NA YEREMIAS NGERANGERA, NAMTUMBO
Urani ni metali ya asili yenye kawaida ya kutoa mionzi ambapo imekuwepo ardhini tangu kuumbwa kwa dunia miaka bilioni tatu na nusu(3,500,000,000) iliyopita.

Upatikanaji wa urani ikiwa ardhini inaanza na tani mbili na kuendelea katika sehemu mbalimbali ikiwa ndani ya miamba , ndani ya maji ya ardhini na baharini

Serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na makampuni ya kigeni zilifanya utafiti wa madini katika ardhi ya wilaya ya Namtumbo mwaka 2006 na kugundua uwepo wa madini ya Urani katika mto mkuju kijiji cha Likuyusekamaganga.

Ugunduzi wa madini ulileta matumaini kwa wananchi wa wilaya ya Namtumbo licha ya kutolewa taarifa kuwa mionzi ya madini hayo ni hatari kwa afya ya binadamu .

Mionzi ya madini hayo zikiingia kwenye mwili wa binadamu hufanya kazi ya kuharibu mfumo wa ukuaji wa seli ,lakini wananchi Wilayani Namtumbo wanalalamikia kuchelewa kuanza kwa uchimbaji wa madini , wakiamini kuanza kwa uchimbaji wa madini hayo kutawanufaisha kiuchumi.

Uchimbaji wa madini ya urani yenye mionzi na hatari kwa afya za binadamu huchimbwa kwa njia ya shimo lililowazi au kwa njia ya kuingia ndani ya ardhi yaliko madini .

Licha ya madhara yanayoelezwa na wataalamu kuhusu madini ya urani wananchi Wilayani Namtumbo hususani vijana wanashauku kubwa ya kupata ajira ya kuchimba madini ya urani waweze kujipatia kipato.

Madini ya Urani katika mto mkuju yanapatikana karibu na uso wa dunia kiasi ambacho kitarahisisha uchimbaji wake na uchimbaji wa njia ya shimo lililowazi ndio utakaotumika.

Katika Madini ya Urani kuna mionzi hatari ya aina tatu, Alfa,Beta na mionzi aina ya Gamma kwa pamoja mionzi hiyo inamadhara kwa afya ya binadamu iingiapo mwilini .

Mionzi aina ya Alfa ina madhara mara ishirini zaidi ya madhara yanayoweza kutolewa na mionzi aina ya beta na gamma katika mwili wa binadamu wakati wa uchenjuaji .

Mionzi huingia katika mwili wa binadamu kwa njia ya hewa au kwa njia ya kumeza chembechembe za urani wakati wa uchenjuaji wa madini baada ya kuchimbwa kutoka ardhini.

Hamu ya wananchi wa Namtumbo hasa vijana ya kupata ajira ya kuchimba madini ya Urani licha ya madini hayo kuwa hatari kwa afya za binadamu zinaendelea kupotea baada ya kampuni iliyotegemewa kuanzisha kuchimba madini Mantra Tanzania Limited kutoonesha dalili za kutaka kuchimba madini hayo.

Wananchi katika wilaya ya Namtumbo kupitia vikao vya serikali hawajachoka kuhoji kuhusu ajira zinazosemwa kuwa kuanza kwa uchimbaji wa madini ya urani katika mto mkuju utasaidia vijana kupata ajira huku wakibaki bila majibu sahihi juu ya lini madini hayo yataanza kuchimbwa rasmi.

Afisa Mahusiano wa kampuni ya Mantra Tanzania Limited Adija Pallangyo anadai kampuni ya Mantra haijaanza uchimbaji wa madini kutokana na madini hayo kushuka bei katika soko la dunia kiasi ambacho kitaifanya kampuni kupata hasara endapo wataanza kuchimba madini kulingana na gharama za uendeshaji.

Kampuni ya mantra inakadiriwa kuwepo katika eneo la mto mkuju kwa zaidi ya miaka 12 hali inayopelekea wananchi kuhoji viongozi wa serikali Wilayani Namtumbo mara kwa mara uwepo wao katika eneo hilo huku hakuna shughuli za uchimbaji zinazoendelea.

Mbunge wa jimbo la Namtumbo Edwin Amandus Ngonyani pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Daniel Magnus Nyambo katika ziara zao za kuzungumza na wananchi Wilayani hukutana na swali mara kwa mara linalohusiana na lini madini ya urani katika mto mkuju yataanza kuchimbwa? Ambapo majibu yakiendelea ya kuwataka wananchi kuendelea kuvuta subira .

Bwana Ngonyani kupitia kikao cha kamati kuu ya chama cha mapinduzi mkoa wa Ruvuma amewafafanulia wajumbe wa kikao kuwa ajira asilimia 99.5 za vijana zinasubiriwa kupatikana katika uchimbaji wa madini ya urani huku makampuni ya uchimbaji wa madini hayo yakiendelea kusuasua katika uchimbaji na wananchi wameanza kupoteza matumaini juu ya uchimbaji wa madini hayo kutokana na kusubiri kwa muda mrefu.

Wananchi Wilayani Namtumbo matumaini yao kwa kampuni ya Mantra kuwa ingeanza kuchimba madini hayo kutokana na mwelekeo wake wa kushiriki kikamilifu kuwezesha shughuli za kijamii na ghafla kampuni hiyo inaonekana kuanza kutoweka taratibu kwenye kushiriki shughuli za kijamii na kupunguza wafanyakazi waliopo kwa kiasi kikubwa na kuleta sintofahamu kwa wananchi kuhoji kama uchimbaji wa madini hayo utafanyika .

Wapo wananchi Wilayani hapa wanabishana wao kwa wao wakihoji uhalali wa kampuni hiyo kukaa zaidi ya miaka 12 bila kufanya kazi ya uchimbaji lakini pia wanabiashana kuhusu aina ya kibali kinacho tolewa na wizara inayohusiana na madini ni cha utafiti au cha uchimbaji na kama ni cha utafiti ni kwa muda wote huo na kama cha uchimbaji mbona uchimbaji haufanyiki.na kuacha wananchi katika maswali magumu wakibishana wao kwa wao.

Eneo linalotumiwa na kampuni ya Mantra lipo katika Hifadhi ya misitu ya Undendeule (undendeule forest reserve) ambalo lina urani nyingi wananchi wanahoji kauli ya profesa Dos Santos Silayo katibu mkuu wakala wa misitu Tanzania aliyoitoa katika mkoa wa katavi kuwa hakuna uchimbaji wowote wa madini utakaofanyika katika Hifadhi bila kibali ,kampuni hiyo inawezaje kukaa katika Hifadhi bila kibali na wanahoji ni kibali gani cha utafiti au uchimbaji kinachotolewa kwa muda wa zaidi ya miaka 12 na uchimbaji usifanyike.

Barani afrika urani huzalishwa kwa asilimia 18 ya urani yote duniani na hatua ya uchimbaji na uchenjuaji wa urani Afrika ulianza mwaka 1952 Afrika kusini na mwaka 1976 nchini Namibia .

Nchi za Afrika ambazo zina kiasi kikubwa cha madini ya urani ni Algeria,Botswana,Jamhuri ya kidemokrasia ya kati , Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo ,Gabon,Guinea,Eguatorial guinea,Malawi na Mali.

Zingine ni nchi ya Mauritania ,Morocco,Namibia ,Niger ,Afrika kusini ,Tanzania ,Zambia pamoja na Zimbabwe

Nchini Tanzania madini ya urani yanapatikana Wilayani Namtumbo,Bahi,Galapo,Minjingu,Mbulu,Simanjiro,Ziwa Natron,Manyoni,Songea,Tunduru ,Madaba na Nachingwea

Katika wilaya ya Namtumbo madini ya urani yanapatikana katika kijiji cha Likuyuseka katika mto mkuju yenye jumla ya tani 58,500 ambayo inaizidi wilaya zingine kwa uwingi wa urani Nchini Tanzania.

Kitendawili cha uchimbaji wa madini ya Urani katika mto mkuju Wilayani Namtumbo kilianza kutolewa na waziri wa viwanda na biashara wa Urusi bwana Denis Manturov kwa kudai kuwa uchimbaji wa madini ya urani katika Mto mkuju utaanza mapema mwaka 2018 kupitia kampuni ya Russian”s Uranium one Inc ya nchini humo.

Katika eneo la mto mkuju kampuni ya Mantra Tanzania Limited ilionekana ndio kampuni yenye dhamira ya dhati ya kutaka kuanza uchimbaji wa madini hayo na kuwatumainisha wananchi katika kutegemea kupata ajira lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea na chakushangaza zaidi wafanyakazi wa kampuni hiyo imeanza kuwaondoa wafanyakazi wake katika eneo hilo na kuwafanya wananchi Wilayani Namtumbo kuanza kupotelewa na matumaini ya ajira kutokana na kuchimba madini hayo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...