Kivuko kipya cha MV.Ilemela 
kikielea majini mara baada ya kushushwa , kivuko hicho ambacho ujenzi 
wake umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.7 za Kitanzania kitakua 
kikitoa huduma kati ya Kayenze na Kisiwa cha Bezi na kina uwezo wa 
kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100.

Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi 
na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi na Mawasiliano) Mhe. Atashasta Nditiye
 katikati akiwa ameshikana mkono na Mkuu wa mkoa wa Mwanza John Mongella
 katika picha ya pamoja mara baada ya kumaliza zoezi za kushusha kivuko 
kipya cha Kayenze na kisiwa cha Bezi kilichogharimu shilingi bilioni 2.7
 ambacho kimepewa jina MV.Ilemela, tukio lililofanyika katika yadi ya 
Songoro Ilemela jijini Mwanza. Kushoto kwa Mongella ni Mbunge wa 
Iilemela Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi Mhe. Angelina Mabula na 
wa tatu kushoto ni Mtendaji Mkuu TEMESA Mhandisi Japhet Maselle. Kivuko 
cha MV.Ilemela kina uwezo wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani
 100.

Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi 
na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi na Mawasiliano) Mhe.  Atashasta 
Nditiye katikati akifurahia jambo na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi 
na Umeme (TEMESA) Mhandisi Japhet Maselle wa pili kushoto mara baada ya 
kumaliza zoezi la kukagua na kukishusha kwenye maji kivuko cha 
MV.Ilemela. Kivuko cha MV.Ilemela kina uwezo wa kubeba abiria 200 na 
magari 10 sawa na tani 100 na kimejengwa kwa gharama ya shilingi 
bilioni2.7.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi
 na Umeme (TEMESA) Mhandisi Japhet Maselle akisoma taarifa fupi ya mradi
 wa ujenzi wa kivuko cha MV.Ilemela wakati wa hafla ya kukishusha majini
 kivuko hicho iliyofanyika katika yadi ya Songoro iliyopo Ilemela jijini
 Mwanza. Kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza John Mongella na katikati ni 
Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi na 
Mawasiliano) Mhe.  Atashasta Nditiye. Kivuko cha MV.Ilemela kina uwezo 
wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100 na kimejengwa kwa 
gharama ya shilingi bilioni2.7.
…………………………………………………
NA ALFRED MGWENO (TEMESA MWANZA) 
Wakazi wa Ilemela mkoa wa Mwanza 
leo wameshuhudia kwa mara ya kwanza kivuko kipya cha Kayenze Bezi, 
MV.Ilemela ambacho kimegharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.7 
kikishushwa kwenye maji baada ya kukamilika kwa ujenzi wake. Tukio hilo 
limefanyika katika yadi ya Songoro iliyopo Wilaya ya Ilemela ambapo 
mgeni rasmi alikua Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano 
(Sekta ya Uchukuzi na Mawasiliano) Mhe. Atashasta J. Nditiye (MB).
Akizungumza katika tukio hilo 
Mhe. Nditiye alimshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na serikali ya awamu ya tano kwa 
kuendelea kutimiza ahadi ya miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini.
‘’Hadi sasa Mheshimiwa Rais 
tayari ameshatoa fedha zote kiasi cha shilingi za Kitanzania bilioni 
9,953,916,200 iliyokuwa imepangwa kwenye bajeti ya miradi ya maendeleo 
ya vivuko kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020’’, alisema Mhe. Naibu Waziri 
ambapo aliongeza kuwa kivuko cha MV.Ilemela kitakapoanza kutoa huduma 
kitaondoa changamoto ya usafiri kwa wananchi kati ya Kayenze na kisiwa 
cha Bezi. 
‘’Kivuko hiki kitakapoanza kutoa 
huduma ni dhahiri kuwa kitaondoa changamoto ya usafiri kwa wananchi kati
 ya Kayenze na kisiwa cha Bezi hivyo kitainua maisha ya wananchi wa 
maeneo hayo kibiashara, kiuchumi na kijamii, mara tu mtakapokamilisha 
majaribio anzeni kutoa huduma ’’. Aliongeza Naibu Waziri ambapo pia 
alitoa wito kwa watumishi wa TEMESA kufanya kazi kwa weledi na 
kuhakikisha kivuko hicho pamoja na vivuko vingine vinatunzwa vizuri na 
vinadumu kwa muda mrefu huku wakizingatia usalama wa abiria na mali zao.
Awali, Mtendaji Mkuu wa 
Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mhandisi Japhet Y. Maselle, akisoma 
taarifa kwa mgeni rasmi katika tukio hilo alisema serikali kupitia 
TEMESA inaendelea na ujenzi wa vivuko vingine vipya kwa ajili ya Mafia 
Nyamisati kwa gharama ya shilingi bilioni 5.3, Bugorola Ukara kwa 
gharama ya shilingi bilioni 4.2 pamoja na Chato Nkome kwa gharama ya 
shilingi bilioni 3.1. 
‘’Vivuko hivi vyote vinagharimu 
jumla ya shilingi za Kitanzania bilioni 15.3 na fedha zote hizi 
zinatolewa na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania’’, alisema 
Mhandisi Maselle ambapo aliishukuru serikali ya awamu ya tano 
inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa fedha
 zote zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya ununuzi wa vivuko, 
ukarabati na ujenzi wa maegesho ya vivuko, ambapo alisema Fedha hizo 
zimewezesha miradi hiyo kuanza na mingine kuwepo katika hatua mbalimbali
 za utekelezaji.
Naye Mbunge wa Ilemela Mhe. Naibu
 Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angelina Mabula 
akizungumza katika tukio hilo aliishukuru serikali kwa kuweza kutimiza 
ahadi iliyoitoa. ‘’Nimshukuru Mhe. Rais niwashukuru TEMESA kwa kazi 
kubwa na nzuri ambayo imefanyika, tunao uhakika sasa kwamba adha ya 
usafiri katika eneo la visiwa vya Kayenze Bezi sasa litakua ni 
historia’’, alisema Dkt. Mabula.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John
 Mongella alimuomba Mhe. Nditiye kufikisha salamu za shukrani kwa Rais 
kwa mambo makubwa anayoufanyia mkoa wa Mwanza hasa kwenye sekta ya 
usafiri wa majini ambapo alisema watu wa mkoa huo wanategemea mwezi wa 
pili kuona vivuko  vingine vikiingia ziwani tayari kuanza kutoa huduma 
kwa wananchi.
Kivuko cha MV.Ilemela kina uwezo 
wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100. Hadi sasa Wakala 
unaendesha na kusimamia vivuko 30 katika vituo (Ferry stations) 20 
Tanzania Bara na hivyo kukamilika kwa kivuko cha MV. Ilemela kutafanya 
idadi ya vivuko kufikia 31 na vituo kuwa 21.


 

Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...