NA YEREMIAS NGERANGERA….NAMTUMBO.
Baraza la wafanyakazi katika Halmashauri ya wilaya Namtumbo mkoani Ruvuma limepitisha mapendekezo ya bajeti ya Halmashauri kwa mwaka wa fedha 2021/2022 ikikisiwa kukusanya na kupokea jumla ya Tsh .28,337,660,400 kutoka vyanzo vya ndani,ruzuku kutoka serikali kuu na michango kutoka kwa wadau wa maendeleo.
Akisoma bajeti hiyo afisa mipango wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo bwana Amos Kanige alisema Halmashauri inakisia kukusanya kiasi cha Tsh 1,588,000,000 kutoka mapato ya ndani na inakisia kupokea Tsh 22,871,067,500 kutoka serikali kuu na Tsh.3,778,592,900 kama ruzuku kutoka kwa wahisani.
Kanige alifafanua matumizi ya bajeti hiyo kuwa Tsh 18,043,444,000 itatumika katika mishahara ,Tsh 2,858,693,000 kwa ajili matumizi mengineyo na Tsh 7,337,660,400 kwa ajili ya matumizi ya miradi ya maendeleo.
Hata hivyo bwana Kanige alisema katika mpango wa mapendekezo ya bajeti kwa mwaka 2021/2022 Halmashauri imezingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyowekwa na serikali katika kuandaa bajeti hiyo na ushirikishwaji wa wananchi katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.
Kupitia bajeti hiyo Kanige alisema kutakuwa na uboreshaji wa huduma za elimu kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha sita, uboeshaji wa huduma za afya kwa kuimarisha huduma za tiba na kinga ,kuimarisha vyanzo vya mapato ya ndani kwa kununua mashine 10 ya kukusanyia mapato,kuboresha stendi ya mabasi Namtumbo,kununua na kusambaza mbegu ya ufuta na kuendeleza ujenzi wa soko la kisasa Namtumbo.
Aidha katika bajeti hiyo hiyo kutakuwa na uimarishaji wa huduma za kilimo na mifugo kwa kutoa huduma za ugani katika kata 21,ukarabati wa skimu za umwagiliaji na kujenga skimu 2 mpya ,ukarabati wa machinjio moja,kufanya mpango wa matumizi bora ya ardhi , kuanzisha mnada wa mifugo pamoja na utoaji wa mikopo kwa vikundi 65 vya wanawake,vijana na watu wenye ulemavu ikiambatana na utoaji wa ruzuku ya fedha kwa kaya 4637 katika vijiji 42.
Katibu wa chama cha walimu wilayani Namtumbo Mtamila Achikuo pamoja na kupongeza mapendekezo ya bajeti alidai amefurahishwa na kuingizwa katika bajeti kikao cha baraza la wafanyakazi tofauti na bajeti zilizopita ambazo zilisababisha malalamiko ya wajumbe wa kikao kutolipwa stahiki zao kwa wakati walipokuwa wakihudhuria vikao vya baraza la wafanyakazi ambalo lipo kwa mujibu wa sheria.
Kwa mujibu wa Mwekahazina
wa Halmashauri ya wilaya Namtumbo
Pendo Nyomeye alisema mpaka kufika juni 30,2020 mapato halisi yaliyokusanywa ni Tsh 22,302,818,436.19 sawa na asilimia
91.79 ya fedha iliyoidhinishwa huku makusanyo ya mapato ya ndani yalikuwa
1,694,578,977.53 sawa na asilimia 119.6 ya lengo la mwaka ,mishahara Tsh 16,434,760,623,23.matumizi mengineyo Tsh
1,313,064,100 na Tsh 2,860,414,735.40. kwa ajili ya maendeleo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...