Na Frank Mvungi,MAELEZO-Dar es Salaam

SERIKALI kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi imetoa kiasi cha Tsh. Milioni 440 katika mwaka 2015/16 kwa  vikundi 73 vya uvuvi ili  kuiwezesha sekta ya uvuvi kuongeza tija na kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa Viwanda nchini.

Hayo yamesemwa jana Jijini Dar es salaam na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Yohana Budeba wakati wa mahojiana maalum katika Kipindi cha “TUNATEKELEZA” kinachoratibiwa na Idara ya Habari (MAELEZO) kurushwa hewani kupitia Kituo cha Televisheni ya Taifa (TBC).

Dkt. Budeba alisema Serikali imekusudia kuinua mchango wa sekta ya uvuvi kwa kuviwezesha vikundi vya wafugaji kuendesha shughuli zao kwa ufanisi mkubwa kwa kuvipatia ruzuku na mikopo kutoka katika taasisi mbalimbali za kifedha ikiwemo mabenki na mifuko ya hifadhi za jamii.

“Wizara inashirikiana na Halmashauri za Wilaya nchini katika kuwapatia fedha vikundi vyote vya wafugaji samaki waliopo katika ushirika, ambapo asilimia 40 hutolewa na Serikali ikihusisha ruzuku ya zana bora za uvuvi ikiwemo injini, nyavu na chakula cha samaki” alisema Dkt. Budeba.

Kwa mujibu wa Budeba alisema katika kuhamasisha ujenzi wa uchumi wa viwanda nchini kupitia mchango wa sekta hadi kufikia sasa Serikali imeanisha jumla ya viwanda 48 vya usindikaji samaki nchini, ikiwemo viwanda vidogo 36 vilivyopo katika ukandwa wa pwani wa bahari ya hindi, viwanda 11 vilivyopo kanda ya ziwa na kiwanda kimoja kilichopo katika ukanda wa ziwa Tanganyika.

Aidha Dkt. Budeba alifafanua kuwa katika kuwajengea uwezo vikundi hivyo, Serikali imekusudia kuajiri Maafisa Ugani katika kila kata nchini, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi na kuweza kutumika kama pato na lishe kwa wananchi.

Akizungumzia kuhusu maendeleo ya sekta hiyo, Dkt. Budeba alisema mpaka sasa Tanzania ina jumla ya mabwawa 22,000 yenye uwezo wa kuzalisha tani 10,000 za samaki, ambapo katika kipindi cha miaka mitano ijayo Serikali imekusudia kuvuna tani 50,000 za samaki, hatua inayolenga kuiwezesha nchi kujitosholeza na akiba ya samaki.

Akifafanua zaidi, Dkt. Budeba aliongeza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wanafuga kitaalamu zaidi, ambapo Serikali inaendelea kutoa mafunzo kwa wataalamu wake katika vituo vya kutotoleshea vifaranga vya samaki vilivyopo Mbegani, Nyegezi na Igunga.

Alisema mikakati iliyopo kwa sasa ni pamoja na kuwawezesha wavuvi kukopa kutoka Benki ya Kilimo ili  kuwawezesha kuzalisha samaki na pia kuanzisha ufugaji wa Samaki katika maeneo mbalimbali kwa kutumia mfumo wa vizimba.

Dkt. Budeba alisema katika kuvutia wawekezaji katika sekta hiyo tayari Serikali imetoa amesema leseni 76,000, hatua inayolenga kuongezeka kiwango cha uzalishaji wa samaki nchini.
Alibainisha kuwa miongoni mwa changamoto zinazoikabili Wizara hiyo kwa sasa ni pamoja na uhaba wa Maafisa ugani, ambapo kwa sasa ina maafisa ugani 800 ingawa mahitaji halisi ni maafisa ugani 16,000.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...