamu katika kuhakikisha
masuala ya haki za binadamu yanapata msukumo mkubwa hapa nchini.
Bwana Onesmo Olengurumwa
(kulia) kutoka taasisi ya watetezi wa haki za binadamu
(THRDC) akijadiliana jambo na Mkurugenzi
wa Idara ya huduma za sheria wa Tume ya Haki za Binadamu, Bwana Nabor
Assey( aliyevaa shati la bluu). Nyuma yao ni Bwana Laurent Burilo Burilo,
Mratibu wa Mpango kazi wa Haki za Binadamu(katikati) na Bwana Deugratius Bwire
kutoka (THRDC.
Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Haki
za Binadamu na Utawala Bora, Mhe. Iddi Mapuri akisoma muhtasari wa mkutano huo kabla ya
kumkaribisha Mgeni rasmi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Katiba na Sheria, Mhe. Amon Mpanju (kulia) akiteta jambo na Bwana
Onesmo Olengurumwa kutoka taasisi ya watetezi wa haki
za binadamu (THRDC) katika mkutano huo wa kujadili mapendekezo ya tathmini ya
utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu na kuweka mikakati ya kuishawishi
serikali kukubali mapendekezo mengine ambayo iliyakataa.
Wadau walioshiriki mkutano huo
wakiwa katika picha ya pamoja na Mgeni rasmi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Katiba na Sheria, Mhe. Amon Mpanju.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...