Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya akisalimiana na wajumbe wa kamati ya utendaji ya MVIWATA mkoa wa Dodoma leo alipowasili kwa ajili ya ufunguzi wa mkutano wa mwaka wa mtandao huo jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya ( kushoto) akisikiliza maelezo ya Mwenyekiti wa MVIWATA mkoa wa Dodoma Bw. Said Matonya ( aliyesimama) leo wakati wa mkutano mkuu wa mwaka jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya (katikati) akizungumzaa na wanachama wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) leo alipofungua mkutano mkuu wa mwaka jijini Dodoma. Kushoto ni Bw. Jeremia Maina mlezi wa MVIWATA Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya akiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wa MVIWATA toka wilaya ya Kongwa mara baada ya kufungua mkutano mkuu wa mwaka wa mkoa wa Dodoma leo.

KATIBU Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya ameuagiza uongozi wa Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) kutatua changamoto za upatikanaji wa pembejeo, mbegu bora na mikopo kwa wanachama wake husasan walioko vijijini kwa kushirikiana na wizara.

Akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano mkuu wa MVIWATA Mkoa wa Dodoma leo  (08.12.2020) Kusaya amesema hafurahishwi kusikia malalamiko ya wakulima wadogo kukosa mbolea na mbegu bora au kusikia wakiuziwa kwa bei ghali wakati umoja wao upo.

“MVIWATA tumieni umoja wenu kuagiza mbolea kwa mfumo wa pamoja kupitia Wakala wa mbolea (TFRA) ambapo mtanunua kwa bei nafuu na kusambaza kwa wana chama wenu vijijini. Wizara ipo na itasimamia kwa karibu ili kuleta unafuu kwa wakulima “ alisema Kusaya

 Kusaya aliongeza kusema mtandao huo una jukumu pia la kutafuta mbegu bora za gharama nafuu za mazao ya mahindi ,alizeti ,mpunga na mengine kwa kuwasilisha mahitaji yao kwenye Wakala wa Mbegu wa Serikali (ASA).

Aidha wakulima hao katika risala  iliyosomwa na mwenyekiti wa mtandao huo mkoa wa Dodoma Said Matonya waliiomba serikali kupitia wizara ya kilimo kusaidia upatikanaji wa mbegu za mazao ya chakula na biashara mapema kabla ya msimu kuisha na mbegu hizo ziuzwe kwa gharama nafuu.

Matonya alitaja mbegu za mahindi mfuko wa kilo mbili zinauzwa vijijini kwa gharama ya kati ya Shilingi 10,000 hadi 12,000 hatua ambayo inakwamisha wakulima wadogo kununua hivyo kujikuta wakipanda mbegu za asili na zisizo na ubora.

“Wakulima tunakabiliwa na ukosefu wa pembejeo, mbegu bora, mafunzo na mikopo kutokana na kuwa za gharama kubwa, hivyo serikali itusaidie tupate huduma hizi kwa gharama nafuu” alisema Matonya .

Akijibu hoja hiyo Kusaya alisema serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli  inawathamini wakulima ndio maana hatua mbalimbali ikiwemo Wakala wa Mbegu (ASA) na Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea wameelekezwa kufikisha huduma zao vijijini kwa bei elekezi ya serikali.

“Uwepo wangu hapa leo ni uthibitisho kuwa serikali inawathamini na kuwajali wakulima wadogo nchini. Naagiza tena Wakala wa Mbegu nchini (ASA) ahakikishe mbegu bora za mahindi zinafika Dodoma na mikoa mingine yote na kuuzwa si zaidi ya Shilingi 6,000 kwa mfuko wa kilo mbili” aliagiza Kusaya.

Katika hatua nyingine Kusaya ametoa wito kwa MVIWATA kutumia uwepo wa vyuo 14 vya mafunzo ya kilimo vya serikali (MATI) na vituo 4 vya mafunzo ya wakulima nchini kupeleka wakulima  na wanafunzi (vijana) kujifunza mbinu za kisasa ili wafanye kilimo biashara na cha kisayansi.

Alitaji kituo cha wakulima wadogo Bihawana kilichopo Dodoma kama sehemu muhimu ambapo MVIWATA wanaweza kutumia kufundisha wanachama wake namna ya kuongeza tija na ujuzi wa kuendesha kilimo biashara.

Kusaya aliwashauri na kuwasisitiza wakulima kupitia MVIWATA kutumia uwepo wa Mfuko wa Pembejeo (AGITF) unaosimamiwa na Wizara ya Kilimo kwani utawezesha kupata zana bora za kilimo kama trekta, powertiller, na pembejeo kwa riba nafuu.

“ Mfuko wa pembejeo ni maalum kwa ajili ya kukopesha wakulima na riba zake ni nafuu kwani kikundi hukopeshwa kwa riba ya asilimia 6 na mkulima binafsi hukopeshwa kwa asilimia 7 na kufanya marejesho kwa muda wa miezi 72” alisisitiza Kusaya.

Mkutano huo wa mwaka wa wanachama wa Mtandao wa Wakulima Tanzania (MVIWATA) mkoa wa Dodoma umehudhuriwa na wakulima 100 kati ya 800 kutoka wilaya za Dodoma Mjini, Chamwino, Kongwa, Mpwapwa ,Bahi na Kondoa ambapo pia utafanya uchaguzi mkuu .

Mkutano huo unafanyika ukiwa na kauli mbiu isemayo “MVIWATA Sauti ya Mkulima, Mtetezi wa Mkulima ni Mkulima Mwenyewe”.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...