Na Ripota wetu,Tunduru

BAADHI ya wazee wa Kijiji cha Amani kata ya Namasakata Halmashauri ya wilaya Tunduru mkoani Ruvuma,wameiomba Serikali kuongeza kasi  kampeni ya uchunguzi wa  ugonjwa wa kifua kikuu  ambao umekuwa  tishio na kusababisha vifo vya watu wengi  hususani  wazee waishio vijijini.

Wakizungumza jana wakati wa kampeni ya uchunguzi wa ugonjwa wa kifua kikuu kwa wakazi wa kijiji hicho, wazee hao wameomba wataalam wa Afya waendelee  na kampeni  ya kijiji hadi kijiji  kwani itasaidia kuibua watu wengi ambao wanashindwa kwenda Hospitali ya wilaya umbali wa km 20 kwa ajili ya vipimo pamoja  na tiba ya ugonjwa huo.

Hamis Rashid(65) na Ahamd  Majikita(70)  licha ya kuipongeza  Hospitali ya wilaya kupitia kitengo cha kifua kikuu na ukoma  kuanzisha kampeni ya uchunguzi wa kifua kikuu kwa watoto na watu wazima.

Hata hivyo  walidai,  kuna haja ya wataalam hao kwenda katika maeneo yote hasa vijijini ambako kuna idadi kubwa ya watu wenye viashiria vya ugonjwa wa kifua kikuu lakini hawajapata vipimo wala tiba na wanaendelea kuteseka.

Ahmad Majikita alisema, tatizo linalochangia kukithiri kwa magonjwa  maeneo ya vijijini  ni hali duni ya kipato, kutokana na kukosa fedha za nauli, gharama za chakula na maradhi pindi wanapohitajika kwenda Hospitali ya wilaya Tunduru au katika vituo vya Afya kwa ajili ya kupata matibabu.

Alisema,kwa hiyo kama wataalam watafika kila kijiji  itasaidia wazee wengi kutambua hali ya Afya zao na kupata matibabu.

Alisema, maeneo ya vijijini wazee wengi wanapoteza maisha kwa kukosa vipimo na tiba sahihi kwani licha ya kuwepo kwa zahanati lakini tatizo  ni vifaa tiba kwa ajili ya vipimo, wataalam  na  baadhi ya dawa  ambazo zinapatakana katika hospitali ya wilaya Tunduru mjini na  katika vituo  vikubwa  vya Afya.

Kwa upande wake mratibu wa kifua kikuu na ukoma wa Hospitali ya wilaya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole alisema,serikali kupitia kitengo cha kifua kikuu katika Hospitali ya wilaya imeanza kuchukua hatua kwa kutembelea  vijijini kwa ajili ya kufanya  uchunguzi wa ugonjwa wa kifua kikuu sambamba na kuwaanzishia dawa wale watakabainika kuwa na vimelea vya maradhi hayo.

Kwa mujibu wa Kihongole,Serikali imekuwa ikishirikiana na wadau wengine  kama shirika la MDH katika kutokomeza ugonjwa  huo ambao unatajwa ni miongoni mwa  ugonjwa hatari unaoongoza kuuwa watu wengi Ulimwenguni.

Alisema, ugonjwa wa kifua kikuu unatibika kwa mtu  kupata tiba sahihi, na makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kupata ugonjwa huo ni pamoja  na wazee,watoto walio chini ya miaka mitano na watu wanaoishi kwenye mazingira yenye mwanga hafifu na hata hewa  mzito.

Kihongole alitaja kundi lingine ni watumiaji dawa za Hospitali kwa muda mrefu bila kufuata ushauri wa  kitaalam na wale wenye magonjwa sugu na utapia mlo kwa watoto wadogo.

Dkt Kihongole ameshauri wananchi kwenda kufanyiwa vipimo vya afya zao mara kwa mara badala ya kukimbilia kununua dawa na kumeza au kusubiri hadi pale hali inapokuwa mbaya kwani ni hatari kwa usalama wao.

Baadhi ya wakazi wa kijiji cha Amani kata ya Namasakata Halmashauri ya wilaya Tunduru mkoani Ruvuma,wakimsikiliza mratibu wa kifua kikuu na Ukoma wa Hospitali ya wilaya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole(hayupo pichani)wakati wa  zoezi la uchunguzi wa ugonjwa wa kifua kikuu kwa wakazi wa kijiji hicho,hata hivyo wazee hao wameiomba Serikali kukiongezea nguvu kitengo cha kkifua kikuu na Ukoma ili wataalam wake waweze kufika maeneo mengi kwa ajili ya uchunguzi wa ugonjwa huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...