

KAMATI ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiagiza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kuhakikisha inakiwezesha Chuo cha Mabaharia cha Dar es Salaam (DMI), kununua meli ya mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi wanaosoma katika chuo hicho.
Hatua hiyo itakiwezesha chuo hicho kufanyakazi kazi zake kwa ufanisi na hivyo kutoa wahitimu wengi watakaokidhi soko la ajira la ndani na kimataifa.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Suleiman
Kakoso, amesema kwa kuwa Chuo hicho kwa sasa kinahudumia wanafunzi kutoka nchi
mbalimbali kama vile Uganda, Kenya, Rwanda na Zimbabwe kwa hiyo kikiwezeshwa kuwa
na meli ya mafunzo kitapelekea wanafunzi wake kuwa na ujuzi wa kutosha wa
mafunzo kwa vitendo na hivyo
kitafanikiwa kupata wanafunzi wengi kutoka nchi nyingine barani Afrika.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo hicho Dkt. Erick Masami, akiwasilisha taarifa ya Chuo hicho mbele ya kamati hiyo amesema Chuo hicho bado kinakabiliwa na upungufu wa majengo ya madarasa na ofisi.
Mjumbe wa kamati hiyo Mhe. Mwanaisha Lulenge amezungumzia umuhimu wa Taifa kuwekeza katika masomo ya ubaharia kwani wataalam wa fani hiyo hapa nchini bado ni wachache.
Naye, Naibu wa Waziri wa Ujenzi na
Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya amesema Wizara imeyapokea na itayafanyia kazi
mapendekezo yote ya Kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu ili kukiwezesha
chuo cha mabaharia nchini kuwa kituo cha mafunzo cha umahiri katika ukanda wa
Afrika Mashariki na Kati.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...