Na Woinde Shizza , Arumeru
MAAFISA wawezeshaji wa TASAF Halmashauri ya Wilaya ya Meru watakiwa kuwa waadilifu wakati wa zoezi la uhakiki wa Kaya za Wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF) katika utekelezaji wa kipindi cha pili cha awamu ya tatu ya TASAF.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru Emmanuel J. Mkongo wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo na Wawezeshaji wa TASAF juu ya utekelezaji wa Kipindi cha Pili cha Awamu ya Tatu ya TASAF .
Mkongo aliwataka wawezeshaji hao kuwa makini wakati wa mafunzo ili kufanikisha zoezi la uhakiki wa kaya za walengwa wa TASAF na kuondoa dhana iliyojengeka kwa jamii ya kuwepo Walengwa hewa.
Aidha, Mkurugenzi Mkongo aliwataka wawezeshaji hao ambao ni watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru kuwa waaminifu na waadilifu wakati wa zoezi hilo.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa TASAF Tatu Mwaruka wakati wa hotuba ya ufunguzi, amesema tathimini ya utekelezaji wa kipindi cha kwanza cha awamu ya tatu ya TASAF imeonyesha kuwa mpango huo umechangia kufikiwa kwa azma ya Serikali ya kupunguza umaskini nchini ambapo umaskini wa mahitaji ya msingi kwa kaya umepungua kwa asilimia 10. Pia umaskini uliokithiri umepungua kwa asilimia 12 kwa kaya Maskini sana nchini.
Tatu alieleza kuwa Serikali iliamua kuendelea na kipindi cha pili katika awamu ya tatu ya TASAF ili kaya zote zinazoishi katika mazingira duni zipate usaidizi kwani katika kipindi cha kwanza cha TASAF awamu ya tatu, idadi ya kaya zilizofikiwa ni sawa na 70 % ya Kaya zenye mazingira duni nchini.
Hivyo, kipindi cha pili cha TASAF awamu ya tatu kitatekelezwa katika Halmashauri zote 185 Tanzania Bara na Wilaya zote za Zanzibar ambapo jumla ya kaya milioni moja laki nne na nusu zenye jumla ya watu zaidi ya milioni 7 kote Nchini zitafikiwa ikiwa ni ongezeko la kaya laki tatu na nusu.
Mwakilishi huyo wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF amewatahadharisha wawezeshaji watakao fanya kazi ya uhakiki kuwa waadilifu kwani watawajibishwa endapo itabainika uwepo wa Kaya zisizo na sifa katika eneo walilofanya kazi.
Semina hiyo ya kuwajengea uwezo Wawezeshaji wa Halmashauri hiyo inafanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe Julai 13 hadi 14.
Aidha zoezi la kuhakiki Kaya za wanufaika wa TASAF litaanza tarehe 15 hadi 17 Julai 2020.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...